OCHA:#ItTakesAVillage ni kampeni ya Siku ya Msaada wa Kibinadamu
Na Angella Rwezaula – Vatican.
Umoja wa Mataifa kupitia ofisi yake ya kuratibu misaada ya dharura, OCHA katika kuelekea siku ya kimataifa ya Msaada wa kibinadamu mwaka 2022 ifanyikayo kila tarehe 19 Agosti imesema kuwa ‘inahitaji juhudi za watoa misaada ya kibinadamu ili kusaidia jamii inayokabiliwa na majanga. Kwa mfano nchini Uganda, huko Afrika Mashariki linalopokea wakimbizi, misaada hutoka si tu kwa mashirika ya kimataifa kama yale ya Umoja wa Mataifa bali pia watu binafsi. Kwa maana hiyo wakimbizi kutoka Congo DRC, na wakimbizi kutoka Sudan Kusini wameweza kusaidiwa iwe nchini Uganda, lakini hata Waganda wamesaidiwa nchini Tanzania na wenyeji. Watu ni wengi duniani ambao wanasaidiwa kwa namna moja au nyingine na watu mahalia bila kusubiri mashirika ya kimataifa.
Katika wiki moja OCHA imeendesha kampeni iitwayo, #ItTakesAVillage ambayo kila mtu anaweza kushiriki kwenye mtandao wa kijamii na kutoa maoni, kuchapisha au kushirikisha wengine kama njia ya kuonesha mshikamano na watu wanaohitaij msaada na shukrani kwa wale wanaoweka rehani maisha yao kusaidia wengine.
Mnamo 19 Agosti 2003, kulitokea shambulio katika Hoteli ya Canal huko Baghdad, Iraq, ambayo iliua wafanyakazi na wahudumu 22 wa utoaji misaada, akiwemo Mwakilishi Maalum wa Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa nchini Iraq, Bwana Sergio Vieira de Mello. Miaka mitano baadaye, mwaka 2009, Baraza Kuu lilipitisha azimio A/RES/63/139 linaloitaja kuwa 19 Agosti iwe Siku ya watoa Misaada ya Kibinadamu Duniani. Hii ni fursa ya kusherehekea wafanyakazi wa utoaji misaada ya kibinadamu duniani kote, lakini pia wale ambao wamepoteza maisha yao huku wakisaidia maskini zaidi, watu waliotengwa na wanaoishi katika mazingira magumu. Kila mwaka, Siku ya Kutoa msaada wa Kibinadamu Duniani huzingatia mada, inayoleta pamoja washirika kutoka katika mfumo wa kibinadamu ili kutetea uhai, ustawi na utu wa watu walioathiriwa na migogoro na usalama wa wafanyakazi wa kibinadamu. Mwaka huu 2022, madhumuni ya Siku hii yanayomulika wale wote watoao misaada kwenye maeneo yao bila kusubiri nani aanze au mashirika.