Papa Francisko:Kardinali Fernandez,alikuwa mwaminifu na shuhuda wa Kanisa la Malaysia
Sr. Angela Rwezaula – Vatican.
Katika salam zake za rambi rambi kufuatia na kifo cha Kardinali Soter kilichotokea, tarehe 28 Oktoba 2020, Papa Francisko amezielekeza kwa Askofu Mkuu Julian Leow Beng Kim, wa Jimbo Kuu Katoliki la Kuala Lumpur, kwamba “baada ya kupata taarifa za huzuni kwa kifo cha Kardinali Anthony Soter Fernandez, ninakupa pole nyingi kwako wewe, makuhani, watawa na walei wa Jimbo kuu la Kuala Lumpur".
Papa Francisko akiendelea na salam hizo anasema "Kwa shukrani ya ushuhuda mwaminifu wa Kardinali Fernandez kwa Injili, huduma yake ya ukarimu kwa Kanisa huko Malaysia na kujitoa kwake kwa muda mrefu katika kukuza utengamano na mazungumzo ya kidini, ninaungana nanyi kwa moyo wote kumuombea ili apate pumziko lake milele". Papa Francisko aidha katika ujumbe huo amesema “ na kwa wote ambao wanaomboleza kutokana na kifo cha marehemu Kardinali katika tumaini la kweli la Ufufuko ninawatumia Baraka yangu ya Kitume kama ahadi ya kutoa faraja na amani katika Yesu Kristo Mwokozi wetu”, mehitimisha.
Misa ya mazishi ya Kardinali itaadhimishwa Jumamosi tarehe 31 Oktoba saa 4.30 asubuhi majira ya huko katika Kanisa Kuu katoliki la Kuala Lampur ambapo tangu leo hii kwa siku nzima hadi Jumamosi mwili wake utakuwa kanisani kwa ajili ya kutoa buriani.