Papa Fracisko ashauri kutazama Maria na kusali Rosari mwezi Mei!
Na Sr. Angela Rwezaula - Vatican
Jana ilikuwa ni Siku ya Kimataifa ya Umoja wa Mataifa ya kukomesha Malaria. Tukiwa katika harakati za mapambano ya janga la virusi vya corona, tupeleke mbele hata jitihada kuzuia na kutibu Malaria, ambayo ni tishio la mabilioni ya watu katika nchi nyingi. Ndiyo mwanzo wa maneno yake Papa Francisko mara baada ya tafakari na sala ya Malkia wa mbingu, Dominika ya III ya Pasaka tarehe 26 Aprili 2020 katika ukumbi wa Maktaba ya Kitume mjini Vatican, kwa wakati huu wa vizuizi vya mikusanyiko katika mapambano ya virusi vya corona. Papa Francisko aidha ameonyesha ukaribu wake kwa wagonjwa wote, wale wote ambao wanawatibu na wale ambao wanafanya kazi ili kila mmoja aweze kupata huduma msingi ya kiafya.
Wiki kitaifa ya kusoma maandiko matakatifu Poland
Papa Francisko amewakumbuka na kuwasalimia wote ambao leo hii nchini Poland wanashiriki toleo Kitaifa la "usomaji wa Maandiko matakatifu". Ameongeza kusema kuwa yeye mara nyingi amekwisha wambia na sasa kwa kurudia kwa upya kuwa ni jinsi gani ilivyo muhimu kuwa na tabia ya kujisomea Injili, hata kwa dakika chache kila siku. “Tubebe Biblia katika mifuko na katika mikoba. Biblia iwe karibu nasi, hata kimwili na kuisoma kidogo kila siku”. Amesisitiza Papa Francisko.
Mwezi Mei ni wa Rosari
Muda mfupi tutaanza mwezi Mei ambao kwa namna ya pekee ni wa Bikira Maria amesema Papa na kwamba kwa barua fupi,iliyotangazwa tarehe 25 Aprili, Papa Francisko amethibitisha kuwa amewaalika waamini wote katika mwezi Mei kusali Rosari kwa pamoja katika familia au binafsi, pamoja na sala mbili ambazo amezielekeza. https://www.vaticannews.va/sw/pope/news/2020-04/barua-baba-mtakatifu-francisko-waamini-wote-duniani-rozari-2020.html Na kwa kuhitimisha amesema kuwa “ Mama yetu atatusaidia kukabiliana kwa imani na matumaini kipindi hiki cha majaribu ambacho tunakipitia. Amewatakia mwezi mwema wa Mei na Dominika njema lakini pia wasisahau kusali kwa ajili yake