Tafuta

2021.01.18 : Askofu Mkuu Mwandamizi Abel Gabuza wa Jimbo Kuu Durban Afrika Kusini ameaga dunia Jumapili  17 Januari 2021 2021.01.18 : Askofu Mkuu Mwandamizi Abel Gabuza wa Jimbo Kuu Durban Afrika Kusini ameaga dunia Jumapili 17 Januari 2021  

Afrika kusini yaomboleza kifo cha Askofu Mkuu Gabuza

Bado Kanisa Barani Afrika linapoteza mfuasi wa Kristo.Askofu Mkuu Mwandamizi Abel Gabuza wa jimbo Kuu katoliki Durbun ameaga dunia Jumapili asubuhi baada ya kuambukizwa na COVID-19.

Na Sr. Angela Rwezaula -Vatican.

Kwa mara nyingine tena katika muda mfupi tu, Kanisa barani afrika linampoteza mchungaji wake kwa mujibu wa Kardinali Wilfrid Fox Napier OFM, Askofu Mkuu wa  Jimbo Kuu Katoliki Durban, Afrika Kusini, kuwa mwandamizi wake amefariki Askofu Mkuu Abel Gabuza siku ya Jumapili tarehe 17 Januari 2021. Kardinali Napier ametangaza kifo hicho kwa uchungu mkubwa ya kuwa mauti ya askofu Mkuu mwandamizi yalimfikia akiwa amelazwa Hospitali ya Hillcrest saa 5.45 asubuhi.

“Askofu Mkuu amekuwa pamoja nasi huko Durban kwa muda mfupi, pungufu  ya miaka miwili tu, lakini wakati huo huo tumekuja kumtambua kama mchungaji mpole, anayejali na mwenye moyo wa uchangamfu. Kupitia upole wake, kujali na mchangamfu, ameweza kutengeneza kwa haraka urafiki kwa kila mtu ambaye alikuwa na bahati ya kufanya urafiki naye. Hiyo ni sababu ambayo inaonesha kwamba kuondoka kwake ni hasara kubwa sana kwetu na kwa Kanisa lote Afrika Kusini”, amesema Kardinali Napier.

Katika tweet iliyochapishwa mnamo tarehe 10 Januari 2021, Kardinali Napier aliwaomba waamini kuwa na mshikamano wa kiroho na Askofu Mkuu Abel Gabuza. Wakati huo huo ilisemekana kuwa alikuwa katika Kitengo cha Wagonjwa Mahututi (ICU) kutokana na aina ya pili mpya ya COVID-19. “Tafadhali muombee Askofu Mkuu wa  Mwandamizi wa Durban, Abel Gabuza, ambaye amepima na kukutwa na virusi vya corona , COVID-19 na yuko ICU,” Kardinali Napier aliandika. Kama mwandamizi Askofu Mkuu Gabuza, ilitabiriwa kuwa  angemrithi Kardinali Napier kama Askofu Mkuu wa Durban. Kardinali ambaye amekuwa Askofu Mkuu wa Durban tangu 1992 alichaguliwa kuwa katika Baraza la Makardinali mnamo 2001, aliwasilisha kujiuzulu kwake mnamo 2016 katika siku ya miaka 75 ya kuzaliwa, kulingana na vifungu vya Sheria ya Kanisa ya Kanoni. Lakini Papa Francisko, hata hivyo, alimwomba Kardinali Napier kuendelea kukaa kwa muda kama Kawaida ya Jimbo kuu.

Askofu Mkuu Gabuza alizaliwa tarehe 23 Machi 1955. Baba Mtakatifu Francisko tarehe 9 Desemba 2018, alimteua kuwa Askofu Mkuu mwandamizi wa Jimbo kuu la Durban, hadi wakati huo alikuwa Askofu wa Jimbo la Kimberley nchini Afrika Kusini, Askofu Mkuu Gabuza alikulia katika mji wa Alexandra, wakati wa siku ngumu za ubaguzi wa rangi. Alikuwa akikumbuka changamoto za kukua katika mji huo. Mama yake alimpeleka katika shule ya bweni, ikiwa kama njia ya kumlinda Gabuza akiwa kijana. Baba yake alikufa akiwa bado kijana. Askofu mkuu Gabuza kila wakati alimpa mama yake sifa kama mmoja wa wale ambao walitengeneza wito wake na mtazamo wa maisha. Alipewa daraja la ukuhani  katika Jimbo kuu la Pretoria mnamo tarehe 15 Desemba 1984.

Wakati wake kama Askofu, alikuwa ni mwenyekiti wa Tume ya Haki na Amani ya Baraza la Maaskofu Katoliki Kusini mwa Afrika, ambapo Askofu Mkuu Gabuza aliendeleza sifa yake kama Askofu aliyekuwa wazi, anayeheshimiwa na hata aliye kuwa wazi kukemea  masuala ya ufisadi na ukosefu wa usawa kijamii. Wakati wa kuteuliwa kwake kama Askofu Mkuu mwandamizi wa Durban, Askofu Mkuu Gabuza ameweza kuzungumzia wasiwasi wake juu ya kuhama kutoka Jimbo la Kimberley vijijini kwenda Jimbo kuu mji  Durban.

18 January 2021, 10:06