Tafuta

Siku ya Afya ya Akili Duniani huadhimishwa na Jumuiya ya Kimataifa kila mwaka ifikapo tarehe 10 Oktoba! Siku ya Afya ya Akili Duniani huadhimishwa na Jumuiya ya Kimataifa kila mwaka ifikapo tarehe 10 Oktoba!  (AFP or licensors)

Siku ya Afya ya Akili Duniani Tarehe 10 Oktoba 2023

Maadhimisho ya Siku ya Afya ya Akili Duniani kwa Mwaka 2023 inayonogeshwa na kauli mbiu “Afya ya akili ni haki ya binadamu kwa wote" lengo ni kuboresha ujuzi, kuongeza ufahamu na kuendesha vitendo vinavyokuza na kulinda afya ya akili ya kila mtu kama haki msingi ya binadamu ulimwengu wote. Ikumbukwe kwamba, Afya ya akili ni haki ya msingi kwa watu wote. Kila mtu, yeyote yule na popote alipo, ana haki ya kufikia kiwango cha juu zaidi cha afya ya akili.

Na Padre Richard A. Mjigwa, C.PP.S. – Vatican.

Siku ya Afya ya Akili Duniani huadhimishwa na Jumuiya ya Kimataifa kila mwaka ifikapo tarehe 10 Oktoba kwa lengo la kuongeza uelewa wa matatizo ya afya ya akili duniani kote na kuhamasisha jitihada za kusaidia afya ya akili. Siku hii iliadhimishwa kwa mara ya kwanza tarehe 10 Oktoba 1992, kwa ushirikiano na Shirikisho la Afya ya Akili Duniani “World Federation of Mental Health” pamoja na kuungwa mkono na Shirika la Afya Duniani (WHO). Siku hii inatoa fursa kwa wale wote wanaohusika katika ngazi mbalimbali katika nyanja ya afya ya akili kuchunguza na kubadilishana uzoefu, mang’amuzi ya masuala muhimu na mapendekezo, ili kuchangia katika kufanya huduma kwa watu wenye matatizo ya akili kuwa halisi, inayopatikana, huduma inayojumuisha pamoja na kuleta ufanisi bora duniani kote. "Akili zetu, haki zetu.” Maadhimisho ya Siku ya Afya ya Akili Duniani kwa Mwaka 2023 inayonogeshwa na kauli mbiu “Afya ya akili ni haki ya binadamu kwa wote" lengo ni kuboresha ujuzi, kuongeza ufahamu na kuendesha vitendo vinavyokuza na kulinda afya ya akili ya kila mtu kama haki msingi ya binadamu ulimwengu wote. Ikumbukwe kwamba, Afya ya akili ni haki ya msingi kwa watu wote. Kila mtu, yeyote yule na popote alipo, ana haki ya kufikia kiwango cha juu zaidi cha afya ya akili. Hii ni pamoja na haki ya kulindwa kutokana na hatari za afya ya akili, haki ya kupatikana, kufikiwa, kukubalika, na matunzo bora, na haki ya uhuru, uhuru na ushirikishwaji katika jamii. Afya bora ya akili ni muhimu kwa afya na ustawi wa jamii kwa ujumla. Bado mtu mmoja kati ya wanane duniani kote anaishi na hali ya afya ya akili, ambayo inaweza kuathiri afya yao ya kimwili, ustawi wao, jinsi wanavyoungana na wengine, na maisha yao. Hali ya afya ya akili ni changamoto kubwa miongoni mwa vijana wa kizazi kipya.

Siku ya Afya ya Akili Duniani kwa Mwaka 2023
Siku ya Afya ya Akili Duniani kwa Mwaka 2023

Kuwa na mgogoro katika hali ya afya ya akili kamwe kusiwe sababu ya kumnyima mtu haki zake za kibinadamu au kuwatenga na maamuzi kuhusu afya yake. Hata hivyo duniani kote, watu walio na mmgogoro wa hali ya afya ya akili wanaendelea kukumbwa na ukiukwaji mbalimbali wa haki za binadamu. Wengi wametengwa na maisha ya jamii na kubaguliwa, wakati wengi zaidi hawawezi kupata huduma ya afya ya akili wanayohitaji au wanaweza tu kupata huduma ambayo inakiuka haki zao za kibinadamu. Shirika la Afya Duniani, WHO, linaendelea kushirikiana na wadau wake ili kuhakikisha afya ya akili inathaminiwa, inakuzwa, na kulindwa, na kwamba hatua za haraka zinachukuliwa ili kila mtu atumie haki zake za kibinadamu na kupata huduma bora ya afya ya akili anayohitaji. Jiunge na kampeni ya Siku ya Afya ya Akili Duniani 2023 ili kujifunza zaidi kuhusu haki yako ya msingi ya afya ya akili na pia jinsi ya kulinda haki za wengine. Unyanyapaa na ubaguzi vinaendelea kuwa kikwazo kwa ushirikishwaji wa kijamii na upatikanaji wa huduma na matunzo ya kutosha; “Sote tunaweza kufanya sehemu yetu katika kuongeza ufahamu kuhusu ni hatua zipi za kuzuia afya ya akili zinafaa, na Siku ya Afya ya Akili Duniani ni fursa ya kufanya hivi kwa pamoja. Tunafikiria ulimwengu ambapo afya ya akili inathaminiwa, kukuzwa na kulindwa; ambapo kila mtu ana fursa sawa za kufurahia afya ya akili na kutumia haki zake za kibinadamu; na ambapo kila mtu anaweza kupata huduma ya afya ya akili anayohitaji.” Linabainisha Shirikisho la Afya ya Akili Duniani.

Wagonjwa wa Afya ya Akili wanaishi katika mazingira hatarishi
Wagonjwa wa Afya ya Akili wanaishi katika mazingira hatarishi

Dalili za matatizo na changamoto ya afya ya akili ni pamoja na: Kuwa na hasira kupindukia. Kukosa furaha na kutokuona thamani katika maisha, hali inayopelekea mtu kuwa na upweke hasi. Kuwa na wasiwasi wa kupindukia, kiasi hata cha kujaribu kutema zawadi ya maisha. Hali ya kukosa usingizi. Kuwa na msongo mkali wa mawazo kiasi hata cha kushindwa kufanya maamuzi. Ni muhimu kwa jamii kufanya utafiti wa kutosha ili kuzuia magonjwa ya akili: kama watu binafsi na kama jamii na kama Jumuiya ya Kimataifa. Jamii, familia na watu binafsi wajitahidi kuwa karibu zaidi na watu wenye dalili za afya mbaya ya akili, ili kujaribu kuokoa maisha yao. Wajitahidi kuzungumza nao kuhusu hisia na changamoto wanazopitia pamoja na kumjulia hali mara kwa mara. Kama kuna dalili za hatari jamii inashauriwa kuwasiliana na kitengo cha dharura kilichoko karibu naye. Ili kulinda afya ya akili na mwili kwa ujumla. Watu wanashauriwa wasivute sigara, wahakikishe kwamba, wanapata nafasi ya kulala vyema, wapende na kuthamini sana kinga, kuliko falsafa ya kuponya magonjwa. Watu wajenge utamaduni wa kufanya mazoezi mara kwa mara sanjari na kujenga mahusiano na mafungamano ya kijamii, sanjari na kuzingatia lishe bora na mwishoni kujipatia maji safi na salama. Watu wasifiche hisia zao, waoneshe upendo na ukarimu kwa jirani zao. Waepuke matumizi haramu ya dawa za kulevya pamoja na mitandao ya kijamii.

Matumizi haramu ya dawa za kulevya ni chanzo cha mgogoro wa afya ya akili
Matumizi haramu ya dawa za kulevya ni chanzo cha mgogoro wa afya ya akili

Shirika la Afya Duniani, WHO linasema, kuna haja ya kuendelea kutoa wito kwa serikali za kitaifa na za mitaa kuweka kipaumbele katika kupunguza mambo yanayojulikana kuwa hatari kwa afya ya akili ya watu: kama vile ukata na ugumu wa maisha, migogoro ya kijamii na kimapenzi na jambo hili linaanza kuchukua kasi ya ajabu kwa jamii nyingi. Unyanyapaa kwa watu wenye mahitaji maalum pamoja na dhana au Mila potofu katika jamii. Pia kuna haja ya kuwaimarisha wale wote wanaoshughulika: kulinda afya za akili kuanzia mtu mmoja mmoja hadi mashirika binafsi na kuunda nyenzo zinazohitajika kwa watu kustawi na kuneemeka. Siku ya Afya ya Akili Duniani ni nafasi ya kuzungumza kuhusu afya ya akili kwa ujumla, jinsi binadamu anavyohitaji kuitunza, na jinsi ilivyo muhimu kuzungumza kuhusu watu wanavyojisikia, ili hatimaye kupata msaada ili kumaliza tatizo na changamoto za kiafya. Uchunguzi unaonesha kwamba, waathirika wakuu wa afya ya akili ni wanaume. Vyanzo vya magonjwa ya afya ya akili vinaweza kuwa ni vya kibaiolojia, kwa kurithi au kushikwa na magonjwa mbalimbali. Kisaikolojia: baadhi ya visababishi ni malezi, familia tenge, ugumu wa maisha na kuondokewa na watu wa karibu sana katika maisha. Kijamii inakuwa ni changamoto za kiuchumi, matatizo ya ndoa na familia pamoja na upweke hasi. Takwimu za Umoja wa Mataifa zinaonesha kwamba, takribani watu bilioni 1 duniani kote wanaishi na matatizo ya akili.

Watu wanahimizwa kushiriki katika michezo kwa ajili ya kudumisha afya bora
Watu wanahimizwa kushiriki katika michezo kwa ajili ya kudumisha afya bora

Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa Antonio Guterres kupitia ujumbe wake kwa siku hii amesema, inabidi hatua zichukuliwe ili kuhakikisha kunakuwa na huduma bora ya afya ya akili kwa wote Mambo ya kuzingatia ili kuboresha afya ya akili: Wakati wa changamoto na hali ngumu zaidi maishani, una uwezo wa kushughulikia chochote kinachokujia na kufanikiwa kupitia kila hali au hali. Kuwafikia wengine kuomba msaada sio udhaifu na katika jamii ambayo watu wengi hawapendi kuomba msaada, kuomba msaada ni ishara ya nguvu na ujasiri. Ushujaa unatokana na njia ambazo tunajifunza kufikiria na kutenda tunapokabiliwa na vizuizi. Tunaposaidia kukuza njia ya maisha inayoona vizuizi kama sehemu muhimu ya mafanikio, tunasaidia watu kukuza ujuzi wa kukabiliana na kujenga uthabiti. Kuunganishwa kwa kijamii kunaboresha ustawi wa mwili, kiakili, na kihemko. Mafungamano ya kijamii huongeza hali ya mtu kuwa mali na hazina muhimu; hukuza hisia za thamani ya kibinafsi, hutoa ufikiaji wa vyanzo vya msaada, na hupunguza hatari ya mtu kutema zawadi ya maisha.

Siku ya Afya ya Akili Duniani
09 October 2023, 13:48