Tafuta

Kutokana na migogoro ya Sudan watu wengi wanakimbilia Chad , ambapo tayari ina migogoro yake ya ndani Kutokana na migogoro ya Sudan watu wengi wanakimbilia Chad , ambapo tayari ina migogoro yake ya ndani 

Chad:Inatosha umwagaji damu kwa wasio na hatia!

Baraza la Maaskofu wa Chad (CET)katika risala waliyosoma mbele ya Rais wa Mpito limeiomba serikali kushughulikia matatizo yanayowakumba wananchi kama vile kuenea kwa ukosefu wa usalama,uhaba wa mahitaji msingi na muundo wa tume ya kitaifa inayosimamia kuandaa kura ya maoni ya katiba (Conerec).

Na Angella Rwezaula, - Vatican.

Damu na machozi ya Wachad yametiririka vya kutosha na lazima yakome. Ndivyo wamonya Maaskofu wa Baraza la Maaskofu Catoliki nchini  Chad katika risala iliyoelekezwa kwa Rais wa Mpito, Kaimu Mkuu wa Nchi, Mahamat Idriss Déby. Katika risala hiyo Baraza la Maaskofu wa Chad (CET) limeiomba serikali kushughulikia matatizo yanayowakumba wananchi kama vile kuenea kwa ukosefu wa usalama, uhaba wa mahitaji msingi na muundo wa tume ya kitaifa inayosimamia kuandaa kura ya maoni ya katiba (Conerec). Kwa mujibu wa Maaskofu hao, ni vigumu kuamini kwamba mauaji na uhaba wa mahitaji ya msingi nchini Chad ni ya kawaida na ya bahati mbaya. “Hali hizi zinazoundwa kwa hiari au kwa kutojua zinaleta changamoto kwetu sote, lakini kwanza kwa watawala ambao wamejipa dhamira moja ya kudhamini usalama na ustawi wa watu wao”, walisema.

Migogoro haina kikomo

Orodha ya migogoro ya umwagaji damu na waathirika wa ghasia ni ndefu na mbaya walisisitiza Baraza la  Maaskofu wa Chad wakitoa mfano kuwa “huko Salamat, huko Moyen Chari, katika Logones mbili, Mayo Kebbi Mashariki na Magharibi, na kama ilivyo Mashariki Magharibi mwa Nchi  nzima na katikati mwa Guéra, kuna ukiwa uleule na orodha haijakamilika.” Kwa mujibu wa taarifa ni kwamba hivi karibuni watu kadhaa walipoteza maisha katika mapigano kati ya wakulima na wafugaji huko Bahr Sara, kilomita 600 kusini mashariki mwa N’Djamena, eneo la nchi hiyo. Miongoni mwa uhaba mkubwa wa mahitaji ya kimsingi kuna yale ya mafuta, ambapo walisema ni kitendawili cha mkataba kwa nchi inayosafirisha mafuta. Kwa hiyo: “Serikali lazima ichukue hatua bila upendeleo wowote na kwa kutumia jina la sheria, ikiwa haitaki kutuhumiwa kuwa mwandishi wake na kutumia ugaidi kama njia ya kutawala, kudumisha au kuhifadhi madaraka”, walieleza kwa kutaja  ukandamizaji mkali wa mnamo tarehe 20 Oktoba 2022 kuhusu maandamano yaliyoitishwa kupinga kusalia madarakani kwa miaka mingine miwili ya Rais wa Mpito Mahamat Déby.

Msamaha kwa waliondamana na kutaka mapinduzi

Mnamo  tarehe 24 Mei 2023, aliwasamehe watu 67 waliopatikana na hatia ya kushiriki katika maandamano ya Oktoba 20, na wengine 11 kwa mapinduzi yalizuiwa mwezi Desemba kulingana na mamlaka ya N'Djamena. Baada ya kifo cha babake, Idriss Déby, tarehe 20 Aprili 2021, Mahamat Déby alichukua mamlaka, na kusimamisha Katiba, na kujiweka kama mkuu wa Baraza la Mpito. Mahamat Déby mara moja aliahidi kurudisha mamlaka kwa raia kupitia uchaguzi baada ya kipindi cha mpito cha miezi 18. Lakini mwishoni mwa mamlaka yake alikuwa ameongeza muda wake kwa miaka miwili kwa pendekezo la mazungumzo ya upatanisho wa kitaifa yaliyosusiwa na takriban wengi wa upinzani wa kiraia (na ambapo Baraza la Maaskofu pia liliamua kutoshiriki) na harakati kuu za waasi wenye silaha. “Hatimaye, tunakumbuka kwamba madhara ya vita kati ya makundi ya kijeshi nchini Sudan yana uzito kwa Chad  kutokana na kwamba watu wanaokimbia ghasia wanaendelea kufika nchini humo kwa wingi, wamesisitiza.

Maaskofu Chad

 

02 June 2023, 11:29