Mgogoro wa Afghanistan kwa wakimbizi ni mgumu!
Na Sr. Angela Rwezaula – Vatican.
Rais wa Marekani Bwana Joe Biden amesema anaweza kurefusha uwepo wa wanajeshi wa Marekani nchini Afghanistan hata baada ya tarehe 31 Agosti 2021, ambayo ndio muda wa mwisho. Ameyasema hayo katika mahojiano na kituo cha televisheni cha ABC cha nchini Marekani, akijibu swali la nini kitafanyika ikiwa baada ya tarehe hiyo, watakuwepo raia wa Marekani wanaosalia kwenye ardhi ya Afghanistan.
Hata hivyo inaaminika kuwa hadi sasa wapo Wamarekani wapatao 15,000 nchini Afghanistan, ambayo iko chini ya udhibiti wa Taliban. Aidha, Bwana Biden amekataa ukosoaji dhidi ya utawala wake, kwamba haukufanya vya kutosha kuepusha mtafaruku na ghasia vilivyoambatana na kuondoka nchini Afghanistan baada ya Wataliban kuushikilia mji wa Kabul. Leo hii kuna kikao cha G7 cha Mawaziri wa Nchi za Nje kwa njia ya mtandao.
Mawasiliano na Wataliban yanabaki wazi, japokuwa wanamgambo wanaonya kuwa "hatutatumia demokrasia, sheria ni ya Sharia". Rais wa zamani wa Afghanistan Ghani, labda amehifadhiwa katika Falme za Kiarabu, anaofikiria kurudi nchini, lakini kwa wakati huo Wataliban wameanza kukandamiza wapinzani kwa damu, hadi sasa zaidi ya watu 30 wameuawa huko Jalalabad, wakati mtoto wa Kamanda Massoud, kiongozi mashuhuri wa mapambano dhidi ya Taliban, ametangaza: upinzani wa silaha umeanza tena huko Panjshir. Katika picha zilizooneshwa kwenye vyombo vya habari, vinaoneshwa wazi mahangaiko ya watu wa Afghanistan na wanamgambo hao.