Umoja wa Mataifa: Umoja na Mshikamano dhidi ya Corona
Na Padre Richard A. Mjigwa, C.PP.S. – Vatican.
Katibu mkuu wa Umoja wa Mataifa Bwana Antonio Guterres anaitaka Jumuiya ya Kimataifa kujenga na kudumisha umoja na mshikamano katika mapambano dhidi ya ugonjwa wa homa ya mapafu unaosababishwa na Virusi vya Corona, COVID-19. Nchi maskini zaidi duniani zinapaswa kupewa kipaumbele cha pekee katika mapambano dhidi ya ugonjwa huu hatari sana kwa ustawi, maendeleo na mafao ya familia ya Mungu. Jumuiya ya Kimataifa imeingia katika vita dhidi ya Virusi vya Corona, COVID-19, kumbe, kuna haja ya kubainisha sera na mbinu mkakati wa kupambana na Virusi hivi ambavyo vimekuwa na madhara makubwa katika maisha na ukuaji wa uchumi sehemu mbali mbali za dunia. Changamoto hii inatolewa wakati huu ambapo viongozi wa Kundi la Nchi Tajiri Duniani, G20 wanakutana Alhamisi, tarehe 26 Machi 2020 huko Riyadhi, Falme za Kiarabu ili kujadili pamoja na mambo mengine, kuhusu ugonjwa wa homa ya mapafu unaosababishwa na Virusi vya Corona, COVID-19.
Sera na mikakati ya kupambana na Virusi vya Corona, COVID-19 inapaswa kuratibiwa na Shirika la Afya Duniani, WHO, ili hatimaye, dunia iweze kuondokana na Virusi vya Corona, COVID-19. Kuna haja ya kuangalia jinsi ya kuboresha usafirishaji wa dawa na vifaa tiba kwa ajili ya kupambana na Virusi vya Corona, COVID-19. Takwimu za WHO zinaonesha kwamba, kuna zaidi ya watu 423, 121 walioambukizwa na watu 18, 919 wamekwisha fariki dunia na wengine zaidi ya 108, 619 wamebahatika kupona. Idadi ya waathirika na vifo inaongezeka kila wakati lakini hadi wakati huu, Italia inaongoza kwa kuwa na vifo vingi duniani, ikifuatiwa na Hispania. China hali inaendelea kuwa shwari kwa wakati huu.