Burkina Faso:Shambulizi la Kanisa la kiprotestanti
Na Sr. Angela Rwezaula – Vatican
Waamini karibia 24 wameuwawa siku ya Jumapili tarehe 16 Februari 2020 nchini Burkna Faso na watu wenye silaha katika Kanisa la Pansy, Kaskazini mashariki mwa nchi hiyo wakati waamini wanafanya ibada yao na mchungaji wao pia watu 18 kujeruhiwa. Janga hili linajitokeza baada ya siku chache kutekwa nyara na kuuwawa kwa mtawa mmoja na familia yake. Mashambulizi ya makanisa kaskazini mwa Burkina Faso yanadaiwa kufanywa na makundi ya kijihadi ambayo yanazidi kuongezeka siku hadi siku katika ukanda huo licha ya uwepo wa operesheni ya kuwakabili. Hata hivyo makundi hayo yapo pia Mali na Niger.
Kuanzia 2018 hadi sasa mashambulizi yamekuwa takiwalenga wakristo katika ibada mbalimbali kanisani. Hata hivyo wataalam wanasema kuwa mara nyingi wakristo ambao ni wachache wamekuwa wakikabiliana na vurugu na kushambuliwa na wanajihadi ambapo Burkina Faso imekuwa na historia ya muda mrefu ya uvumilivu wa kidini ba ukosefu wa amani na migogoro imefanya wanajihadi kuweza kutawala eneo hilo.
Askofu mkuu wa Ouagadougou amesisitiza juu ya uwepo wa soko la silaha kwamba nchini Burkina Faso, Mali na Niger ni matatizo hayo ya kutisha yanayo sababisha na makundi yanayofanya mashambulizi. Kuna haja ya kufanya mshikamano wa kimataifa kwa ajili ya kusitisha soko la silaha linalosadia watu wengi wawaue ndugu zao bila sababu amesisitiza Askofu Mkuu kwa masikitiko makubwa.