Tafuta

Maparoko 300 toka sehemu mbalimbali za dunia, kushiriki mkutano huo kuanzia tarehe 28 Aprili hadi tarehe 2 Mei 2024 kwa kunogeshwa na kauli mbiu “Maparoko Kwa Ajili ya Sinodi. Mkutano wa Kimataifa.” Maparoko 300 toka sehemu mbalimbali za dunia, kushiriki mkutano huo kuanzia tarehe 28 Aprili hadi tarehe 2 Mei 2024 kwa kunogeshwa na kauli mbiu “Maparoko Kwa Ajili ya Sinodi. Mkutano wa Kimataifa.”   (Vatican Media)

Maadhimisho ya Sinodi ya Maparoko 28 Aprili - 2 Mei 2024: Mkutano wa Kimataifa

Baraza la Kipapa la Uinjilishaji wa Watu, Baraza la Kipapa la Kwa Ajili ya Makanisa ya Mashariki, Sekretarieti kuu ya Sinodi za Maaskofu pamoja na Baraza la Kipapa kwa Ajili ya Makleri, kwa pamoja wameandaa mkutano wa kimataifa utakaowashirikisha Maparoko 300 watakaoshiriki mkutano huo kuanzia tarehe 28 Aprili hadi tarehe 2 Mei 2024 kwa kunogeshwa na kauli mbiu “Maparoko Kwa Ajili ya Sinodi. Mkutano wa Kimataifa: Kusikiliza, Kusali na Kufanya Mang'amuzi.

Na Padre Richard A. Mjigwa, C.PP.S., Vatican.

Baba Mtakatifu Francisko mwanzoni kabisa mwa maadhimisho ya Sinodi ya XVI ya Maaskofu 2021-2024, Jumamosi tarehe 9 Oktoba 2021, alitoa hotuba elekezi, ambayo ni msingi wa maadhimisho ya Sinodi katika hatua mbalimbali za maisha na utume wa Kanisa kwa kunogeshwa na kauli mbiu “Kwa Ajili ya Kanisa la Kisinodi: Umoja, Ushiriki na Utume.” Watu wa Mungu wakajitambua kuwa wao ni sehemu ya Kanisa la Kisinodi, tayari kutangaza na kushuhudia Ufalme wa Kristo Yesu, kwa kushirikiana na binadamu wote, kusikiliza kwa makini kile ambacho Roho Mtakatifu anataka kuyaambia Makanisa. Huu ni wakati wa kuanza tena kufanya hija hii ya kitume, kama mwendelezo wa Maadhimisho ya Sinodi ya XVI ya Maaskofu iliyozinduliwa kunako mwaka 2021 na itafikia kilele chake Mwezi Oktoba 2024.

Kauli mbiu: Maparoko Kwa Ajili ya Sinodi. Mkutano wa Kimataifa
Kauli mbiu: Maparoko Kwa Ajili ya Sinodi. Mkutano wa Kimataifa

Hii ni sehemu ya barua kutoka katika Sekretarieti kuu ya Sinodi za Maaskofu kama sehemu ya maandalizi kwa ajili ya Kanisa la Kisinodi na Kimisionari hatua muhimu kuelekea Sinodi ya Mwaka 2024. Sekretarieti kuu ya Sinodi imekwisha kuchapisha mwongozo utakaotumika katika Maadhimisho ya Awamu ya Pili ya Sinodi ya Maaskofu. Ni katika muktadha huu, Baraza la Kipapa la Uinjilishaji wa Watu, Baraza la Kipapa la Kwa Ajili ya Makanisa ya Mashariki, Sekretarieti kuu ya Sinodi za Maaskofu pamoja na Baraza la Kipapa kwa Ajili ya Makleri, kwa pamoja wameandaa mkutano wa kimataifa utakaowashirikisha Maparoko 300 watakaokuwa wameteuliwa na Mabaraza ya Maaskofu Katoliki toka sehemu mbalimbali za dunia, kushiriki mkutano huo kuanzia tarehe 28 Aprili hadi tarehe 2 Mei 2024 kwa kunogeshwa na kauli mbiu “Maparoko Kwa Ajili ya Sinodi. Mkutano wa Kimataifa.”

Sinodi ya Maparoko: Kusikiliza, Kusali na Kufanya Mang'amuzi
Sinodi ya Maparoko: Kusikiliza, Kusali na Kufanya Mang'amuzi

Lengo ni kuendelea kujenga utamaduni wa kusikiliza, kusali na kufanya mang’amuzi ya pamoja kutoka katika Makanisa mahalia. Hii ni sehemu ya utekelezaji wa mapendekezo yaliyotolewa na Mababa wa Sinodi kuhakikisha kwamba, mchakato huu, unawahusisha: mashemasi, mapadre na maaskofu, ili kusikiliza sauti na mchango wao. Mkutano huu utajikita katika mchakato wa ujenzi wa utamaduni wa kusikilizana, sera na mikakati ya shughuli za kichungaji, majadiliano na wataalam pamoja na maadhimisho ya Liturujia ya Kanisa. Uteuzi wa Maparoko watakaoshiriki katika Maadhimisho haya ni kama ule uliotumika kwa ajili ya kuwachagua wajumbe wa Sinodi ya Maaskofu iliyofanyika mwezi Oktoba 2023. Maparoko walioteuliwa ni wale wenye mchango mkubwa katika kukuza na kudumisha Kanisa la Kisinodi katika medani mbalimbali za maisha na utume wa Kanisa. Maparoko watakaokuwa wameteuliwa, watatumiwa utaratibu wa mkutano huu, hadi kufikia tarehe 15 Mei 2024. Maparoko hawa watapata fursa ya kukutana na kuzungumza na Baba Mtakatifu Francisko. Matunda ya kazi hii ya Maroko kutoka sehemu mbalimbali za dunia, yatachangia kutengeneza Hati ya Kutendea Kazi, “Instrumentum laboris” katika Maadhimisho ya Awamu ya Pili ya Sinodi ya XVI ya Maaskofu 2021-2024, itakayofikia kilele chake mwezi Oktoba 2024.

Sinodi Maparoko

 

04 February 2024, 16:04