Kard. Farrell,Kanisa liwe karibu ba wanawake waathirika wa unyanyasaji
Na Angella Rwezaula, - Vatican.
Katika kuadhimisha Siku ya Kimataifa ya Kutokomeza Ukatili dhidi ya Wanawake, ifanyikayo kila tarehe 25 Novemba ya kila mwaka, Mwenyekiti wa Baraza la Kipapa la Walei, Familia na Maisha, Kardinali Kevin Farrell, alitoa tamko lake huku akisitiza umuhimu wa nafasi ya Kanisa katika kupambana na kuzuia jambo hilo. Kwa mujibu wake alisema kuwa: “Kanisa lina jukumu la kuwa karibu na wanawake ambao ni wahanga wa ukatili na unyonyaji, na ukaribu huo unaweza kuoneshwa kwa njia nyingi: kuanzia katika kutoa makazi salama, kwa waathiriwa wa ukatili, msaada wa kisaikolojia na kiroho ili kuwasaidia waathiriwa wenyewe kushinda kiwewe na kuripoti unyanyasaji huo".
"Kipengele muhimu," Kardinali Farrell aliendelea, "pia ni elimu kuelekea heshima kwa wanawake, ambayo huanza na kutambua tatizo ndani ya familia na jumuiya za Kikristo pia. Kuelimisha watu kuhusu upendo, upole, heshima kwa wengine na kwanza kwa wao wenyewe katika maisha, ambayo ni muhimu sana katika kuzuia unyanyasaji dhidi ya wanawake, ambao yamejikita kwa nguvu na kwa kina katika Injili". Kardinali Farrell aidha alisema, "Kwa hiyo, ninaomba makanisa yote duniani kuchukua hatua ya kuzipatia familia, vijana, wanandoa na jamii njia za elimu zinazolenga kuzuia ukatili dhidi ya wanawake. Hili ni jukumu la kichungaji. Wito wa Kanisa kuwa chombo cha amani unadhihirika” alihitimisha Kardinali.