Hija ya Kitume ya Papa:mchakato wa amani na upatanisho nchini Sudan Kusini
Na Angella Rwezaula;- Vatican.
Katika fursa ya Ziara ya Kitume ambayo imemalizika nchini Congo DRC (31 Januari-3 Feb) na sasa Kusini mwa Sudan, Baraza la Kipapa la Kuhamasisha Umoja wa Kikristo linabainisha kwamba “Kuwasili kwa Papa Francisko nchini Sudan Kusini kuanzia tarehe 3 -5 Februari 2023 kunaashiria mwanzo wa hija ya kiekumene ya amani ambayo haijawahi kutokea. Katika ziara yake ya kitume itakayomuona jijini Juba, ambao ni mji mkuu wa nchi hiyo, Baba Mtakatifu anasindikizana na Askofu mkuu Justin Welby wa Canterbury, na Mchungaji Iain Greenshields msimamizi wa mkutano mkuu wa Kanisa la Scotland. Mbali na kuwa na umuhimu ulio wazi kwa wananchi wa Sudan na kwa hali ya kisiasa na kijamii ya nchi hiyo, Hija hiyo ina thamani kubwa ya kiekumene. Itakuwa ni mara ya kwanza kwa Askofu wa Roma kufanya ziara ya pamoja na viongozi wa Makanisa ya Kianglikani na Kipresbyterian iliyopyaishwa. Takriban theluthi mbili ya wakazi wa Sudan Kusini ni Wakristo na kiwango cha ushirikiano na umoja kati ya tamaduni mbalimbali za Kikristo hadi sasa zimekuwa nzuri sana.
Baraza la Makanisa la Sudan (Scc) lilianzishwa na Askofu wa Kikatoliki Augustino Baroni na askofu wa Kianglikani Oliver Allison mnamo mwaka wa 1965, kabla ya kuanzishwa kwa Sudan Kusini kama taifa tofauti. Katika takriban miaka 60 tangu wakati huo, dhidi ya hali chungu ya mizozo, umwagaji damu na kusambaratika kabisa kwa mashirika ya kiraia, Baraza hilo la Makanisa (SCC) na baraza lililofuata, la Makanisa la Sudan Kusini (SSCC) limefanya kazi kwa bidii sana ili kukuza umoja na mshikamano wa Wakristo. Kwa kuzungumzia Kanisa, Wasudani kusini kwa kawaida hurejea na kujikita zaidi juu ya ushuhuda wa pamoja wa jumuiya mbalimbali za Kikristo ya kwamba ni imani au mapokeo maalum; viongozi wa Kanisa wenyewe mara nyingi hujiona kuwa wachungaji wa kundi zima la Kikristo. Moja ya historia nyingi katika maana hiyo ni ile ya Askofu wa kianglikani ambaye alikumbuka simu alizopokea kutoka kwa mwenzake wa Kanisa Katoliki, na ambaye, kila mara alipolazimika kutokuwepo jimboni, alimpigia simu kabla ya kuondoka na kumuomba atunze watu wake yeye akiwa mbali.
Kwa hiyo hiyo wasiwasi wa Papa Francisko, wa Askofu Mkuu Welby na msimamizi wa Kanisa la Scotland (ambao wamebakiza muda mfupi yaani kwa mwaka mmoja tu katika mamlaka ya Kanisa), kuhusu hali ya Sudan Kusini ni nuru ya asili ya utamaduni wa nchi hiyo wa ushirikiano wa karibu wa kiekumene. Kwa muda mrefu walikuwa wanataka kutembelea nchi hiyo pamoja. Safari hiyo ilibuniwa wakati wa mafungo ya kiroho yaliyofanyika katika Nyumba ya Mtakatifu Marta mnamo 2019, wakati viongozi wa kisiasa wa Sudan Kusini waliahidi kuwa watafanya kazi pamoja kwa ajili ya faida ya watu wao. Akisisitiza mwelekeo wa kiekumene wa ziara hiyo, Papa Francisko hata hivyo alisisitiza jinsi ilivyo muhimu kwake kuchangia mchakato wa amani na upatanisho nchini Sudan Kusini, na kwamba “sio peke yake, bali kwa kufanya hija ya kiekumene pamoja na ndugu wawili wapendwa: Askofu mkuu wa Canterbury na msimamizi wa mkutano mkuu wa Kanisa la Scotland”.
Umoja huo, ambao kwamba kabisa ulikuwa thabiti kati ya jumuiya za Kikristo za Sudan Kusini, umepasuka kwa kiasi fulani katika siku za hivi karibuni na kuibuka kwa mivutano ya kikabila inayoongezeka ndani ya Makanisa na kati ya Makanisa. Viongozi hao watatu wa kikanisa wanaotembelea nchi hiyo kwa pamoja kama mahujaji katika njia ya amani ya kiekumene, wanataka kuwasaidia Wakristo wa Sudan Kusini kupata nafuu na kuimarisha wito wao kama vyombo vinavyoonekana vya upatanisho na umoja. Hija ya Papa, ya Askofu mkuu Welby na msimamizi wa Kanisa la Scotland kwa hiyo ni njia ya kutekeleza agizo la Petro alilokabidhiwa na Bwana la “Kuwaimarisha ndugu” (rej. Lk 22:32). Huo ni ukweli kwamba Papa Francisko anafanya kazi hiyo ya Petro pamoja na Askofu Mkuu Welby na mchungaji Greenshields, msimamizi wa Kanisa la Scotland na umuhimu mkubwa wa kiekumene.
Kusasisha makala tarehe 3 Februari 2023:saa 8.20