Hija ya Kitume ya Papa Francisko Cyprus na Ugiriki:kujikabidhi kwa Mama Maria
Na Sr. Angella Rwezaula – Vatican.
Ikiwa ni utamaduni uliojengeka sasa kabla ya kila safari ya kitume, Jumatano Alasiri tarehe Mosi Desemba katika mkesha wa hija yake ya kwenda Cyprus na Ugiriki, Papa Francisko alifika kwenye Kanisa kuu la Mtakatifu Maria Mkuu, kwa gari ili kukabidhi safari yake ya 35 ya kimataifa kwa Mama Yetu. Kwa mujibu wa taarifa kutoka Ofisi ya Vyombo vya Habari Vatican inasema: “Mchana wa leo, tarehe 1 Desemba, Papa Francisko alikwenda kwenye Katisa kuu la Mtakatifu Maria Mkuu kusali mbele ya picha ya Bikira, Salus Populi Romani na kumkabidhi safari yake ya kwenda Cyprus na Ugiriki na Mwishoni akarudi Vaticani”,
Tendo hili ni tangu mwanzo wa upapa wake ambapo Baba Mtakatifu Fransisko,mara kadhaa kabla ya kuondoka kwenda nje ya nchi, anakwenda kukaa kwa dakika kadhaa, akiwa peke yake, katika sala mbele ya Picha ya Maria afya ya watu wa Roma inayohifadhiwa katika Kikanisa cha pembeni ndani ya Kanisa Kuu ambayo, inayopendwa sana na watu wa Roma. Pia katika safari hii ya Cyprus na Ugiriki, itakayofanyika kuanzia kesho tarehe 2 hadi Jumatatu tarehe 6 Desemba, Papa ameomba ulinzi wa Mama Yetu mara baada ya katekesi yake asubuhi kwenye ukumbi wa Paulo VI kwa akiwageukia waamini na mahujai wote na kutoa wito kwa watu wa Mungu akiwaomba kumsindikiza kwa sala katika ziara hii ya kitume kwenye vyanzo vya imani na udugu wa kiekumene, ambapo, akiwa huko Lesbos, atakuwa na fursa ya kuwa karibu na ubinadamu uliojeruhiwa wa maelfu ya wahamiaji katika kambi za wakimbizi.