Viongozi Wapya Baraza Kipapa La Ibada na Nidhamu ya Sakramenti
Na Padre Richard A. Mjigwa, C.PP.S. – Vatican.
Baba Mtakatifu Francisko amemteuwa Askofu mkuu Arthur Roche, kuwa Mwenyekiti wa Baraza la Kipapa la Ibada na Nidhamu ya Sakramenti za Kanisa. Kabla ya uteuzi huu, Askofu mkuu Arthur Roche alikuwa ni Katibu mkuu wa Baraza la Kipapa la Ibada na Nidhamu ya Sakramenti za Kanisa. Wakati huo huo, Baba Mtakatifu Francisko amemteua Askofu Vittorio Francesco Viola, O.F.M kuwa Katibu mkuu wa Baraza la Kipapa la Ibada na Nidhamu ya Sakramenti za Kanisa na kumpandisha hadhi kuwa Askofu mkuu. Kabla ya uteuzi huu, Askofu mkuu Vittorio Francesco Viola alikuwa Askofu wa Jimbo Katoliki la Tortona, nchini Italia. Wakati huo huo, Baba Mtakatifu Francisko amemteua Monsinyo Aurelio Garcia Marcìas kuwa Katibu mkuu Msaidizi wa Baraza la Kipapa la Ibada na Nidhamu ya Sakramenti za Kanisa.
Itakumbukwa kwamba, Askofu Aurelio Garcia Marcìas Katibu Mkuu Msaidizi wa Baraza la Kipapa la Ibada na Nidhamu ya Sakramenti za Kanisa alizaliwa tarehe 28 Machi 1965 huko Pollos, Hispania. Baada ya masomo na majiundo yake ya Kikasisi, kunako mwaka 1992 akapewa Daraja Takatifu ya Upadre. Akajiendeleza zaidi katika masomo na kujipatia Shahada ya Uzamivu katika Liturujia kutoka katika Taasisi ya Kipapa ya Liturujia, Chuo Kikuu cha Kipapa cha Mtakatifu Anselm, kilichoko mjini Roma. Amewahi kuwa ni mwakilishi wa Idara ya Liturujia, Jimbo kuu la Valladolid, Hispania na Gambera wa Seminari ya Jimbo. Tangu tarehe 1 Septemba 2015 alianza kutekeleza utume wake kwenye Baraza la Kipapa la Ibada na Nidhamu ya Sakramenti za Kanisa na mwaka 2016 akateuliwa na Papa Francisko kuwa ni mkuu wa Ofisi ya Baraza la Kipapa la Ibada na Nidhamu ya Sakramenti za Kanisa.