Tafuta

Tarehe 2 Januari 2020 yamefanyika mazishi ya Kardinali Prosper Grech aliyeaga diunia tarehe 30 Desemba 2019 Tarehe 2 Januari 2020 yamefanyika mazishi ya Kardinali Prosper Grech aliyeaga diunia tarehe 30 Desemba 2019 

Mazishi ya Kard.Grech:Alikuwa mwenye mafundisho makubwa na tasaufi ya kina!

Papa Francisko,Alhamisi tarehe 2 Januari 2020 majira ya asubuhi kwenye Kanisa kuu la Mtakatifu Petro mjini Vatican,ameongoza Ibada ya Mazishi ya Kardinali Prosper Grech aliyeaga dunia,tarehe 30 Desemba 2019 akiwa na umri wa miaka 94.Ibada ya Misa Takatifu imeongozwa na Kardinali Giovanni Battista Re Makamu,Dekano wa Makardinali.

Na Sr. Angela Rwezaula – Vatican

Alikuwa tayari na mshumaa unawaka akisubiri ili Bwana atakapobisha mlango aweze kumfungulia. Kaeni tayari... kwa maana hamjuhi siku wala saa... (Lc.12,3540). Tahadhali hii imesikika tena katika Injili  iliyo somwa ambayo ni kati ya Injili inayojulikana sana katika Biblia na uzoefu wa kila siku ambao unajionesha kwa wakati huu. Ndiyo mwanzo wa mahubiri ya Kardinali Giovanni Battista Re, Makamu Dekano wa Baraza la Makardinali wakati wa Ibada ya Misa Takatifu kwa ajili ya Mazishi ya Kardinali Prosper Grech aliyefariki tarehe 30 Desemba 2019 mjini Roma. Baada ya Misa Papa Francisko ameongoza Ibada ya Mazishi ya Kardinali Grech.

Akiendelea na mahubiri hayo Kardinali Re amesema licha ya hayo yote  kila mara Bwana anakuja kubisha mlango kwa kila mtu na wakati huo huo hatujuhi ujio wake na kila mara inapotokea tunapatwa mshangao! Na zaidi tuna tabia ya asili ya kutaka kushikilia maisha lakini ambayo mara nyingi tunadanganywa, kwa maana  hata umri unaongezeka na hali halisi ya matatizo ya kiafya kujitokeza. Usiku wa sikukuu ya Kuzaliwa kwa Bwana Kardinali Prosper Grech alikuwa katika Kanisa Kuu la Mtakatifu Petro akishiriki katika maadhimisho ya Misa na Papa Francisko. Jumatati katika wiki hiyo alikuwa kama kawaida mezani na jumuiya yake ya Kiagostiniani huku akizungumza kama kawaida ya tabia yake, lakini masaa machache baadaye, Bwana Mungu alimwita kwake.

Kwa hakika kifo hakijamkuta bila kuwa na maandalizi. Maisha yake marefu aliyokuwa tayari ametimiza miaka 94 wakati wa mkesha wa Kuzaliwa kwa Bwana na maisha yake ya kutiwa wakfu kwa Mungu katika Shirika la Mtakatifu Agostino vimemwezesha kuwa na subira ya wakati ule wa siku ya mwisho ya kuitwa na Bwana. Na uhakika wa imani ambao aliokuwa amewafundisha wengine ilimpatia mwanga wa utambuzi kwamba kufa ni kuingia katika furaha kubwa sana ya upendo wa Mungu. Ni katika kipimo cha kati cha maisha yake marefu na ya bidii katika maisha yake Kardinali Grech na zaidi ya kuwa mtawa katika Shirika la Wagostiniani, alikuwa ni mtaalam wa mafunzo ya kina ya Taalimungu na katika imani kamili ya utume wa Kanisa .

Na kama mshauri wa Baraza la Kipapa la Mafundisho Tanzu ya Kanisa alikuwa kwa hakika na ushirikiano wa karibu sana na Kardinali Joseph Ratzinger( Baba Mtakatifu Mstaafu Benedikto XVI, wakati huo akiwa ni Rais wa Baraza la Kipapa hilo). Na kwa kuongezea, kwa zaidi ya miaka 20 alifundisha  masomo ya kichungaji katika Taasisi ya Kipapa ya Biblia na Taalimungu ya Biblia katika Chuo Kikuu cha Kipapa cha Laterano. Ni makala nyingi na vitabu  kuhusu maandiko matakatifu na kuhusu Mababa wa Kanisa. Alikuwa ni mwanaume thabiti katika imani na mafundisho ya Mababa wa Kanisa ambapo kwa hakika Kardinali  Grech alipenda sana Mtakatifu Agostino  na mtafiti wa umuhimu wa mafundisho yake. Alikuwa anaamini kwamba "kwa kusoma maandiko ya Mtakatifu Agostino, tunaweza kupata kitu juu yetu binafsi".

Katika suala hili, katika fursa  kadhaa alithibitisha kwamba Mtakatifu Agostino, hasa katika kitabu cha “ Maungamo”, alizungumza juu yake mwenyewe, juu ya uzoefu wake, lakini kwa kuwa ni uzoefu ya kuwa mwanadamu anaishi katika kila wakati, kwa hiyo kusoma maandisho ya Mtakatifu  Agostino tunasoma kuhusu sisi wenyewe, shida za Kanisa leo hii, shida za jamii, za uhusiano kati ya Serikali na Kanisa na kadhalika, kwa sababu anasema, "inatosha kusoma kazi yoyote ya Mtakatifu Agostino ambayo hupata kila kitu ambacho huzungumza moja kwa moja na moyo". Katika Liturujia hiyo, aidha Kardinali Re amesisitiza kuwa inawalika kuinua mtazamo wao zaidi ya mipaka ya kifo na ili kuilekeza   katika dunia ambayo sasa Kardinali Grech yupo kwa sasa.

Katika somo la Kwanza, Kitabu cha Nabii Ezekili linatoa meneno ya faraja na matumaini na kusema: “Tazama mimi ninafanya aingie ndani mwenu roho na mtaishi… mtatambua kuwa mimi ni Bwana." Maono ya Nabii amesema, yanatuelekeza katika ule ushindi wa mwisho wa Mungu ambaye atafanya wafu wafufuke katika maisha yasiyo na mwisho. Aidha Nabii anazungumzia juu ya  umati wa jeshi kubwa lililoangamizwa, ikiwa na maana ya kutufanya tufikirie kwamba waliokombolewa walikuwa ni umati mkubwa. Kati ya hao tufikirie kwamba yumo hata  Ndugu Kardinali Grech ambaye alikuwa ni mtawa na mwenye elimu kubwa na tasaufi ya kina, aliyependa Kanisa na maisha ya kitawa hasa ambaye aliwekwa Mungu katika nafasi ya kwanza na zaidi ya yote!

Kwa kuhitimisha Kardinali Re ameomba wote wasali kwa Mungu kwa ajili ya roho yake ambaye kama Mtaalimungu na mara nyingi aliye mzungumzia Mungu na kuandika sana juu yake. Kardinali Prosper Grech, alizaliwa  huko Birgu (Vittoriosa) katika kisiwa cha Malta kunako tarehe 24 Desemba 1925 na kubatizwa kwa jina la Stanley. Alibadilisha jina kuwa Prosper wakati alipojiunga kwenye shirika la wagostiniani. Amepata kushika nafasi mbali mbali na uongozi hasa kama profesa na pia kama mmoja wa waanzilishi wa Taasisi ya Masomo ya Kitaalimungu na masomo ya Baba wa Kanisa Agostino, Mjini Roma.

02 January 2020, 15:02