Askofu mkuu Bruno Musarò ateuliwa kuwa Balozi Costa Rica
Na Padre Richard A. Mjigwa, C.PP.S. – Vatican.
Baba Mtakatifu Francisko amemteua Askofu mkuu Bruno Musarò kuwa Balozi mpya wa Vatican nchini Costa Rica. Kabla ya uteuzi huu Askofu mkuu Bruno Musarò alikuwa ni Balozi wa Vatican nchini Misri na mwakilishi wa Vatican kwenye Umoja wa Falme za Kiarabu. Amewahi pia kuwa Balozi wa Vatican nchini Cuba. Itakumbukwa kwamba, Askofu mkuu Musarò alizaliwa huko Otranto, nchini Italia tarehe 27 Juni 1948. Baada ya masomo na majiundo yake ya kikasisi, akapadrishwa kunako tarehe 19 Septemba 1971. Tarehe 3 Desemba 1994 aliteuliwa na Mtakatifu Yohane Paulo II kuwa Askofu mkuu na kuwekwa wakfu hapo tarehe 6 Januari 1995. Tangu wakati huo amekuwa ni Balozi wa Vatican nchini: Madagascar, Visiwa vya Comoro, Visiwa vya Seychelles, Mauritius, Guatemala, Perù, Cuba na mwishoni alikuwa akitekeleza utume wake wa Kidipomasia nchini Misri na mwakilishi wa Vatican kwenye Umoja wa Falme za Kiarabu.