Tafuta

Shida na mahangaiko ya wakimbizi na wahamiaji 3, 000 wanaopata hifadhi kwenye Kambi ya Wakimbizi na Wahamiaji huko Lajas Blancas, Panama, Amerika ya Kusini, Shida na mahangaiko ya wakimbizi na wahamiaji 3, 000 wanaopata hifadhi kwenye Kambi ya Wakimbizi na Wahamiaji huko Lajas Blancas, Panama, Amerika ya Kusini,  

Waamini Onesheni Upendo na Faraja Kwa Wahamiaji na Wakimbizi

Baba Mtakatifu Francisko katika ujumbe wake kwa wakimbizi na wahamiaji hawa anasema, ametamani sana kuwa pamoja nao wakati huu, kwani hata yeye ni Mtoto wa wahamiaji, kwani wazazi wake, waliondoka nchini Italia ili kutafuta maisha bora zaidi ughaibuni. Katika kipindi hiki, walikumbana na changamoto za maisha, kiasi kwamba, hata wakati mwingine, walikuwa hawana chakula, huku wakiwa na mikono mitupu, lakini nyoyo zao zilisheheni matumaini.

Na Padre Richard A. Mjigwa, C.PP.S., Vatican.

Baba Mtakatifu Francisko katika Waraka wake wa Kitume “Misericordia et misera” yaani “Huruma na amani” anasema, huruma ni kielelezo makini cha upendo wa Mungu unaosamehe, unaoongoa, unaopyaisha na kubadili mwelekeo wa maisha. Ni kielelezo cha ufunuo wa Fumbo la Mungu ambalo ni huruma ya milele, inayowakumbatia na kuwaambata wote pasi na ubaguzi, kiasi cha kuwakirimia maisha mapya, chemchemi ya furaha na matumaini mapya, yanayovunjilia mbali ubaguzi, ubinafsi na uchoyo ili kutenda wema, kufikiri vyema na kuondoa huzuni moyoni. Huu ni mwaliko kwa waamini kufanya mang’amuzi ya huruma inayowakirimia furaha, hata kama maisha yao bado yanasheheni matatizo na changamoto mbalimbali, ili kuondokana na utamaduni wa huzuni, utupu na upweke unaopelekea msongo wa mawazo kwa watu wengi!

Waamini wawe vyombo vya huruma na faraja kwa wakimbizi na wahamiaji
Waamini wawe vyombo vya huruma na faraja kwa wakimbizi na wahamiaji

Baba Mtakatifu Francisko anasema, sera na mbinu mkakati wa Kanisa Katoliki katika huduma kwa wakimbizi na wahamiaji inajikita katika mambo makuu manne yaani: “Kuwapokea, kuwalinda, kuwaendeleza na kuwahusisha wakimbizi na wahamiaji” katika maisha ya jamii inayowapokea na kuwapatia hifadhi, usalama na matumaini ya maisha. Ni matumaini ya Baba Mtakatifu kwamba, sera na mikakati hii itaendelea kumwilishwa pia kwenye Makanisa mahalia, ili kuwasaidia watu hawa ambao mara nyingi wanajikuta wakitumbukia katika biashara haramu ya binadamu na viungo vyake; mifumo mbalimbali ya utumwa mamboleo na nyanyaso mambo ambayo kimsingi yanasigina: utu, heshima na haki msingi za binadamu.

Wakimbizi na wahamiaji ni changamoto kubwa ulimwenguni
Wakimbizi na wahamiaji ni changamoto kubwa ulimwenguni

Ni katika muktadha wa shida na mahangaiko ya wakimbizi na wahamiaji 3, 000 wanaopata hifadhi kwenye Kambi ya Wakimbizi na Wahamiaji huko Lajas Blancas, Panama, Amerika ya Kusini, Maaskofu Katoliki kutoka Colombia, Costa Rica na Panamà kuanzia tarehe 19 hadi 22 Machi 2024 wamekutana mpakani kati ya Colombia na Panamà, huku wakiongozwa na kauli mbiu “Sherehe ya Pasaka Na Ndugu Zetu Wahamiaji.” Baba Mtakatifu Francisko katika ujumbe wake kwa wakimbizi na wahamiaji hawa anasema, ametamani sana kuwa pamoja nao wakati huu, kwani hata yeye ni Mtoto wa wahamiaji, kwani wazazi wake, waliondoka nchini Italia ili kutafuta maisha bora zaidi ughaibuni. Katika kipindi hiki, walikumbana na changamoto za maisha, kiasi kwamba, hata wakati mwingine, walikuwa hawana chakula, huku wakiwa na mikono mitupu, lakini nyoyo zao zilisheheni matumaini.

Wakimbizi na wahamiaji ni amana na utajiri wa Kanisa na Jamii.
Wakimbizi na wahamiaji ni amana na utajiri wa Kanisa na Jamii.

Baba Mtakatifu ametumia fursa hii kuwashukuru na kuwapongeza Maaskofu kutoka Amerika ya Kusini pamoja na wafanyakazi wote wanaowashughulikia wakimbizi na wahamiaji katika shida na mahangaiko yao. Ikumbukwe kwamba, hawa ni ufunuo wa sura ya Mama Kanisa anayesafiri na watoto wake katika huzuni na mapendo, kama ilivyokuwa kwa Mtakatifu Veronika kwenye Njia ya Msalaba, kuwatuliza na kuwafariji wakimbizi na wahamiaji. Hawa ni Fumbo la Mwili wa Kristo, unaoendelea kuteseka, kwa kuyakimbia makazi yao na kuanza kukabiliana na hatari na ugumu wa safari baada ya kukosa njia mbadala. Baba Mtakatifu anawakumbusha wakimbizi na wahamiaji kuhusu utu, heshima na haki zao msingi. Wawe na ujasiri wa kutazamana machoni, kwani hata wao ni sehemu ya familia kubwa ya watoto wa Mungu. Baba Mtakatifu anawapongeza kwa kukutana mahali hapa. Mwishoni mwa ujumbe wake, Baba Mtakatifu Francisko amewakabidhi chini ya ulinzi na tunza ya Bikira Maria, Mama wa Kanisa.

Faraja Kwa Wahamiaji

 

26 March 2024, 14:08