Tafuta

Baba Mtakatifu Francisko, Jumatatu tarehe 22 Januari 2024 amekutana na kuzungumza na washiriki wa Kongamano la Divai lililoandaliwa na Makampuni ya Vinitaly. Baba Mtakatifu Francisko, Jumatatu tarehe 22 Januari 2024 amekutana na kuzungumza na washiriki wa Kongamano la Divai lililoandaliwa na Makampuni ya Vinitaly.  (Vatican Media)

Wakulima Wanapaswa Kujikita Katika: Teknolojia, Kanuni Maadili Na Utu Wema

Baba Mtakatifu Francisko, Jumatatu tarehe 22 Januari 2024 amekutana na kuzungumza na washiriki wa Kongamano la Divai lililoandaliwa na Makampuni ya Vinitaly. Hawa ni wakulima na wazalishaji wa divai nchini Italia na kwamba, hawa wanaunda mtandao mkubwa wa wazalishaji na wauzaji wa divai nchini Italia. Kongamano hili pamoja na mambo mengine, limejadili kuhusu kanuni maadili na utu wema mintarafu maisha na utume wa Mtakatifu Francisko wa Assisi.

Na Padre Richard A. Mjigwa, C.PP.S., Vatican.

Divai kama zawadi kutoka kwa Mwenyezi Mungu, ambayo watu, lakini hasa wazalishaji, lazima wajue jinsi ya kusimamia vizuri utengenezaji wake iwezekanavyo. Kwa "sayansi na dhamiri", ili kuiboresha sanjari na kuheshimu pamoja na kutunza mazingira bora nyumba ya wote kwa kufuata kanuni msingi za Uchumi wa Papa Francisko, “Francis Economy.” Baba Mtakatifu Francisko anasema, uchumi katika maana yake ya ndani ni utawala thabiti wa dunia kama nyumba ya wote, kwa sababu ya mwingiliano na mafungamano yake katika maisha na mahusiano ya watu. Uchumi halisi unasimikwa katika misingi inayowashirikisha watu kwa lengo la kutaka kuinua na kuboresha maisha; kulinda na kudumisha utu, heshima na haki msingi za binadamu badala ya kuabudu na kuthamini fedha. Lengo ni kuondokana na vurugu na ukosefu wa usawa. Rasilimali fedha iwe ni kwa ajili ya huduma makini kwa watu wa Mungu. Faida ya kweli iwe ni kwa ajili ya ustawi, maendeleo na mafao ya wengi. Maendeleo ya sayansi na teknolojia pamoja na matumizi ya: muda, rasilimali pamoja na nguvu yasiwapeleke watu “mchakachaka” bali yasaidie kujenga uzoefu wa mafungamano ya kibinadamu. Huu ni mwaliko wa watu kuwa wabunifu na wajenzi watakaojikita zaidi katika ustawi, maendeleo na mafao ya wengi, kwa kuibua sera na mikakati ikayosaidia kuleta maendeleo fungamani ya binadamu. Huu ni ugunduzi wa upendo unaotoa maana ya maisha ya sasa na kujielekeza zaidi katika maboresho ya leo na kesho iliyo bora zaidi. Wongofu wa kiikolojia na ubunifu ni mambo msingi ambayo wanapaswa kurithishwa vijana wa kizazi kipya. Hawa ni wachumi na wajasiriamali vijana.

Divai ni zawadi kutoka kwa Mungu.
Divai ni zawadi kutoka kwa Mungu.

Baba Mtakatifu Francisko anasema, “Economy of Francesco” yaani “Uchumi wa Francisko ni sehemu ya mbinu mkakati wa utume wa Kanisa miongoni mwa vijana wa kizazi kipya, unaotekelezwa kwa namna ya pekee, na Kanisa. Mtakatifu Francisko wa Assisi alimchagua Mwenyezi Mungu kuwa ni dira na mwongozo wa maisha yake! Akajisadaka bila ya kujibakiza kwa ajili ya: Amani, huduma kwa maskini na utunzaji bora wa mazingira nyumba ya wote. Maamuzi yake magumu ya kuambata na kukumbatia ufukara, yalikuwa ni mwanzo wa mwono mpya wa uchumi, ambao bado ni mfano bora wa kuigwa. Kuna haja ya kuwekeza miongoni mwa vijana wa kizazi kipya, watakaokuwa wadau wa uchumi kwa siku za usoni. Ni muhimu sana kuwaandaa vijana watakaojisadaka kwa ajili ya huduma kwa Jumuiya zao sanjari na utunzaji bora wa mazingira nyumba ya wote; vijana wanaothamini utu, heshima, haki msingi za binadamu na udugu wa kibinadamu na kwamba, rasilimali fedha ni matokeo ya mambo hayo makuu.

Uchumi wa Francisko: Utunzaji Bora wa Mazingira Nyumba ya Wote
Uchumi wa Francisko: Utunzaji Bora wa Mazingira Nyumba ya Wote

Ni katika muktadha wa Uchumi wa Francisko, Baba Mtakatifu Francisko, Jumatatu tarehe 22 Januari 2024 amekutana na kuzungumza na washiriki wa Kongamano la Divai lililoandaliwa na Makampuni ya Vinitaly. Hawa ni wakulima na wazalishaji wa divai nchini Italia na kwamba, hawa wanaunda mtandao mkubwa wa wazalishaji na wauzaji wa divai nchini Italia. Kongamano hili pamoja na mambo mengine, limejadili kuhusu kanuni maadili na utu wema mintarafu maisha na utume wa Mtakatifu Francisko wa Assisi. Kumbe, ubora wa divai inayozalishwa ni muhimu sana kwa kuzingatia teknolojia ya uzalishaji na ubora wa ardhi mambo yanayohitaji umakini na uvumilivu mkubwa. Baba Mtakatifu anasema, tema hizi zote zimejadiliwa kwenye Maandiko Matakatifu: “Tazama, mkulima hungoja mazao ya nchi yaliyo ya thamani, huvumilia kwa ajili yake hata yatakapopata mvua ya kwanza na ya mwisho.” Yak 5:7. Lakini picha ambayo Kristo Yesu amewaachia wafuasi wake ni pale aliposema: “Mimi ndimi mzabibu wa kweli, na Baba yangu ndiye mkulima. Kila tawi ndani yangu lisilozaa huliondoa; na kila tawi lizaalo hulisafisha, ili lizidi kuzaa. Ninyi mmekwisha kuwa safi kwa sababu ya lile neno nililowaambia. Kaeni ndani yangu, nami ndani yenu. Kama vile tawi lisivyoweza kuzaa peke yake, lisipokaa ndani ya mzabibu; kadhalika nanyi, msipokaa ndani yangu. Mimi ni mzabibu; ninyi ni matawi, akaaye ndani yangu nami ndani yake, huyo huzaa sana; maana pasipo mimi ninyi hamwezi kufanya neno lo lote. Mtu asipokaa ndani yangu, hutupwa nje kama tawi na kunyauka; watu huyakusanya na kuyatupa motoni yakateketea. Yn 15:1-6.

Utunzaji wa mazingira unakita mizizi yake katika misingi ya haki na amani
Utunzaji wa mazingira unakita mizizi yake katika misingi ya haki na amani

Huu ni ujumbe makini katika maisha ya kiroho unaozingatia ukulima wa zabibu, lakini katika masuala ya kiteknolojia, maelezo haya yanakita mizizi yake katika hekima ya kibinadamu kwa kununua ardhi ya uzalishaji na hatimaye, kumhusisha mtu mzima katika utendaji wake wa kazi. Kumbe, kuna haja ya kuwa na matumizi sahihi ya rdhi, nguvu kazi, uzalishaji na ulaji wa mazao ya shamba; ujenzi wa mahusiano na mafungamano ya kijamii; utunzaji bora wa mazingira nyumba ya wote sanjari na kuendelea kujikita katika matendo adilifu ya kuthamini athari za kila tendo na uamuzi vinavyofanywa katika ulimwengu unaowazunguka. Kwa kuzingatia yote haya, jamii inaweza kuleta mabadiliko ya maana sana katika jamii. Rej. Laudato si 208. Masimulizi ya kale yaliyosheheni ishara, yanatoa ushuhuda wa imani ambayo waamini wote wanaishiriki, kwamba, kila kitu kinahusiana na kingine na kwamba matunzo halisi ya maisha ya binadamu na mahusiano yao na maumbile hayatengani na udugu, haki na uaminifu kwa wengine. Rej. Laudato si, 70. Baba Mtakatifu Francisko anakaza kusema divai, ardhi na shughuli za uzlishaji ni zawadi kutoka kwa Mungu na kwamba, binadamu amekabidhiwa tu kuilinda na kuitunza, kazi anayopaswa kuitekeleza kwa uaminifu kama chemchemi ya furaha ya kweli na hasa kwa maskini.

Divai
23 January 2024, 14:34