Tafuta

Papa Francisko: Ukweli Mbele ya Mungu na Ukweli Nafsini: Dhambi na Ufisadi

Jambo la msingi linalowekwa mbele ya waamini hapa ni ukweli mbele ya Baba yao na ukweli katika nafsi zao! Mtoto wa kwanza alikataa, wa pili alikosea, lakini akabaki kuwa mkweli mbele ya Baba yake, na mkweli nafsini mwake. Huu ni mwaliko kwa waamini kuchunguza dhamiri zao mbele ya Mwenyezi Mungu ikiwa kama wanaishi katika mwanga wa ukweli na ukarimu mbele ya Mungu, na kuendelea kujitahidi kufanya mapenzi ya Mungu katika safari ya maisha yao!

Na Padre Richard A. Mjigwa, C.PP.S. – Vatican.

Liturujia ya neno la Mungu, Dominika ya 26 ya Mwaka A wa Kanisa, Mwinjili Mathayo anaweka mbele ya waamini mfano wa wana wawili katika kutimiza mapenzi ya Baba yao. Wa kwanza alipoambiwa na Baba yake kwenda kufanya kazi katika shamba la mzabibu akajibu kwa haraka kwamba, anaenda, lakini asiende. Wa pili naye akamwambia vilevile, lakini akasema, “sitaki”; baadaye akatubu, akaenda! Rej. Mt 21:28-32. Kwa hakika kwenda kufanya kazi katika shamba la mzabibu kunahitaji moyo wa majitoleo na kujisadaka bila ya kujibakiza, licha ya kutambua kwamba, kama watoto wa mwenye shamba wanayo haki ya kurithi mali na utajiri wa Baba yao! Jambo la msingi linalowekwa mbele ya waamini hapa ni ukweli mbele ya Baba yao na ukweli katika nafsi zao! Mtoto wa kwanza alikataa, wa pili alikosea, lakini akabaki kuwa mkweli mbele ya Baba yake, na mkweli nafsini mwake. Hii ni sehemu ya tafakari iliyotolewa na Baba Mtakatifu Francisko, Dominika tarehe Mosi Oktoba 2023 wakati wa Sala ya Malaika wa Bwana kwenye Uwanja wa Kanisa kuu la Mtakatifu Petro mjini Vatican. Baba Mtakatifu anakaza kusema, mtoto wa kwanza alijibu kwamba, anaenda, lakini hakwenda, kwani hakukusudia kutoka moyoni mwake kutekeleza mapenzi ya Baba yake, wala hakutaka kujadiliana wala kuzungumza na Baba yake.

Kuna tofauti kati ya mdhambi na fisadi.
Kuna tofauti kati ya mdhambi na fisadi.

Ni mtoto aliyeficha ukweli na kutawaliwa na uvivu, ili kuficha uso wake. Kwa hakika mtoto wa kwanza hakuonesha utii wala heshima kwa Baba yake ingawa alikuwa huru kabisa kumwambia kwamba, hataki. Hizi ni dalili za mtenda dhambi na fisadi, kwa sababu ili kuficha hali yake ya kutotii, anakataa kuzama katika majadiliano na mazungumzano katika ukweli na uwazi. Mtoto wa pili aliyesema “hataki” lakini baadaye akatubu na kwenda shambani, si mkamilifu lakini ni mkweli kutoka nafsini mwake, ingawa ingependa tangu mwanzo kusema, “Nakwenda”, hapa anaonesha matokeo ya ujasiri wake, unaomwajibisha na kutenda ukweli katika mwanga angavu. Msingi huu wa ukweli unapelekea majadiliano yanayomrejesha katika hatua na njia sahihi. Kwa hakika ni mdhambi, lakini si fisadi. Ikumbukwe kwamba, kwa mdhambi daima kuna matumaini ya wokovu, lakini kwa fisadi kuna ugumu wake kutokana na unafiki pamoja na tabia yake ya kuficha ukweli, hali ambayo inampelekea kusutwa daima na dhamiri fuatizi!

Waamini wawe tayari kusema ukweli na kutekeleza mapenzi ya Mungu
Waamini wawe tayari kusema ukweli na kutekeleza mapenzi ya Mungu

Baba Mtakatifu Francisko anawaalika waamini pamoja na watu wote wenye mapenzi mema, kuchunguza dhamiri zao mbele ya matukio haya mawili, ili kuangalia ikiwa kama wanaishi maisha katika mwanga wa ukweli na ukarimu, kwa kuendelea kujitahidi kutekeleza mapenzi ya Mwenyezi Mungu, tayari kusema, “Ndiyo” hata kama “Ndiyo” hii ina gharama zake! Hata pale inaposhindikana kutekeleza mapenzi ya Mungu, waamini wawe waaminifu na wa kweli mbele ya Mungu, tayari kumwonesha udhaifu na mapungufu yao. Baba Mtakatifu anawauliza waamini, Je? Pale wanapoteleza na kuanguka dhambini, wako tayari kuanza mchakato wa toba na wongofu wa ndani? Au wanaendelea kujificha na kuona kwamba, mambo yote yako sawa, ili waonekane kama watu wema na wazuri. Kila mwamini ni mdhambi, lakini Je, katika maisha kuna ndago za ufisadi? Bikira Maria, kioo cha utakatifu, awasaidie waamini kuwa ni Wakristo wa kweli!

Papa Tafakari

 

01 October 2023, 14:38

Sala ya Malaika wa Bwana ni sala inayowakumbusha waamini Fumbo la Umwilisho na husaliwa mara tatu kwa siku: Saa 12:00 asubuhi, Saa 6:00 mchana na Saa 12:00, wakati ambapo kengele ya Sala ya Malaika wa Bwana hugongwa. Neno Malaika wa Bwana limetolewa kutoka katika Sala ya Malaika wa Bwana aliyempasha Bikira Maria kwamba, atamzaa Kristo Yesu na husaliwa Salam Maria tatu. Sala hii husaliwa na Papa kwenye Uwanja wa Kanisa kuu la Mtakatifu Petro wakati wa Jumapili na Wakati wa Siku kuu na Sherehe. Kabla ya Sala, Papa hutangulia kutoa tafakari akifanya rejea kwa Masomo ya siku. Baadaye kunafuatia salam kwa wageni na mahujaji. Kuanzia Sherehe ya Pasaka hadi Pentekoste, badala ya Sala ya Malaika wa Bwana, waamini husali Sala ya Malkia wa Bwana, sala inayokumbuka Ufufuko wa Kristo Yesu na mwishoni, husaliwa Sala ya Atukuzwe Baba mara tatu.

Sala ya Malaika wa Bwana/ Malkia wa Mbingu ya hivi karibuni

Soma yote >