Papa atoa salamu za rambi rambi kwa wahanga huko Benin
Vatican News
Katika Telegramu ya Papa Francisko, iliyotiwa saini na Kardinali Pietro Parolin, Katibu wa Vatican tarehe 26 Septemba 2023 akiielekeza kwa Askofu Aristide Gonsallo, wa Jimbo la Porto-Novo, mji mkuu wa Benin, huko Afrika Magharibi alibainisha kuwa Baba Mtakatifu alipata uchungu kufuatia na habari za moto wa kutisha katika eneno la Sèmè Kraké mnamo tarehe 23 Septemba 2023 na kupoteza maisha ya binadamu.” Kwa njia hiyo Papa “anaungana na familia zinazoomboleza, akielezea mshikamano wake na maumivu. Vile vile Papa anaombea roho za marehemu pumziko la amani huku akiwakabidhi katika huruma ya Mungu na kwa ajili ya kuponya waliojeruhiwa. Papa Francisko aliwakumbuka wale ambao kwa sasa wako karibu na waathirika wa moto huo na alimwomba Bikira Maria awape nguvu na faraja kwa wale wote ambao wameguswa na mkasa huu na aliomba baraka za Mungu kwa kila mtu na kwa taifa zima kama ishara ya faraja.
Mlipuko wa ghala la mafuta
Ajali ya Moto uliotokea Sèmè-Kraké, mji ulio kwenye mpaka kati ya Benin na Nigeria, ulisababishwa na mlipuko wa ghala la siri la mafuta yasiyojulikana(Ufisadi). Inasadikika kuwa ni watu 35 waliokufa, ikiwa ni pamoja na watoto wawili. Bohari hiyo, iliyoko karibu na jengo la Kanisa Katoliki la eneo hilo, ambalo liliharibiwa na moto huo ukasambaa na kuharibu magari kadhaa yaliyokuwa yameegeshwa karibu. Iliwachukua wazima moto masaa kumi kumaliza kuzima moto huo.