Tafuta

Papa Francisko: Ujio wa Roho Mtakatifu Mfariji, Msaidizi, Wakili na Jirani Mwema!

Roho Mtakatifu: Msaidizi anayeitwa awe jirani na msaada kwa wale watakao watuhumu na kuwashitaki. Ni jirani mwema, maana anakaa kwao naye yu ndani yao. Roho Mtakatifu si mgeni wa kupita, bali ni mwandani wa safari anayetamani kukaa katika nyoyo zao. Roho Mtakatifu ni mvumilivu hata pale waamini wanapoteleza na kuanguka, bado anaendelea kubaki kwa sababu anawapenda kweli kweli na kamwe hawezi kuwaacha katika mateso na mahangaiko ya ndani.

Na Padre Richard A. Mjigwa, C.PP.S. – Vatican.

Mababa wa Kanisa wanasema pale tu ilipotimia saa atakapotukuzwa Yesu anaahidi ujio wa Roho Mtakatifu, kwani kifo na ufufuko vitakuwa ni utimilifu wa ahadi waliyopewa Mababa: Roho wa kweli, Msaidizi mwingine atatolewa na Baba kwa ombi la Kristo Yesu; atatumwa na Baba kwa jina la Yesu; Yesu atampeleka atakapokuwa kwa Baba kwa sababu ametoka kwa Baba. Roho Mtakatifu atakuja, na waamini watamjua, atakuwa pamoja nao daima, atawafundisha kila kitu, na kuwakumbusha yote aliyosema Kristo Yesu, naye atatoa ushuhuda. Atawaongoza waamini kwenye kweli yote na atamtukuza Kristo Yesu; atauhakikishia ulimwengu juu ya dhambi, haki na hukumu. Rej. KKK. 729. Liturujia ya Neno la Mungu Dominika ya Sita ya Kipindi cha Pasaka inamzungumzia Roho Mtakatifu, ambaye Kristo Yesu anamwita “Msaidizi,” kadiri ya maana ya neno “Yule ambaye anaitwa awe jirani,” Wakili (Advocatus) na Mfariji, Kristo Yesu akiwa ndiye Mfariji wa kwanza. Bwana Mwenyewe anamwita Roho Mtakatifu kuwa ni Roho wa kweli. Rej. KKK. 692. Baba Mtakatifu Francisko wakati wa Sala ya Malkia wa Mbingu kwenye Uwanja wa Kanisa kuu la Mtakatifu Petro mjini Vatican, Dominika tarehe 14 Mei 2023 amemtafakari Roho Mtakatifu: Msaidizi anayeitwa awe jirani na msaada kwa wale watakao watuhumu na kuwashitaki.

Waamini wakihudhuria Sala ya Malkia wa Mbingu mjini Vatican
Waamini wakihudhuria Sala ya Malkia wa Mbingu mjini Vatican

Roho Mtakatifu ni jirani mwema, maana anakaa kwao naye yu ndani yao. Roho Mtakatifu si mgeni wa kupita, bali ni mwandani wa safari anayetamani kukaa katika nyoyo za waamini. Roho Mtakatifu ni mvumilivu hata pale waamini wanapoteleza na kuanguka, bado anaendelea kubaki kwa sababu anawapenda kweli kweli na kamwe hawezi kuwaacha katika mateso na mahangaiko ya ndani. Roho Mtakatifu ni Mfariji wakati wa majaribu, mahangaiko na mateso, ndiye anayewaletea waamini msamaha na nguvu ya Mungu; anayewasahihisha kwa upole, huruma na upendo. Roho Mtakatifu Mfariji ni rafiki wa kweli na ni mwaminifu anayewafunza waamini yale mambo ya kubadili, ili hatimaye, waweze kukua. Ni Roho ambaye ni mnyenyekevu hata pale anapowasahihisha waja wake, anafanya hivyo kwa upole, bila kuondoa imani kwao, bali anawapatia uhakika kuhusu uwepo na ukaribu wa Mungu. Baba Mtakatifu anakaza kusema, Roho Mtakatifu Mfariji kama Wakili na mtetezi mbele ya watu wanaowashutumu, kiasi cha kuonekana kuwa “si mali kitu” mbele ya walimwengu na mshitaki wa ndugu zao, yeye awashitakiye mbele ya Mungu wao mchana na usiku amefanya yote ili wajisikie watu wasiokuwa na furaha wala uwezo. Lakini mbele ya shutuma na mashitaka yote haya, Roho Mtakatifu Mfariji, atawafundisha yote, na kuwakumbusha yote waliyoambiwa na Kristo Yesu.

Roho Mtakatifu Mfariji, ni Msaidizi, Wakili na Jirani mwema
Roho Mtakatifu Mfariji, ni Msaidizi, Wakili na Jirani mwema

Kumbe, wataweza kumjibu Shetani, Ibilisi kwa maneno ya Kristo Yesu aliyekuwa anazungumza na Baba yake wa mbinguni, aliyewawezesha watoto wake kulifahamu pendo lake. Baba Mtakatifu Francisko anatoa mwaliko kwa waamini kumwomba, kumpokea na kukumbuka ukweli muhimu wa maisha kwamba, ni Yeye anayewalinda waamini dhidi ya shutuma na mashitaka kwa sababu wao ni watoto wapendwa wa Mungu. Jambo la kujiuliza ni kiwa kama waamini wamejenga mazoea na utamaduni wa kumwomba daima Roho Mtakatifu, kiasi cha kumsahau kwamba, ni jirani na kwamba yuko ndani mwao! Je, waamini wamekuwa makini kusikiliza sauti yake na tayari kujirekebisha pale anapowarekebisha? Je, wanaposhutumiwa katika maisha, wanajbu kwa kutumia maneno la Kristo Yesu! Je, wanakumbuka kwamba, wao ni watoto wapendwa wa Mungu? Bikira Maria awasaidie kuwa wanyenyekevu kwa sauti ya Roho Mtakatifu sanjari na kutambua uwepo wake wa daima.

Papa Roho Mfariji

 

14 May 2023, 14:56

Sala ya Malkia wa Mbingu ni nini?
 

Utenzi wa Malkia wa Mbingu ni kati ya tenzi nne za Bikira Maria (nyingine ni:Tunakimbilia Ulinzi wako,  Salam Malkia wa Mbingu, Salam Malkia). Kunako mwaka 1742, Papa Benedikto XIV alipoandika kwamba, waamini wasali Sala ya Malkia wa Mbingu wakiwa wamesimama, kama alama ya ushindi dhidi ya kifo, wakati wa Kipindi cha Pasaka, yaani kuanzia Domenika ya Ufufuko wa Bwana hadi Sherehe ya Pentekoste. Hii ni Sala ambayo husaliwa mara tatu kwa siku kama ilivyo pia Sala ya Malaika wa Bwana: Asubuhi, Mchana na Jioni ili kuweka wakfu Siku kwa Mwenyezi Mungu na Bikira Maria.

Utenzi huu kadiri ya Mapokeo ulianza kutumika kunako karne ya VI au Karne X, lakini kuenea kwake kunaanza kujitokeza katika nyaraka mbali mbali kati kati ya Karne ya XIII, ilipoingizwa kwenye Kitabu cha Sala za Kanisa cha Wafranciskani. Hii ni Sala inayoundwa na maneno mafupi manne yanayohitimishwa na Alleluiya na sala ya waamini wanaomwelekea Bikira Maria, Malkia wa mbingu, ili kufurahia pamoja naye kuhusu Fumbo la Ufufuko wa Kristo Yesu.

Papa Francisko tarehe 6 Aprili 2015 wakati wa Sala ya Malkia wa Mbingu, siku moja baada ya Sherehe ya Pasaka, aliwashauri waamini kuwa na moyo wa furaha wanaposali sala hii. “Tunamwendea Bikira Maria, tukimwomba afurahi, kwa sababu yule Mwanaye mpendwa aliyekuwa amemchukua mimba amefufuka kweli kweli kama alivyosema; tunajiaminisha kwa sala na maombezi ya Bikira Maria. Kimsingi furaha yetu ni mwangi wa furaha ya Bikira Maria kwani ndiye aliyetunza na anaendelea kutunza matukio mbali mbali ya maisha ya Yesu. “Tusali sala hii kwa furaha ya kuwa waana wa Mungu ambao wanafurahi kwa sababu Mama yao anafurahi”

 

Sala ya Malaika wa Bwana/ Malkia wa Mbingu ya hivi karibuni

Soma yote >