Tafuta

Papa Francisko Sherehe ya Pentekoste: Pokeeni Roho Mtakatifu: Ushuhuda!

Roho Mtakatifu ndiye aliyewaondolea wanafunzi wa Yesu ule woga, na kuwakirimia neema ya kutoka nje ili kumtangaza na kumshuhudia Kristo Yesu kwa ujasiri na moyo mkuu. Mateso na kifo cha Kristo Yesu kiliwavuruga wanafunzi wake, kiasi cha kujifungia! Hiki ni kielelezo hata cha waamini wanapokabiliana na matatizo na changamoto za maisha, kiasi cha kukosa tena ile fadhila ya matumaini na ujasiri wa kusonga mbele kwa ari na moyo mkuu kwa kutawaliwa na hofu kuu

Na Padre Richard A. Mjigwa, C.PP.S. – Vatican.

Sherehe ya Pentekoste: Wanafunzi wanamwona Kristo Yesu Mfufuka: Ikawa jioni, siku ile ya kwanza ya juma, pale walipokuwapo wanafunzi, milango imefungwa kwa hofu ya Wayahudi; akaja Yesu, akasimama katikati, akawaambia, Amani iwe kwenu. Naye akiisha kusema hayo, akawaonyesha mikono yake na ubavu wake. Basi wale wanafunzi wakafurahi walipomwona Bwana. Basi Yesu akawaambia tena, Amani iwe kwenu; kama Baba alivyonituma mimi, mimi nami nawapeleka ninyi. Naye akiisha kusema hayo, akawavuvia, akawaambia, Pokeeni Roho Mtakatifu. Wo wote mtakaowaondolea dhambi, wameondolewa; na wo wote mtakaowafungia dhambi, wamefungiwa. Yn 20:19-23. Baba Mtakatifu Francisko wakati wa Sala ya Malkia wa Mbingu, Sherehe ya Pentekoste, Dominika tarehe 28 Mei 2023 amesema, sehemu hii ya Injili inawaonesha Mitume walivyokuwa wamejifungia ndani kwa hofu ya Wayahudi, baada ya mateso na kifo cha Kristo Yesu, akawatokea na kuwapatia zawadi ya Roho Mtakatifu: “Pokeeni Roho Mtakatifu.” Kumbe, Roho Mtakatifu ndiye aliyewaondolea wanafunzi wa Yesu ule woga, na kuwakirimia neema ya kutoka nje ili kumtangaza na kumshuhudia Kristo Yesu kwa ujasiri na moyo mkuu. Mateso na kifo cha Kristo Yesu kiliwavuruga wanafunzi wake, kiasi cha kujifungia! Baba Mtakatifu amekita tafakari yake kwa kitenzi hiki cha “kujifungia ndani” akiuliza ni mara ngapi waamini wamejikuta wakijifungia ndani katika ubinafsi wao wanapokumbana na hali tete na magumu ya maisha binafsi au kifamilia?

Roho Mtakatifu anawaondolea waamini hofu.
Roho Mtakatifu anawaondolea waamini hofu.

Wakati wanakumbana na mateso na mahangaiko kiasi hata cha kukosa tena fadhila ya matumaini na ujasiri wa kusonga mbele kwa ari na moyo mkuu. Kama ilivyokuwa kwa Mitume wa Yesu, waamini wanajikuta wakijifungia katika undani wa maisha na wasi wasi wao. Hii ina maana ya kwamba, mwamini anatoa nafasi kubwa kwa woga na wasi wasi kumtawala na hivyo kujikuta akijifungia katika undani wake. Hofu ya kushindwa kutekeleza, hofu ya kumkuta mwamini akiwa pweke mbele ya mapambano ya maisha ya kila siku, hofu ya kubaki huku akiwa ameshindwa kumudu mapambano ya maisha au kufanya maamuzi tenge. Woga unaposhika kasi, unamkandamiza muhusika na hivyo kushindwa kujinasua na hivyo kujikuta akiwa mpweke: Hivi ndivyo inavyotokea hata kwa wageni au watu waliotafuti na wanavyofikiri na kutenda tofauti. Baba Mtakatifu anakaza kusema, kunawezekana kukawepo na woga hata dhidi ya Mwenyezi Mungu, kwa kumwona kuwa ni katili anayeadhibu! Ikiwa kama waamini watatoa kipaumbele cha pekee kwa hofu, woga na wasi wasi wa namna hii kutawala, kwa hakika milango yao itakuwa imefungwa: nyoyo zao, jamii na hata mlango wa Kanisa kwao, utafungwa na hii ni hatari sana kwa maisha ya kiroho. Kristo Mfufuka anawapatia Mitume zawadi ya Roho Mtakatifu anayewaokoa kutoka katika kifungo cha hofu, woga na wasi wasi.

Roho Mtakatifu anawakirimia waamini ujasiri wa kumtangaza na kumshuhudia Yesu
Roho Mtakatifu anawakirimia waamini ujasiri wa kumtangaza na kumshuhudia Yesu

Mitume walipompokea Roho Mtakatifu siku ile ya Pentekoste ya kwanza, wakatoka kimasomaso kutangaza na kushuhudia Habari Njema ya Wokovu. Ni kwa njia ya Roho Mtakatifu, Mitume wanashinda hofu, woga na wasi wasi na malango yanafunguka, ili kuonja ukaribu na upendo wa Mungu unaofariji, unaoangaza, unaoshinda magumu, woga na hofu ya maisha. Baba Mtakatifu Benedikto XVI anasema Roho wa Mungu anapoingia anafukuzia mbali woga na kuwajalia waamini kujisikia kwamba, wako mikononi salama mwa Mwenyezi Mungu, mwingi wa upendo na hata chochote kile kikitokea lakini upendo wa Mungu utawalinda na kuwaokoa. Kumbe, waamini wanapokabiliwa na changamoto za hofu, wasiwasi na kutaka kujifungia katika ubinafsi wao, wamwombe Roho Mtakatifu kwa ajili yao wenyewe, kwa ajili ya Kanisa na kwa ajili ya ulimwengu mzima, ili Pentekoste mpya iwashukie na hivyo kufukuzia mbali hofu inayowasonga nyoyoni mwao, ili hatimaye, waweze kuishi ule moto wa upendo wa Mungu. Bikira Maria aliyekuwa wa kwanza kujazwa na Roho Mtakatifu, awaombee waamini.

 

 

 

 

28 May 2023, 14:24

Sala ya Malkia wa Mbingu ni nini?
 

Utenzi wa Malkia wa Mbingu ni kati ya tenzi nne za Bikira Maria (nyingine ni:Tunakimbilia Ulinzi wako,  Salam Malkia wa Mbingu, Salam Malkia). Kunako mwaka 1742, Papa Benedikto XIV alipoandika kwamba, waamini wasali Sala ya Malkia wa Mbingu wakiwa wamesimama, kama alama ya ushindi dhidi ya kifo, wakati wa Kipindi cha Pasaka, yaani kuanzia Domenika ya Ufufuko wa Bwana hadi Sherehe ya Pentekoste. Hii ni Sala ambayo husaliwa mara tatu kwa siku kama ilivyo pia Sala ya Malaika wa Bwana: Asubuhi, Mchana na Jioni ili kuweka wakfu Siku kwa Mwenyezi Mungu na Bikira Maria.

Utenzi huu kadiri ya Mapokeo ulianza kutumika kunako karne ya VI au Karne X, lakini kuenea kwake kunaanza kujitokeza katika nyaraka mbali mbali kati kati ya Karne ya XIII, ilipoingizwa kwenye Kitabu cha Sala za Kanisa cha Wafranciskani. Hii ni Sala inayoundwa na maneno mafupi manne yanayohitimishwa na Alleluiya na sala ya waamini wanaomwelekea Bikira Maria, Malkia wa mbingu, ili kufurahia pamoja naye kuhusu Fumbo la Ufufuko wa Kristo Yesu.

Papa Francisko tarehe 6 Aprili 2015 wakati wa Sala ya Malkia wa Mbingu, siku moja baada ya Sherehe ya Pasaka, aliwashauri waamini kuwa na moyo wa furaha wanaposali sala hii. “Tunamwendea Bikira Maria, tukimwomba afurahi, kwa sababu yule Mwanaye mpendwa aliyekuwa amemchukua mimba amefufuka kweli kweli kama alivyosema; tunajiaminisha kwa sala na maombezi ya Bikira Maria. Kimsingi furaha yetu ni mwangi wa furaha ya Bikira Maria kwani ndiye aliyetunza na anaendelea kutunza matukio mbali mbali ya maisha ya Yesu. “Tusali sala hii kwa furaha ya kuwa waana wa Mungu ambao wanafurahi kwa sababu Mama yao anafurahi”

 

Sala ya Malaika wa Bwana/ Malkia wa Mbingu ya hivi karibuni

Soma yote >