Tafuta

Papa Francisko: Dibaji ya Kitabu "Ladha ya mabadiliko - Mpito wa Kiikolojia Kama Njia ya Furaha" Papa Francisko: Dibaji ya Kitabu "Ladha ya mabadiliko - Mpito wa Kiikolojia Kama Njia ya Furaha"   (AFP or licensors)

Ladha ya Mabadiliko: Mpito wa Kiikolojia Kama Njia ya Furaha

Baba Mtakatifu Francisko katika dibaji ya kitabu anasema, Kitabu hiki kinatoa imani na matumaini, dhamana na wajibu wa vijana wa kizazi kipya; umuhimu wa kufanya mabadiliko katika mtindo wa maisha, ili kuheshimu na kujikita katika mchakato wa matumizi bora ya mazingira nyumba ya wote. Mwelekeo wa uchumi hauna uwiano mzuri kwa maskini na ni uchumi ambao ni hatari kwa mazingira. Vijana wafundwe kuhusu umuhimu wa majadiliano katika ukweli na uwazi.

Na Padre Richard A. Mjigwa, C.PP.S. – Vatican.

Dibaji ya Kitabu "Ladha ya mabadiliko - Mpito wa Kiikolojia Kama Njia ya Furaha" kilichoandikwa na: Gaël Giraud na Carlo Petrini. Baba Mtakatifu Francisko katika utangulizi wa kitabu hiki anasema, kimemwamshia ndani mwake hamu ya matumaini na ukweli kwa siku zijazo. Je, tunataka ulimwengu unaounga mkono zaidi au kidogo? Wananchi wa vyama vya ushirika au ushindani? Idadi ya watu wenye ubinafsi au wabinafsi? Jambo kuu katika maisha yetu sio tunamiliki magari mangapi, lakini ubora wa mahusiano kati yetu, asili na watoto wetu ndiyo mambo ya msingi zaidi wanaandika Gaël Giraud na Carlo Petrini ambao wamechangia kwa kiasi kikubwa makala kwenye Jarida la “La Civiltà Cattolica” makala kuhusiana na masuala ya kiuchumi, fedha pamoja na mabadiliko ya tabianchi. Kitabu kinazungumzia kuhusu utunzaji bora wa mazingira nyumba ya wote, unaotoa imani kwa watu wa nyakati hizi na kuonesha madhara ya uharibifu wa mazingira katika maisha ya mwanadamu. Kitabu hiki kinatoa imani na matumaini, dhamana na wajibu wa vijana wa kizazi kipya; umuhimu wa kufanya mabadiliko katika mtindo wa maisha, ili kuheshimu na kujikita katika mchakato wa matumizi bora ya mazingira nyumba ya wote. Mwelekeo wa uchumi hauna uwiano mzuri kwa maskini na ni uchumi ambao ni hatari kwa mazingira. Kumbe, kuna haja ya kufanya maamuzi magumu kuhusu chakula, usafiri na ulaji katika ujumla wake. Makundi makubwa ya vijana sehemu mbalimbali za dunia wanaendelea kuhamasisha haki ya mazingira na haki jamii, mambo yanayotegemeana na kukamilishana katika ukweli wake. Si haki wala sawa kupima ustawi na maendeleo ya uchumi kwa kigezo cha pato ghafi la taifa. Hii inatokana na ukweli kwamba, kazi nyingi zinazofanywa na wanawake majumbani haiziingizwi katika Pato Ghafi la Taifa na kwamba, mchango wa binadamu katika kukuza na kudumisha uchumi hautiliwi maanani kabisa, kwa kuzingatia kigezo cha faida.

Kitabu kinazungumzia utunzaji bora wa mazingira nyumba ya wote
Kitabu kinazungumzia utunzaji bora wa mazingira nyumba ya wote

Baba Mtakatifu Francisko anasema, kitabu "Ladha ya mabadiliko - Mpito wa Kiikolojia Kama Njia ya Furaha" kimeandikwa kwa mtindo wa majadiliano na maongezi ili kutafuta na hatimaye kuweza kuambata ukweli ambao kwa Wakristo ni Yesu mwenyewe. Vijana wa kizazi kipya wanapaswa kuelimishwa na kufundwa kuhusu umuhimu wa watu kukutana na kujadiliana kwa ajili ya ustawi, maendeleo na mafao ya wengi badala ya tabia ya watu wachache kutaka kukumbatia na kueneza ukweli. Waandishi hawa wawili Gaël Giraud anajitambulisha kuwa ni mtu asiye amini kwa Mungu na Carlo Petrini ni Myesuit, lakini licha ya tofauti zao msingi, lakini bado wanaweza kukutana na kuzungumza kama sehemu ya ujenzi wa mazingira bora nyumba ya wote. Kuna heri kubwa kutoa kuliko kupokea. Ujenzi wa udugu wa kibinadamu unawawezesha watu kuishi kwa umoja na maelewano na hivyo ulimwengu unakuwa ni mahali pa salama kwa ajili ya watu wote, bila kujali imani ya mtu awaye yote. Hii ni sehemu ya mchakato wa ujenzi wa udugu wa kibinadamu na urafiki wa kijamii, ili kujenga na kudumisha mahusiano na mafungamano katika ngazi ya mtu binafsi, jumuiya na hata kisiasa. Uchumi unaoangamiza umekuwa ni sababu yak ilio na mateso kwa “maskini na akina yakhe pangu pakavu tia mchuzi!” Leo hii habari zinazotawala kwenye vyombo vya mawasiliano ya jamii ni: Ukame wa kutisha, maafa na majanga asilia, uhamiaji wa shuruti kutokana na athari za mabadiliko ya tabianchi! Yote haya ni matukio ambayo mwanadamu anapaswa kuchukua hatua madhubuti, kulinda, kutunza na kuendeleza kazi ya Uumbaji.

Mpito wa Kiikolojia kama njia ya furaha
Mpito wa Kiikolojia kama njia ya furaha

Maendeleo makubwa ya uchumi yamesababisha mabadiliko makubwa ya tabianchi na athari zake zinajionesha miongoni mwa maskini hususan Barani Afrika! Baba Mtakatifu Francisko anasema, sera na mbinu mkakati wa Kanisa Katoliki katika huduma kwa wakimbizi na wahamiaji inajikita katika mambo makuu manne yaani: “Kuwapokea, kuwalinda, kuwaendeleza na kuwahusisha wakimbizi na wahamiaji” katika maisha ya jamii inayowapokea na kuwapatia hifadhi na usalama wa maisha! Wakimbizi na wahamiaji ni watu wanaotafuta usalama, hifadhi na maisha bora zaidi. Kwa hakika kitabu "Ladha ya mabadiliko - Mpito wa Kiikolojia Kama Njia ya Furaha" kilichoandikwa na: Gaël Giraud na Carlo Petrini ni zawadi muhimu sana inayoonesha njia muafaka za kufuata katika ngazi ya mtu binafsi, jumuiya na kama taasisi katika mabadiliko ya kiikolojia kwa kila mtu kuwajibika katika kulinda na kutunza mazingira bora nyumba ya wote, kwa kupunguza ulaji wa kupindukia, kwa kukuza na kunogesha mahusiano na mafungamano ya kijamii ni mambo yatakayowawezesha watu kufikia lango la furaha ya kweli ya maisha!

Papa Kitabu Ikolojia
23 May 2023, 14:10