Papa Francisko:Rais wa Falme za Uarabuni alikuwa mtu wa mazungumzo
Na Angella Rwezaula – Vatican.
Papa Francisko anasema kuhuzunishwa na kifo cha Sheikh Khalifa Bin Zayed Al Nahyan, aliyekuwa Rais wa Umoja wa Falme za Kiarabu na Mfalme wa Abu Dhabi, aliyefariki tarehe 13 Mei 2022 iliyopita. Katika ujumbe wa salamu za rambirambi, Papa anatoa rambirambi na maombi, huku akitoa heshima kwa uongozi wake uliotukuka na wenye kuona mbali katika utumishi wa taifa lake.
Papa pia anakumbuka umakini wake Sheikh kwa Vatican na jumuiya za Kikatoliki za Emirates(wanaoishi katika falme za kiarabu)lakini pia kujitoa kwake kwa maadili ya mazungumzo, kuelewana na mshikamano kati ya watu na tamaduni za kidini iliyotangazwa kwa dhati na Hati ya kihistoria ya Abu Dhabi na iliyojumuishwa na Tuzo la Zayed kuhusu Udugu wa Kibinadamu .
Matumaini ya Papa Francisko ni kwamba urithi wake utaendelea kuhamasisha juhudi za wanaume na wanawake wenye mapenzi mema kila mahali, ili kudumu katika kusuka vifungo vya umoja na amani kati ya wanafamilia moja ya kibinadamu. Hatimaye, katika salamu hizo Papa Francisko amemhakikishia maombi yake Sheikh Mohammed bin Zayed Al Nahyan, kwa familia yake na watu wote wapendwa wa Falme za Kiarabu.