Tafuta

Papa Francisko wakati wa hija yake ya kitume nchini Ugiriki amekutana na kuzungumza na Wayesuit wanaotekeleza dhamana na utume wao nchini Ugiriki. Papa Francisko wakati wa hija yake ya kitume nchini Ugiriki amekutana na kuzungumza na Wayesuit wanaotekeleza dhamana na utume wao nchini Ugiriki. 

Mahojiano Maalum Kati ya Papa Francisko Na Wayesuit Nchini Ugiriki

Papa aligusia kuhusu: Mchango wa Mabruda, Kipaji cha ubunifu, Uhaba wa miito ndani ya Kanisa; Changamoto ya majadiliano ya kidini na kiekumene. Ameangalia huduma kwa wakimbizi na wahamiaji, kielelezo cha unyenyekevu, tayari kutimiza mapenzi ya Mungu katika maisha yao kwa ari na moyo wa unyenyekvu na mwishoni ni kuhusu Mtandao wa Utume wa Sala Kimataifa.

Na Padre Richard A. Mjigwa, C.PP.S. – Vatican.

Mwaka wa Mtakatifu Inyasi wa Loyola kuanzia tarehe 20 Mei 2021 hadi 31 Julai 2022 ni fursa ya kushirikiana na wadau mbalimbali katika maisha na utume wa Wayesuit, ili kuweza kuyapatanisha yote na Kristo Yesu, anayepaswa kupewa kipaumbele cha kwanza! Maadhimisho haya yananogeshwa na kauli mbiu “Angalieni mambo yote mapya katika Kristo”. Mwaka huu unaongozwa na Mpango Mkakati wa Maisha na Utume wao katika kipindi cha miaka kumi yaani kuanzia mwaka: 2019-2029. Ni katika muktadha huu, Baba Mtakatifu Francisko kuanzia tarehe 4-6 Desemba 2021 alifanya hija ya kitume nchini Ugiriki kwa kunogeshwa na kauli mbiu “Jiwekeni Wazi Kwa Mshangao wa Mungu.” Akiwa nchini Ugiriki, Baba Mtakatifu Francisko Jumamosi tarehe 4 Desemba 2021 alipata nafasi ya “kuchonga na Wayesuit kwa muda wa saa moja na kugusia mchango wa Mabruda katika maisha na utume wa Kanisa, Kipaji cha ubunifu, Uhaba wa miito ndani ya Shirika la Wayesuit; Changamoto ya majadiliano ya kidini na kiekumene. Amegusia huduma kwa wakimbizi na wahamiaji inayosimikwa katika unyenyekevu, tayari kutimiza mapenzi ya Mungu katika maisha yao kwa ari na moyo wa unyenyekvu na mwishoni ni kuhusu mtandao wa utume wa Sala Kimataifa. Baba Mtakatifu anasema, Mabruda ni watu wanaojitahidi kufahamu mambo msingi katika maisha, kwani wana uwezo wa kuunganisha mahusiano na utume wao katika maisha ya kila siku.

Mabruda ni watu wanaopambana na changamoto na kuzipatia ufumbuzi makini. Wito wa wale wanaotaka kujisadaka katika maisha ya Kipadre na Kitawa unapaswa kupimwa si tu kwa kigezo cha akili darasani, bali pia uwezo wa kuweka kwa vitendo kile alichojifunza darasani sanjari na kunogesha mahusiano na mafungamano mema ya kijamii. Kipaji cha ubinifu anasema Baba Mtakatifu Francisko, kiwasaidie watu wa Mungu kusoma alama za nyakati na kuanzisha utume, ambao kimsingi ni kwa ajili ya Kristo Yesu na Kanisa lake. Waasisi wa utume huu, wawe tayari kukaa pembeni na kuangalia mapya na maboresho yanayoweza kufanywa na watu wengine, kwani utume ni kazi ya Kristo Yesu na kamwe wasielemewe na kishawishi cha kugeuza miradi au utume huu kuwa ni mali na utambulisho binafsi. Viongozi watambue mambo msingi yanayopaswa kuendelezwa mintarafu Katiba ya Shirika baada ya kufanya mang’amuzi ya kina. Wayesuti wataendelea kushiriki katika mchakato wa majadiliano ya kidini, kiekumene na kitamaduni kwa ajili ya ustawi, maendeleo na mafao ya wengi, daima wakijitahidi kusoma alama za nyakati. Wanapaswa kuzingatia pia idadi ya Wayesuit waliopo!

Kwa sasa Mashirika mengi ya kitawa na kazi za kitume yanakabiliwa na changamoto ya upungufu wa miito na idadi kubwa ya Mapadre na Watawa wenye umri mkubwa. Upungufu wa miito iwe ni fursa ya kujikita katika toba, wongofu wa ndani na unaosimikwa katika unyenyekevu, ili kujifunza kugundua kile ambacho Mwenyezi Mungu anataka kutoka katika undani wa maisha yao. Mapadre na watawa wawe waaminifu kwa Kristo Yesu na Kanisa lake. Watekeleze dhamana na nyajibu zao kwa furaha, amani na utulivu wa ndani, ili hatimaye, waweze kuwa ni wimbo mzuri wa sifa na shukrani kwa Mungu. Wajitahidi kuwa ni wafuasi, vyombo na mashuhuda wema, watakatifu na waaminifu kwa Kristo Yesu na Kanisa lake. Licha ya udhaifu wao wa kibinadamu lakini wajitahidi kuwa ni vyombo vya furaha ya Injili na huduma kwa watu wa Mungu. Mapadre na watawa wajifunze kujisadaka bila kujibakiza kwa ajili ya huduma kwa watu wa Mungu, wakitambua kwamba, mwisho wa maisha yo hapa duniani watahukumiwa kutokana na matendo ya huruma waliyobahatika kutenda katika maisha. Wajiandae kushangazwa na mpango wa Mungu katika maisha yao.

Baba Mtakatifu Francisko tarehe 27 Machi 2018 aliidhinisha Katiba Mpya ya Mtandao wa Utume wa Sala Kimataifa kama sehemu ya utume wa Kipapa na makao yake makuu yakahamishiwa mjini Vatican. Kwa miaka mingi, Utume wa Sala umekuwa ukiratibiwa na Wayesuit, kwa kuandaa na kusambaza Nia za Baba Mtakatifu kwa kila mwezi. Baba Mtakatifu akamteuwa Padre Frédéric Fornos, SJ., kuwa Mkurugenzi wa Mtandao wa Utume wa Sala Kimataifa. Utume wa Sala umeenea katika nchi 98 duniani na unashirikiana kwa karibu sana na Chama cha Kitume cha Vijana wa Ekaristi. Mtandao wa Utume wa Sala pamoja na mambo mengine unajihusisha kikamilifu katika kuandaa picha za video zinazonogesha Nia za Baba Mtakatifu kwa kila mwezi (www.ilvideodelpapa.org) pamoja na Jukwaa la Sala kwa ajili ya utume wa Kanisa. Sala inapaswa kupewa kipaumbele cha pekee katika maisha na utume wa Kanisa.

Papa Wayesuit Ok
18 December 2021, 16:39