Papa Francisko:Uharibifuu wa mazingira ya binadamu ni jambo zito sana!
Na Sr. Angela Rwezaula- Vatican
Uharibifu wa mazingira ya wanadamu ni jambo zito sana, si tu kwa sababu Mungu alitukabidhi ulimwengu, lakini pia kwa sababu maisha yenyewe ya mwanadamu ni zawadi na lazima kulindwa. Ndiyo ujumbe wa Papa Francisko katika mitandao ya kijamii Alhamisi, tarehe 24 Septemba 2020. Katika muktadha wa Kipindi cha kazi ya uumbaji ambacho ni matashi ya Papa Francisko kilichoanza tangu tarehe Mosi Septemba na kitahitimishwa tarehe 4 Oktoba 2020, sambamba na siku kuu ya Mtakatifu Francis wa Assisi mtawa wa Kifranciskani na mtetezi mkuu wa mazingira. Ujumbe wake ni kuhamasisha zaidi juu ya Wosia wake wa kitume, “Laudato si”, yaani “Sifa iwe kwako” kuhusu utunzaji bora wa nyumba yetu ya pamoja.
Katika Wosia wake, Laudato si, Papa anakazia sana juu ya utunzaji bora wa mazingira na kwamba ni changamoto inayojikita katika misingi ya haki, amani na mshikamano kwa sababu mazingira ni sehemu muhimu sana ya maisha ya mwanadamu. Papa anabainisha kwamba utunzaji wa uumbaji ni kazi ya huruma na kuitunza nyumba yetu ya pamoja inadai au inatupasa kuitafakari kazi ya uumbaji kwa moyo wa shukrani, na katika kukeleza hilo basi mwanadamu atakuwa amekuwa chombo cha huruma kwa wengine. Hata hivyo kila kitu katika mazingira ya ulimwengu huu pamoja na viumbe vyake vinasukana na hutegemeana hivyo huitaji wa upendo na utunzaji, ni muhimu na ambapo limapatia mwanadamu yale mamlaka ya kutunza mazingira pamoja na viumbe vyote vya angani na majini na hatimaye kuweza kumsifu na kumeudishia Mungu aliyeviumba.
Papa Francisko katika Waraka wake wa Lauda Si aidha anabainisha kuwa utunzaji wa mfumo wa ikolojia unadai kuwa na hekima ya kuona mbali kwa sababu hakuna mtu mwenye kutafuta faida ya haraka haraka anayenuia kuulinda mfumo wa ikolojia. Lakini Gharama za uharibifu zinazosababaishwa na ukosefu wa uwajibikaji ni kubwa zaidi kuliko faida za kiuchumi zinazoweza kupatikana. Pale ambapo spishi fulani zinaharibiwa au kudhurika, gharama zinazohusika hazikadiriki. Tutakuwa mashihidi wa dhuluma zinazotendeka endapo tunafikiri kwamba tutapata faida kubwa kwa kuwafanya watu wote wa kizazi hiki na cha baadaye kulipa gharama kubwa mno za uharibifu wa mazingira.