Tafuta

2020.05.24 Bikira Maria  Sheshan, nchini China 2020.05.24 Bikira Maria Sheshan, nchini China 

Papa kwa waamini wa China:Muwe na nguvu katika imani na ushuhuda wa matumaini!

Mara baada ya tafakari na sala la Malkia wa Mbingu tarehe 24 Mei Papa Francisko ametoa salam kwa Wakatoliki wa China ambao wanafanya Siku kuu ya Bikira Maria Msaada wa Wakristo na Msimamizi wa China na anayeheshimiwa katika Madhabahu ya Sheshan huko Shanghai.

Na Sr. Angela Rwezaula- Vatican

Papa Francisko tarehe 24 Mei 2020 ambapo Mama Kanisa anaadhimisha Siku Kuu ya Kupapa kwa Bwana, mara baada ya sala ya Malkia wa Mbingu  amewakabidhidi waamini wa nchi ya  China kwa Bikira Maria katika siku ambayo wanasheherekea  Bikira Maria Msaada wa wakristo. Papa amesema  “Kwa Mama wa mbinguni tumkabidhi kuongoza na kulinda  wachungaji na waamini wa Kanisa Katoliki katika Nchi kubwa hiyo,kwa sababu waweze kuwa  na nguvu katika imani na kidete katika muungano kidugu, mashuhuda wa furaha na wahamasishaji wa upendo na matumaini, udugu na uraia mwema”.

Papa Francisko amesema, “wakatoliki nchini China ninapenda kuwahakikishia kuwa Kanisa la ulimwengu ambao nanyi ni sehemu yake, mnashirikishana matumaini na kuwasaidia katika majaribu. Kanisa linawasindikiza kwa sala kwa ajili ya uvuvio wa Roho Mtakatifu ili nanyi mpate kuangazwa na mwanga na uzuri wa Injili, nguvu ya Mungu kwa ajili ya wokovu kwa kila anayeamini. Na kwa kuelezea  hili kwa moyo wa dhati ninawabariki na baraka ya kitume. Maria awalinde daima!

Mama Maria kimbilio la msaada alinde wafuasi wake

Mwisho Papa Francisko amewambea wote kwa maombezi ya Bikira Maria wa msaada kwa wafuasi wa Bwana na watu walio na mapenzi mema katika kipindi hiki kigumu kila upande wa dunia ambao wanafanya kazi kwa shauku kubwa na jihada za amani , kwa ajili ya mazungumzo kati ya mataifa, kwa ajili ya huduma kwa maskini, kwa ajili ya utunzaji wa kazi uumbaji, kwa ajili ya mazingira na kwa ajili ya ishindi wa binadamu dhidi ya magonjwa ya mwili na ya roho.

Siku ya Maombi ilitangazwa kwa ajili ya Kanisa la China ilitangazwa 2007

Siku ya maombi kwa ajili ya Kanisa la China iliyotangazwa kunako 2007 na Papa Mstaafu Benedikto XVI kwa “Barua ya wakatoliki wa China”. Siku hii inafanyika kila mwaka ifikapo tarehe 24 Mei. Ni tarehe ambayo Mama Kanisa anadhimisha  Siku kuu ya Bikira Maria Msaada wa Wakristo, kwa namna ya pekee anayeheshimiwa katika Madhabahu ya “Mama Yetu, Bikira Maria wa Sheshan, huko  Shanghai nchini China. Katika fursa hii ambayo sasa ni mwaka 13, Papa Benedikto XVI aliandika sala kwa Bikira Maria ambapo alikuwa akiomba awaongoze Watu wa Mungu “katika njia ya ukweli na ya upendo” ili kuwa kwa namna ya pekee wawe chachu ya Maelewano na kuishi kwa pamoja kati ya watu wote, kusaidia “ jitihada za wale wote ambao nchini China kila siku kwa ugumu wanaendelea kuamini, kutumaini na kupenda; na vile vile wasiogope kuzungumza juu ya Yesu na ulimwengu wa Yesu. Hatimaye katika sala hiyo alikuwa anamwomba Mama wa Mungu awasaidie wakatoliki wawe daima mashuhuda waaminifu wa pendo kwa kubaki kidete katika mwamba wa Petro mahali ambapo Kanisa limejengwa.

Umakini wa Kanisa la China umeendelezwa na Papa Francisko

Umakini wa Kanisa la China umeendelezwa pia na msimamo wa dhati wa Papa Francisko tangu aanze huduma yake kama kharifa wa Mtume Petro na  ambaye katika fursa ya Siku ya sala  hii, hakukosa kamwe kuonyesha ukaribu wake na upendo kwa wakatoliki wote wa China “ambao kila siku pamoja na ugumu na majaribu wanaendelea kuamini, kutumaini na kupenda. Papa amekuwa akiwashauri na kuwaweka chini ya Ulinzi wa Bikira Maria ili wabaki wameungana katika umoja wa Kanisa.

Ni muhimu kutembea kwa pamoja kwa ajili ya maelewani na jamii nzima

Hii inakumbusha pia Makubaliano ya muda ya kihistoria kati ya Vatican na Jamhuri ya Watu wa China yaliyotiwa sahini kunako tarehe 22 Septemba 2018  na ambapo kwa mujibu wa Kardinali Pietro Parolin, Katibu wa Vatican alisema kwamba “ni hatua ya kufika baada ya mchakato mrefu wa safari lakini pia ni hatua ya kuanzia kwa ajili ya mchakato wa hatua mpya inayohitaji ushirikiano mkubwa kwa ajili ya wema wa jumuiya nzima ya kikatoliki huko China na kwa ajili ya maelewano ya jamii nzima”. Tunatakiwa kutembea pamoja”, alisema Kardinali Parolin wakati wa mahojiano na 'The Global Times' (gazeti la kila siku nchini China la masuala ya kimataifa) ni kwa njia hiyo tu tunaweza kweli kuponyesha majeraha na masuala ya kizamani ya kutoelewana ili kuonesha ulimwengu hata kwa kuanzia na nafasi ya mbali ili kufikia matunda ya kweli mkataba”.

Wachungaji kwa mujibu wa huruma ya Mungu

Papa Francisko aliandika katika Ujumbe kwa Wakatoliki wa China na kwa Kanisa la Ulimwengu kunako tarehe 26 Septemba 2018 kuwa “Mkataba wa muda ni tunda la muda mrefu na mazungumzo makubwa ya Taasisi ya Vatican na Mamlaka tawala ya China, yaliyokuwa yameanzishwana Mtakatifu Yohane Paulo II na kuendeleza na Papa Mstaafu Benedikto XVI”.  “Hili siyo suala la kuteua maafisa kwa ajili ya usimamizi wa masuala ya kidini,bali ya kuwa na Wachungaji halisi kwa mujibu wa moyo wa Yesu, wanaojikita kufanya kazi kwa ukarimu katika huduma ya Watu wa Mungu”.

Uhusiano wa Vatican na  China kwa miaka ya hivi karibuni

Mambo mengi muhimu yaliyoanzishwa kwa miaka miwili ya mwisho yameweza kukuza uhusiano katika ya Vatican na China kwa mfano: Serikali ya Baijing kutoa ruhusa kwa maaskofu wawili, Giuseppe Guo Jincai na Giovanni Battista Yang Xiaoting, ili kushirikia Sinodi ya Maaskofu kuhusu vijana kunako mwaka 2018; hadi kufikia kuwekwa wakfu kwa Maaskofu akiwapo mwakilishi wa Kipapa kunako mwezi Agosti 2019 kwa maasko Antonio Yao Shun na Stefano Xu Hongwei, wote wawili maaskofu wa Jining/Wulanchabu, na huko  Mongolia ya ndani. kwa  askofu mwambata wa Hanzhong, Katika wilaya ya Kaskazini Magharibu mwa Shaanxi.

Ushirikiano katika masuala ya dharura ya janga la corona

Hivi karibuni, tangu kuanza kwa janga la virusi vya corona, kumekuwa na dhihirisho la ishara za kubadilishana za mshikamano kati ya Vatican na China na michango kwa pande zote mbili kuhusu zana na vifaa vya kinga za afya na vifaa vya usalama vinavyolenga kupambana na virusi. Waamini wengi wa China pia wameshiriki kupitia mitandao ya kijamii katika maadhimisho ya kila siku ya Misa ya Papa Francisko iliyokuwa ikiendeshwa katika Kanisa la Mtakatifu Marta saa 1 asubuhi majira ya Ulaya, wakati nchini China ilikuwa saa 7 mchana tangu mwezi Machi.

Maonyesho ya sanaa nchini China

Mazungumzo, maarifa na safari ya pamoja ili kujenga wakati endelevu wa pamoja wa maelewano ya hali ya juu, kama matashi mema ya Papa  yanaweza kupitia katika utamaduni na uzuri. “Uzuri unajumuisha sisi. Sanaa ya China kutoka Jumba la Makumbusho la Vaticani”, ndiyo ilikuwa mada iliyoongzwa katika maonyesho ya thamani kubwa na ya mfano, iliyoandaliwa huko Beijing na Jumba la Makumbusho la Vatican tangu tarehe  28 Mei hadi 14 Julai 2019 kwenye Jumba la Makumbusho la Jiji lililokatazwa.

24 May 2020, 14:10