Tafuta

Je wewe katika familia yako,unajua kuwasiliana au unafanana kama wale vijana wakiwa mezani wameshika kila mmoja simu za mkononi wanachat? Tupyaishe kuwasiliana ndani ya familia! Je wewe katika familia yako,unajua kuwasiliana au unafanana kama wale vijana wakiwa mezani wameshika kila mmoja simu za mkononi wanachat? Tupyaishe kuwasiliana ndani ya familia! 

Sikukuu ya Familia Takatifu:wazazi na watoto wasaidiane kufuata Injili!

Yesu,Maria na Yosefu wanaweza kuwa mfano wa utakatifu kwa ajili ya familia zetu.Ndiyo tafakari ya kabla ya sala ya Malaika wa Bwana ambapo Papa Francisko anaelekeza namna ya kuwajibika na kukubali Mapenzi ya Mungu kama njia ya kuelekea katika utakatifu hata leo hii kati ya wazazi na watoto.Anaweka wazi hayo katika siku ambayo Mama Kanisa anaadhimisha Sikukuu ya Familia Takatifu ya Yesu,Maria na Yosefu.

Na Sr. Angela Rwezaula – Vatican

Papa Francisko katika tafakari yake kabla ya Sala ya Malaika wa Bwana anajikita kuelekeza namna ya kuwajibika na kukubali Mapenzi wa Mungu kama njia ya kuelekea katika utakatifu hata leo hii kati ya wazazi na watoto. Amesema hayo kwa waamini na mahujaji wote waliofika katika kiwanja cha Mtakatifu Petro, Vatican Dominika tarehe 29 Desemba 2019 wakati Taifa la Mungu linaadhimisha Siku kuu ya Familia Takatifu ya Yesu Maria na Yosefu. Wazo kuu la Papa Francisko ni lile la kuhimiza kwa kina katika kupyaisha namna ya kuwasiliana ndani ya familia  na wakati wa kuhitimisha amewatakia matashi mema ya mwaka mpya wa amani na amani ndani ya moyo. Papa Francisko akianza tafakari yake amesema:Kwa kweli leo hii ni siku njema…Leo hii tunaadhimisha siku kuu ya Familia Takatifu ya Nazareth. Maana ya neno Takatifu linajikita ndani ya familia kwa mantiki ya kwamba, utakatifu ni zawadi ya Mungu, lakini wakati huo huo ni uhuru, uwajibikaji na mpango wake. Na ndivyo ulivyokuwa kwa familia ya Nazareth. Yeye mwenyewe aliwajibika kwa  dhati na kuitikia mapenzi ya Mungu.

Kushangazwa na mfano wa upole wa Maria

Ni kwa namna gani tusiweze tumeshangazwa  kwa mfano na upole wa Maria kutokana na  matendo ya Roho Mtakatifu ambaye anamwomba awe Mama wa Masiha?  Papa Francisko anauliza swali hili. Maria kama ilivyokuwa kwa kila kijana mwanamke wa wakati ule, alikuwa anataka kutimiza mpango wake wa maisha yaani kuolewa na Yosefu. Lakini alipotambua kuwa Mungu anamwita katika utume wa namna ya pekee hakusita kuitikia  kwamba: “ yeye ni mtumishi wake” ( Lk 1,28). Na kuwa na sifa zake kubwa, si  kwa sababu ya nafasi aliyonayo kama mama, bali ni kwa ajili ya utii kwa Mungu. “Heri wale wasikiao Neno la Mungu na kujikita katika matendo! ( Lk 11,28). Na alipokuwa aelewi vema matukio hayo yanayomsibu, Maria alikaa kwa ukimya na kutafakari, anatafakari na kuabudu mapenzi ya Mungu. Uwepo wake chini ya miguu ya msalaba ni tendo la wakfu kutokana na kukubali na utayari wake. Hata hiyo kwa upande wa Yosefu, Injili haioneshi hata neno moja. Kwa maana Yeye hazungumzi na badala yake anajikita katika matenda kwa kutii. Ni mwanaume wa ukimya; na ni mwanaume wa utii. Injili ya Siku (Mt 2,13-15.19-23), inatoa mwaliko kwa mara tatu kuhusu utii huo wa Yosefu mwenye haki, huku akioneshwa anavyo kimbilia Misri na kurudi katika nchi ya Israeli. Injili inaonesha akiwa chini ya ulinzi wa Mungu unaowakilishwa na Malaika, kwamba Yosefu alikimbia na familia yake dhidi ya hatari ya Erode!

Familia takatifu inatoa mshikamano na familia zote na zaidi wakimbizi

Papa Fracisko akiendelea na tafakari yake anafafanua amesema: " Familia takatifu inatoa mshikamano kwa familia zote duniani na ambazo zinalazimika kukimbia; inatoa mshikamano na wale wote ambao wanalazimishwa kuacha ardhi zao na nchi zao kutokana na kusongwa, vurugu na vita. Hatimaye nafasi ya tatu ya Familia Takatifu ni Yesu mwenyewe. Na kwake Yeye, Mtakatifu Paulo anasema hapakuwapo na majibu mawili ya ndiyo na hapana, bali jibu moja tu la ndiyo (2Kor 1,19). Na ndivyo ilivyoonesha katika vipindi vingi vya wakati wake. Kwa mfano katika matukio ya kipindi kile ambacho wazazi wake wakiwa na uchungu walikuwa wanamtafuta na yeye aliwajibu : “Hamjuhi kuwa napaswa kushughulika mambo ya Baba yangu? ( Lk 2,49); na katika mwendelezo huo anasema: “ Chakula changu ni kufanya mapenzi ya Yule aliyenituma” ( Yh 4,34); Sala yake katika bustani ya mizeituni anasema: “Baba yangu, ikiwa haiwezekani kikombe hiki kiniepuke nisipokunywa, basi mapenzi yako yatimizwe (Mt 26,42). Matukio yote hayo ni makamilifu katika maneno ya Kristo mwenyewe asemaye :” Wewe hukupenda sadaka wala zabihu (…) Na kwa maana hiyo ninasema: “Tazama nimekuja (…) ee Bwana kuyafanya Mapenzi yako (Eb 10,5-7; Zab 40,7-9).

Yesu, Maria na Yosefu ni familia takatifu inayowakilisha jibu la mapenzi ya Baba

Papa Francisko amesema kuwa Yesu Maria na Yosefu ni Familia takatifu inayowakilishwa na jibu la pamoja katika mapenzi ya Baba. Watu watatu wa familia hii wanasadiana kwa pamoja ili kugundua mpango wa Mungu. Hawa wanasali, wanafanyakazi na wanawasiliana. Lakini, “Mimi ninajiuliza: Je wewe katika familia yako, unajua kuwasiliana au unafanana kama wale vijana wakiwa mezani wameshika kila mmoja simu za mkononi wakichat? Katika meza hiyo utafikiri wako kimya kama vile katika misa… na kumbe hawasemezani. Kwa maana hiyo Papa Francisko anatoa mwito kuwa: "tunatakiwa kupyaisha kuwasiliana ndani ya familia.” Aidha anawashauri: “ Baba wote, wazazi wote na watoto, bibi  na babu ni  lazima kuwasiliana na ndugu kati yao…. Hiyo ndiyo kazi ya kufanya leo hii, katika siku kuu ya kweli ya Familia Takatifu”. Familia Takatifu inaweza kusaidia kuwa mfano wa familia zetu ili wazazi na watoto waweze kusaidiana pamoja katika kuifuata Injili ambayo ni msingi wa utakatifu wa Familia. Tumkabidhi Maria Malkia wa familia, familia zote ulimwenguni hasa zile ambazo zimejaribiwa na mateso na ugumu  na tusali kwa ajili ya ulinzi wake wa kimama.Papa Francisko amehitimisha.

29 December 2019, 13:36