Tafuta

Kardinali Pierbattista Pizzaballa,Patriaki wa Yerusalemu ya Kilatini amezungumza na  vyombo vya habari Vatican Kardinali Pierbattista Pizzaballa,Patriaki wa Yerusalemu ya Kilatini amezungumza na vyombo vya habari Vatican 

Kard.Pizzaballa:kuwaachilia mateka ni hatua ya kwanza kuelekea kumaliza mzozo

Patriaki wa Yerusalemu alitoa maoni yake kuhubu habari ya mazungumzo ambayo yalipelekea kuachiliwa kwa baadhi watekwa nyara na Hamas tangu tarehe 7 Oktoba 2023 na kuachiliwa kwa baadhi ya wafungwa wa Kipalestina.Tunahitaji"matarajio ya kisiasa kwa Gaza,tunahitaji kuondoa mizizi ya itikadi ya Hamas."

ANDREA TORNIELLI

Kuachiliwa kwa baadhi ya mateka, ni hatua ya kwanza kuelekea mwisho wa mzozo unaoendelea kati ya Israel na Hamas. Hayo yalisemwa na Patriaki wa Kilatini wa Yerusalemu, Kardinali Pierbattista Pizzaballa, aliyefikiwa kwa njia ya simu na vyombo vya habari vya Vatican.

Je, una maoni gani kuhusu habari za saa chache zilizopita?

"Ukweli kwamba makubaliano yamefikiwa juu ya kuachiliwa kwa angalau baadhi ya mateka ni chanya, kwa sababu hadi sasa njia pekee ya mawasiliano ilikuwa ya kijeshi. Kinyume chake, kwa njia hii inachukuliwa hatua ya kwanza kuelekea kupunguza mvutano wa ndani na kimataifa. Halafu pia ni njia ya kuanzisha masuluhisho mengine ambayo si ya kijeshi: namaanisha suluhisho za kumaliza mzozo."

Kulikuwa na hisia tofauti za habari ya kuachiliwa kwa mateka, hakika ya kuridhisha. Lakini pia kumekuwa na wachambuzi wengine wanaoamini kwamba, kiukweli, mazungumzo yenyewe kwa namna fulani yanawakilisha kushindwa ...

"Wale ambao - wacha tuwaite "mwewe"-wanataka kutambua amani na ushindi, labda wanaweza kufikiria hivi. Lakini amani, suluhisho la migogoro, haiwezi kuwa ushindi kamili. Haipo. Kwa hiyo ni wazi kuwa suluhisho haliwezi kuachiwa jeshi pekee. Ni wazi kuwa siasa lazima zichukue udhibiti wa hali hiyo, juu ya yote kutoa matarajio, kwa sababu wanajeshi hawana. Kwa hivyo ni wazi kwamba mazungumzo, kuachiliwa kwa mateka, ni hatua za kwanza za kuanza njia za matarajio ya kisiasa ya Gaza baada ya vita hivi. Ni lazima".

Tuna ripoti kwamba watu waliokimbia makazi yao kaskazini mwa Gaza wanajaribu kurejea katika kile ambacho mara nyingi ninachofikiria, ni nyumba zilizoharibiwa. Ina maana gani?

"Kwa kadiri ninavyoweza kuelewa bado hakuna uwezekano kama huo. Wengine wanataka kurejea kwa sababu hali, hata kusini mwa Gaza, ambako mamilioni haya ya watu wamesongamana, si rahisi. Kwa hivyo wanataka kutoka huko, ninaelewa vizuri sana. Hata Wakristo wetu waliofungiwa ndani ya kiwanja hicho kidogo cha Kanisa hawawezi kustahimili tena. Lakini kwakuwa hakuna mitazamo wazi ya kisiasa au uwazi juu ya awamu zinazofuata, hii bado haiwezekani na inaweza kuwa hatari."

Je, ugaidi unaweza kushindwa vipi? Je,itikadi kama hiyo ya Hamas inawezaje kushindwa?

"Siyo rahisi. Ni lazima tuuondoe, kidogo kidogo, kwa subira - inachukua muda mrefu - kila kitu kinachochochea itikadi hiyo. Kwa hivyo, lazima iondolewe mizizi. Haina maana kukata matawi, kwa sababu yanaweza kukua tena. Kwanza tunatakiwa kuwapa Wapalestina mtazamo fulani. Nilisema hili na najua kwamba wengi hawakulipenda: tunahitaji kutoa mtazamo wa kitaifa ambao bado hawana. Vita hivi ni ushuhuda wa wazi kabisa kwamba watu hawa wawili hawawezi kuishi pamoja, hata kama si kwa wakati huu. Watalazimika kuwa na mitazamo iliyo wazi, iliyofafanuliwa, sahihi, zaidi ya ambayo imefanywa hadi sasa. Kisha kuna kipengele kingine. Hamas pia ni itikadi ya kidini; kwa hivyo mazungumzo ya kidini ni muhimu sana, kama vile ilivyo muhimu sana kumwilisha na kukuza mazungumzo ya kidini ambayo hayana msingi wa chuki."

Tunaweza kufanya nini tukiwa Wakristo, lakini kwa ujumla kama watu ambao, ijapokuwa wanaishi mbali na maeneo hayo, wanajihisi kuwa karibu kwa sababu ni mahali pa kuishi, pa kuishi kwa Yesu duniani? Ni nini kinaweza pia kufanywa katika kiwango cha maoni ya umma?

“Kwanza kabisa kuna maombi kwa waamini ambayo ni jambo la kwanza la kufanya. Kisha kuna haja pia ya msaada wa kweli, ikiwa ni pamoja na msaada wa kibinadamu. Kipengele kingine muhimu: Nimeona kwamba migawanyiko yenye nguvu imeanzishwa ulimwenguni, moja dhidi ya mwingine. Inaonekana kama haiwezekani kuwapenda wote wawili. Ninaamini ni muhimu, kama Wakristo, pia kuwa wazi katika mazungumzo yetu, lakini si ya kipekee. Kuita vitu kwa majina yao, ukweli wao, na wakati huo huo kujaribu kuweka uhusiano wazi na kila mtu na kuwaambia kila mtu, wote wawili, kwamba tunawapenda."

25 November 2023, 12:30