Krakow:Askofu Henrik Stubkjær wa Denmark amechaguliwa kuwa rais wa LWF
Na Angella Rwezaula, - Vatican
Askofu Henrik Stubkjær wa Denmark amechaguliwa kuwa Rais mpya wa Shirikisho la Walutheri Dunini (LWF) ili kuongoza ushirika wa kimataifa wa makanisa ya kiluteri katika miaka ijayo. Mtaalimungu, ambaye anajulikana sana kwa kazi yake ya kidiakoni na kiekumeni, kwa sasa anahudumu kama mkuu wa Jimbo la Viborg katika Kanisa la Kiinjili la Kilutheri nchini Denmark. Alichaguliwa Jumamosi tarehe 16 Septemba 2023 na wajumbe kutoka ulimwenguni kote waliohudhuria Mkutano wa Kumi na Tatu huko Kraków, Poland ambao unaendelea hadi tarehe 19 Septemba 2023. Katika hotuba yake ya kwanza, Askofu Stubkjær alisema kuwa kazi ya LWF chini ya uongozi wake itaendelea kutegemea nguzo nne ambazo shirika hilo lilianzishwa, yaani, “kazi kwa ajili ya wahitaji na wanaokandamizwa, mipango ya pamoja katika utume, juhudi za pamoja katika taalimungu na jibu la pamoja kwa changamoto ya kiekumeni.” Rais mpya alithibitisha: kwamba Maono yake kwa LWF ni kwamba wanapata thamani zaidi kwa kufanya kazi pamoja kama ushirika wakijitahidi kuweka imani ya Kikristo katika matendo kupitia kazi ya kibinadamu na maendeleo, utetezi, ushuhuda wa pamoja na mazungumzo.
Kiongozi mpya huyo alibainisha kwamba kuwa Mlutheri ni kuwa na muktadha, kwani utofauti unaopatikana katika miktadha tofauti ni ishara ya jinsi ambavyo Mungu, kupitia Mwana wake Yesu Kristo, anavyolea wao kama makanisa wanachama [....] kuhubiri injili kwa njia inayofaa. Kwa hivyo, aliongeza, kwamba yeye anaona kama jukumu lake la kupata utofauti na kwamba sauti zote zitasikika. Wakati huo huo, alibainisha kuwa ulimwengu unazidi kuwa na ubaguzi na unabadilika haraka sana. Alinukuu maneno ya Papa Francisko wakati wa ziara ya mwisho ya LWF mjini Vatican kutia saini makubaliano ya kuongeza ushirikiano kati ya Huduma ya LWF na shirikisho la Caritas Internationalis la mashirika ya Kikatoliki ya kibinadamu. Akiondoka kwenye andiko lake rasmi, Papa aliuambia uongozi wa LWF: “Mnapaswa kujihadhari, kwamba ni nyakati za mabadiliko, Roho Mtakatifu ana nafasi kubwa zaidi ya kubadili mawazo yetu.” Katika maneno hayo, Askofu Stubkjær aliongeza, ni “ishara ya tumaini” kwamba makanisa ya Kikristo yanaitwa kuwa “katikati ya ulimwengu usio na tumaini mara nyingi.”
Kabla ya kuchaguliwa kwake kama Askofu mnamo 2014, Stubkjær alihudumu kwa karibu muongo mmoja kama katibu mkuu wa shirika la kibinadamu la Denmark DanChurchAid (DCA). Tangu Mkutano wa Kumi na Mbili wa Shirikisho la Kiluteri Ulimwenguni (LWF) nchini Namibia, amekuwa mjumbe wa Baraza la Uongozi la LWF, ambapo ameongoza kamati yake ya Huduma ya Ulimwenguni na mjumbe wa kamati yake ya utendaji. Askofu Stubkjær ameshikilia majukumu ya uongozi katika Muungano wa ACT. Yeye pia ni mwenyekiti wa shirika ambalo linasaidia wanaume wasio na makazi nchini Denmark ili kuwasaidia kuondokana na ulevi au utumiaji wa dawa za kulevya.
Kando na shauku yake ya kazi ya kishemasi na ya kibinadamu, Stubkjær anajulikana kwa ushiriki wake wa kiekumeni na kuzingatia elimu ya taaalimungu. Kuanzia 2016 hadi 2019 alihudumu kama mwenyekiti wa Baraza la Kitaifa la Makanisa nchini Denmark. Ndani ya Jimbo la Viborg, amehimiza ujenzi wa uhusiano na wahamiaji wa Kiorthodox kutoka Ulaya Mashariki, pamoja na wanaotafuta hifadhi na watu wa imani zingine. Kwa njia hiyo Askofu Stubkjær atasimikwa rasmi, pamoja na washiriki wa Baraza jipya, wakati wa ibada ya kufunga Mkutano huo mnamo Jumanne alasiri tarehe 19 Septemba 2023. Mkutano wa kwanza wa Baraza jipya chini ya uongozi wake utafanyika siku inayofuata, tarehe 20 Septemba 2023.