Tafuta

2023.02.10 Washiriki wa Mkutano wa kibara wa Australia na visiwa vyake kuanzia 5-10 Februari 2023, huko Suva, Fiji. 2023.02.10 Washiriki wa Mkutano wa kibara wa Australia na visiwa vyake kuanzia 5-10 Februari 2023, huko Suva, Fiji. 

Sinodi huko Suva-Fiji imehitimishwa na uhakika wa kusikilizwa kilio cha dunia

Mkutano wa Siku sita wa Sinodi ya Bara la Australia na visiwa vyake uliofanyika huko Suva,Fiji ulihitimishwa 10 Februari huku Maaskofu wakieleza furaha yao ya Juma zima la kusikiliza kilio cha masikini,dunia na bahari wakati wanasali na kutumia muda wao wakizingatia utume wao pamoja kama Wachungaji wa kanda yao.

Na Angella Rwezaula;- Vatican.

Ni kwa Juma zima walisindikizwa na tafakari ya maombi na utambuzi kuhusu mwitikio wao kama maaskofu wa Bara huku wakisaidiwa na Hati  kitendea Kazi ya Hatua ya Bara ya Sinodi. Ni kwa mujibu wa mwakilishi wetu wa Vatican News, Sr Bernadette M. Reis, fsp, aliyefuatilia Mkutano wa Kibara uliofunguliwa Dominika tarehe 5 Februari kwa washiriki ambao waliwalikisha Mabaraza ya Maaskofu wa Australia, New Zealand, Papua New Guinea na Visiwa vya Solomon pamoja na visiwa vya Pasifiki ambao umehitimishwa Ijumaa tarehe 10 Februari 2023 huko kisiwa cha Suva- Viji. Kwa mujibu wake alibanisha kwamba kwa hakika wazungumzaji mbalimbali na kundi la wataalimungu walitoa michango yao mikubwa kuhusu mada tatu zilizoainishwa kwa ajili ya kutafakari kwa kina ambazo zilikuwa ni: “sinodi, utunzaji wa bahari na malezi kwa ajili ya utume”.

Mkutano wa kibara wa Sinodi katika kisiwa cha Suva - Fiji kuanzia 5-10 Februari umehitimishwa
Mkutano wa kibara wa Sinodi katika kisiwa cha Suva - Fiji kuanzia 5-10 Februari umehitimishwa

Katika makabiliano hayo wajumbe  waliweza hata kuzunguka katika mazingira yao ya ndani na wakipitia liturujia mbili zilizojaa tamaduni na mila za Kifiji. Vile vile waliweza kufanya ziara kwenye mto wa ndani na njia ya bahari ambazo ziliruhusu wale walioshiriki kuona hata uharibifu uliofanywa dhidi ya asili, kupitia mazoezi ya uchimbaji na mabadiliko ya tabianchi kwa ujumla. Pamoja na hayo pia washiriki walifurahia onesho la moja kwa moja lililojumuisha muziki, dansi na historia zinazosimulia tabia ya nchi zote za Bara hilo la Visiwa ambamo waweza kusikia kweli vilio vya watu wa visiwa hivyo wanamoishi na bahari.

Umuhimu wa kujaza mapungufu katika suala la wanawake

Katika mahojiano ya mwisho, na Askofu Mkuu Peter Loy Chong Mkuu  Suva na Rais wa Baraza la Maaskofu wa Pasifiki (CEPAC) lililokuwa mwenyeji wa Mkutano wa kibara  alisema jinsi  alivyofurahishwa na kuridhishwa na matokeo ya Mkutano huo. Yeye aliweza kuhisi nguvu katika mkutano huo na  alitoa shukurani zake kwa Sekretarieti inayoundwa na walei wengi wao wakiwa ni wanawake ambao waliweza kuandaa na kufanikisha Mkutano huo. Akizungumzia kuhusu jibu la Hati ya Kitendea Kazi kwa Hatua ya Bara, Askofu Mkuu alibainisha kwamba maaskofu wa visiwa hivyo walitoa mchango wao na kujaza kile walichofikiri ni mapungufu. Pengo moja alilobainisha lilikuwa ni kuhusu wanawake na suala la jeuri za nyumbani, ambalo  alithibitisha kuwa ni tatizo kubwa kwa visiwa vya Fiji na Papua New Guinea, lakini hata Australia.”

Sr. Nathalie:Roho Mtakatifu amevuma katika watu waliokusanyika Suva

Kwa upande wa Sr. Nathalie Becquart, Katibu Mkuu Msaidizi wa Sekretarieti ya Sinodi, alielezea Mkutano huo kama tukio zuri na la kina. Kwa upande wake alielezea  alivyoguswa moyo aliposhuhudia Maaskofu wakitoa “sauti” kwa Kanisa katika sehemu hiyo ya dunia na roho yao ya umisionari. Kwa hiyo ,Sr Nathalie alisema  kwamba hata hivyo  Sinodi tayari imepachikwa kwa njia nyingi na  alihisi Kanisa la visiwa hivyo kupitia uzoefu wake hapo na kwamba  limesikiliza kwa kina sauti ya maskini, kilio cha dunia, kilio cha bahari na kilio cha watu wakati huo  linajaribu kujibu wito huo wa Mungu kwa kuendelea kuwa Kanisa lililo karibu na watu katika muktadha huo, ili kusisitizia malezi kwa ajili ya utume na kuwa zaidi na zaidi Kanisa la Sinodi. Kiukweli alisema, inawezekana kutafakari kazi ya Roho kwamba inavuma juu ya bahari na kupitia mioyo ya watu waliokusanyika huko  Suva.

Sr. Nathalie Katibu Mkuu msaidizi wa Sekretarieti ya Sinodi ya Maaskofu

Katika taarifa yao iliyotolewa Ijumaa tarehe 10 Februari 2023,  wakati wa kuhitimisha Mkutano huo, Shirikisho la Mabaraza ya Maaskofu Katoliki wa Visiwa vya Australia walibainisha kuwa: “imekuwa ni furaha kubwa kwa Maaskofu wa  wa Bara hili kukusanyika Fiji kwa  Juma hili kwa ajili ya kusali na kuzingatia utume wetu wa pamoja, kama wachungaji Wakuu wa Kanda yetu. Kama tulivyowaombea watu wetu, tumekuwa tukifahamu maombi ambayo wamekuwa wakitoa kwa ajili ya kusanyiko letu na huduma yetu. Kusanyiko letu limetoa fursa kwetu kusali pamoja, kujenga uhusiano wa kidugu, kujifunza kutoka kwa mtu mwingine na kuzingatia changamoto za kawaida za kichungaji.”

Kisiwa cha Sufa-Fiji na madhari yake kilikuwa mwenyeji wa Mkutano wa kibara 5-10 Februari 2023
Kisiwa cha Sufa-Fiji na madhari yake kilikuwa mwenyeji wa Mkutano wa kibara 5-10 Februari 2023

Katika Mkutano huo wa Sinodi wa Juma moja ambao ulihitimishwa tarehe 10 Februari 2023 kwa kuadhimisha Misa Takatifu,  wachungaji hao wa ndani hatimaye wametumwa kwa upya kwa ajili ya utume wa kimisionari katika maeneo yao yote ya visiwa vyao. Kutokana na hili ni matazamio yao ya kuwepo katika  maadhimisho ya kikao cha kwanza cha Sinodi  kitakachofanyika mwezi Oktoba 2023 mjini Vatican huku wakitambua kuwa sauti zao zimesikika!

Matoleo ya Sadaka wakati wa misa ya kuhitimisha Mkutano wa kibara wa Sinodi huko  Suva-Fiji
Matoleo ya Sadaka wakati wa misa ya kuhitimisha Mkutano wa kibara wa Sinodi huko Suva-Fiji
11 February 2023, 10:51