Tafuta

Chuo cha Ufundi Mgongo ni Chuo ni cha Wamisionari wa Consolata na kiko Jimbo Katoliki la Iringa, Tanzania. Chuo cha Ufundi Mgongo ni Chuo ni cha Wamisionari wa Consolata na kiko Jimbo Katoliki la Iringa, Tanzania.  (ANSA)

Chuo Cha Ufundi Mgongo, Jimbo Katoliki la Iringa: Ufundi, Elimu, Ujuzi, Maadili na Utu Wema!

Chuo cha Ufundi Mgongo ni Chuo kinachoendeshwa na kusimamiwa na Wamisionari wa Consolata na kiko Jimbo Katoliki la Iringa, Tanzania. Chuo kinapokea vijana walio maliza kidato cha nne wenye moyo wa kujifunza na kujiandaa kwa ajili ya maisha. Kauli mbiu: Elimu ni dira na ufundi ni uhai. Chuo kinakazia nidhamu, utu na maadili; Utunzaji bora wa mazingira kwa mafao ya wengi.

Na Padre Danstan Mushobolozi, Balayangaki, IMC, - Iringa, Tanzania.

Mkataba wa Mfumo Mpya wa Elimu Kimataifa “Global Compact on Education” ulitiwa mkwaju hapo tarehe 15 Oktoba 2020. Baba Mtakatifu Francisko anakazia kuhusu: Janga la elimu duniani, maana ya elimu, umuhimu wa kupyaisha mfumo wa elimu na hatimaye, mambo msingi yanayopaswa kuzingatiwa katika maboresho ya Mfumo wa Elimu Kimataifa. Hii ni pamoja na kuragibisha utunzaji bora wa mazingira nyumba ya wote; haki na amani; mafao ya wengi, ukarimu kwa wageni, wakimbizi na wahamiaji pamoja na ujenzi wa udugu wa kibinadamu. Hii ni changamoto ambayo imeanza kuvaliwa njuga na viongozi wa kidini, shule, taasisi za elimu ya juu pamoja na vyuo vikuu. Baba Mtakatifu anakaza kusema, amani ya kweli inafumbatwa katika utunzaji bora wa mazingira nyumba ya wote na kwamba, amani inapaswa kulindwa na kudumishwa na wote daima. Baba Mtakatifu Francisko katika Waraka wake wa Kitume “Misericordia et misera” yaani “Huruma na amani” anasema, huruma ni kielelezo makini cha upendo wa Mungu unaosamehe, unaoongoa, unaopyaisha na kubadili mwelekeo wa maisha. Ni kielelezo cha ufunuo wa Fumbo la Mungu ambalo ni huruma ya milele, inayowakumbatia na kuwaambata wote pasi na ubaguzi, kiasi cha kuwakirimia maisha mapya, chemchemi ya furaha na matumaini mapya, yanayovunjilia mbali ubaguzi, ubinafsi na uchoyo ili kutenda wema, kufikiri vyema na kuondoa huzuni moyoni.

Serikali ya Tanzania inathamini sana elimu ya ufundi miongoni mwa vijana
Serikali ya Tanzania inathamini sana elimu ya ufundi miongoni mwa vijana

Vijana wana thamani kubwa katika maisha na utume wa Kanisa na Kristo Yesu anawapenda upeo. Vijana watambue kwamba, wao ni matumaini ya Kanisa na Jamii katika ujumla wake. Wanandoa na Makleri, wanahamasishwa kuwa ni wanyoofu, watulivu na mashuhuda wa upendo na huduma kwa Kristo Yesu na Kanisa lake hususan miongoni mwa vijana wa kizazi kipya. Baba Mtakatifu Francisko anasema, Maandiko Matakatifu yanaonesha upendeleo wa pekee ambao Kristo Yesu aliwaonesha vijana waliotamani kumfuasa katika maisha na utume wake kama inavyojionesha kwa yule kijana tajiri, ambaye Kristo Yesu, alimwona, akampenda na hatimaye, akamwita kumfuasa, lakini kwa bahati mbaya, yule kijana alizongwa mno na malimwengu kiasi cha kukataa kutikia wito wa Kristo Yesu. Rej Mk 10:21. Tangu mwanzo wa maisha na utume wake, Kristo Yesu alipenda kuandamana na vijana, kwa kujenga urafiki, matumaini na kuonesha ule umuhimu wa kutembea pamoja katika kutangaza na kushuhudia Ufalme wa Mungu kati ya watu wa Mataifa. Vijana ni chanzo na chemchemi ya matumaini ya maisha na utume wa Kanisa.

Chuo kinazingatia: elimu, ujuzi, maarifa, maadili na utu wema.
Chuo kinazingatia: elimu, ujuzi, maarifa, maadili na utu wema.

Kwa kutambua na kuthamini elimu ya ufundi, Serikali inayo azma ya kujenga Chuo cha Ufundi Stadi katika kila Mkoa na Wilaya nchini Tanzania. Katika mwaka huu wa fedha 2022/2023, Serikali imetenga kiasi cha Shilingi Bilioni Mia moja (100 Bil). Kiasi hicho cha fedha ni kwa ajili ya kuanza ujenzi wa Vyuo vya Ufundi Stadi katika Wilaya 62 kwa Wilaya ambazo zilikuwa hazijajengewa Vyuo vya Ufundi Stadi. Aidha, Wilaya ya Manyoni ni miongoni mwa Wilaya hizo 62 ambazo zipo kwenye mpango wa kujengewa Vyuo vya Ufundi Stadi kwa mwaka huu wa fedha. Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia Mhe Prof Adolf Mkenda amesema hayo hivi karibuni Bungeni Jijini Dodoma wakati akijibu swali la Mhe Dkt. Pius Stephen Chaya, Mbunge wa Jimbo Manyoni Mashariki aliyetaka kufahamu serikali ina Mpango gani wa kujenga Chuo cha VETA Wilayani Manyoni. Waziri Mkenda amesema kuwa katika mwaka huu wa fedha 2022/23, Serikali imetenga kiasi hicho cha fedha kwa ajili ya kuanza ujenzi wa Vyuo vya Ufundi Stadi katika Wilaya 62 kwa Wilaya ambazo zilikuwa hazijajengewa Vyuo vya Ufundi Stadi.

Vijana wanapohitimu masomo yao, tayari wanaweza kujiajiri na kuajiriwa
Vijana wanapohitimu masomo yao, tayari wanaweza kujiajiri na kuajiriwa

Chuo cha Ufundi Mgongo ni Chuo kinachoendeshwa na kusimamiwa na Wamisionari wa Consolata na kiko Jimbo Katoliki la Iringa, Tanzania. Chuo kinapokea vijana walio maliza kidato cha nne wenye moyo wa kujifunza na kujiandaa kwa ajili ya maisha. Chuo hiki kinaandaa vijana kwenye ujuzi wa nyanja mbali mbali yakiwemo maadaili na kujitegemea. Chuo kinachukua vijana wa jinsia zote kike na kiume, dini zote na kabila zote. Lengo letu ni malezi kwa vijana na kuwaandaa kuambata maisha yajayo wanajifunza komputa, Kiingereza, ujasili maji na Stadi za maisha (life skills) na maadili na dini. Chuo kimesajiliwa na VETA REG. NO: VET/IRA/FR/2020/B/116 ni Chuo cha kundi B. Kauli mbiu ya Chuo hetu ni Elimu ni Dira, Ufundi ni Uhai. HISTORIA YA CHUO: Chuo kilianzishwa mwaka 1997 sasa kina miaka 25, ikiwa na nia ya kuendeleza vijana ambao wamisionari wetu waliwapokea kama watoto yatima waliokuwa nyumba yetu ya watoto yatima ya Faraja House. Mwaka 2012 wazo likawa pengine si watoto yatima tu wanataka faraja ya maisha bali ni vijana wote ambao tukijifunza na kufanya kazi nao watakuza ubunifu na sanaa ya ufundi. Basi wazo hilo limekuwa na kuzaa matunda.

Nidhamu, maadili na utume wema ni muhimu sana kwa malezi ya wanafunzi
Nidhamu, maadili na utume wema ni muhimu sana kwa malezi ya wanafunzi

MAFANIKIO YA CHUO: Tunao vijana wanaweza kujifunza fani mbali mbali zikiwemo: Ushonaji Miaka 2: Uunganishaji wa vyuma miaka 2: Umeme majumbani miaka 2: Ufundi magari miaka 2: Ufugaji bora miaka 3. Mpaka sasa vijana wanaotoka chuoni kwetu wamepata nafasi za kazi nzuri na wengine tumewaajiri sisi wenyewe kwenye jumuiya na taasisi zetu. Wengine wamejiajiri wenyewe na kufungua vituo vyao vya kazi. Wao ni waajiri wa wao wenyewe mfano wameanzisha, maduka ya vifaa vya umeme na kusaidia kufunga umeme, kuanza ufugaji na kusaidia watu wa mazingira yao kufuga kitaalam, utengenezaji wa majiko sanifu kwa wanao chomelea ambayo upunguza utumiaji mwingi wa nishati ya kuni na hivyo kulinda mazingira. CHANGAMOTO: Kama mkurugenzi naona changamoto zipo nyingi tukianza na mwamko wa kuitikia huduma hii ya malezi ya vijana. Tunao vijana wachache, sababu wengi uwaza kuwa ufundi ni elimu ya kiwango cha chini. Changamoto ya pili ni umaskini siyo kila mtu anaweza kulipia jampo malipo yetu ni nafuu, ni Laki tano kwa mtu wa kutwa na milioni moja kwa mtu wa Bweni, bado ugumu wa maisha wa watu unafanya waengine washindwe kulipia.

Changamoto ya umaskini ivaliwe njuga ili vijana wapate elimu ya ufundi
Changamoto ya umaskini ivaliwe njuga ili vijana wapate elimu ya ufundi

USHAURI KWA VIJANA NA SERIKALI: Ufundi ni sanaa kwa hiyo mtu akiwa na ujuzi ni tajiri wa kutosha, vijana mjitokeze kwa wingi kujifunza kuwa na taaluma mkononi. Kwa Serikali yangu pendwa ya Tanzania na nchi zote zinazo enedelea ufundi ndo mkombozi wetu. Tuwahimize vijana wasome ufundi. Wakimaliza tayari wana ajira mkononi ili tutengeneze wataalam wa kati. Kwa vile changamoto ni umaskini wengine wanashindwa kulipa ada serikali iongee ruzuku, ili kuwawezesha vijana wengi kupata fursa ya mafunzo na hatimaye, kupungumza mzigo kwa jamii. Watu binafsi na wenye shule binafsi na mashirika mbalimbali na wananchi wote kwa ujumla waje wapate ujuzi huku ili kupata ujuzi, maarifa na stadi za kazi. Ni rahisi sana kumwandaa mtu amalize na ajira kuliko kumaliza masomo ya shahada akatembea na bahasha ya kaki kutafuta fursa ya ajira.

Chuo cha Ufundi Mgongo
27 December 2022, 15:33