Tafuta

Shirikisho la Mashirika ya Watawa wa Kike Afrika Mashariki na Kati, ACWECA limekuwa mstari wa mbele katika kuchangia mchakato wa uinjilishaji mpya Afrika Mashariki na Kati Shirikisho la Mashirika ya Watawa wa Kike Afrika Mashariki na Kati, ACWECA limekuwa mstari wa mbele katika kuchangia mchakato wa uinjilishaji mpya Afrika Mashariki na Kati 

Mkutano Mkuu wa 20 wa AMECEA: Mchango wa Watawa wa Kike ACWECA Katika Uinjilishaji

Shirikisho la Mashirika ya Watawa Kike Afrika Mashariki na Kati, ACWECA pamoja na mambo mengine, linapania: Kukuza na kuendeleza majiundo makini ya watawa; kuwajengea uwezo watawa ili waweze kushiriki kikamilifu katika mchakato wa kujenga na kudumisha misingi ya haki, amani, upatanisho pamoja na kujitegemea. Wadau muhimu sana katika mchakato wa uinjilishaji mpya.

Na Padre Richard A. Mjigwa, C.PP.S. – Vatican.

Shirikisho la Mabaraza ya Watawa wa Kike Afrika Mashariki, ACWECA. “The Regional Association of Consecrated Women in Eastern and Central Africa) lilianzishwa kunako mwaka 1974 na kwa sasa linawajumuisha Watawa wa kike wapatao 30, 000 kutoka katika Nchi za Afrika Mashariki na Kati. Kwa hakika, hawa ni Watawa wa Shirikisho la Mabaraza ya Maaskofu Katoliki Afrika Mashariki na Kati, AMECEA. ACWECA pamoja na mambo mengine, linapania: Kukuza na kuendeleza majiundo makini ya watawa; kuwajengea uwezo watawa ili waweze kushiriki kikamilifu katika mchakato wa kujenga na kudumisha misingi ya haki, amani, upatanisho pamoja na kujitegemea. Ni Shirikisho linalotoa msaada wa kiufundi kwa Mashirika ya kitawa, ili kweli watawa waweze kuwa ni mashuhuda wa Kristo Yesu kati ya watu wanaowahudumia katika sekta mbalimbali za maisha, kama sehemu ya uinjilishaji wa kina. Wanaunga mkono jitihada za Baba Mtakatifu Francisko katika utunzaji bora wa mazingira nyumba ya wote kama anavyobainisha katika Waraka wake wa Kitume “Laudato si” yaani “Sifa iwe kwako” juu ya utunzaji wa nyumba ya wote.

ACWECA liko mstari wa mbele katika malezi na ulinzi wa watoto wadogo
ACWECA liko mstari wa mbele katika malezi na ulinzi wa watoto wadogo

Shirikisho linajielekeza zaidi katika nyanja kuu nne yaani: Malezi na utume, Familia na Utume wa Vijana, Haki, Amani na Uumbaji fungamani sanjari na ustawi, maendeleo na mafao ya Mashirika ya Kitawa. Watawa wanashiriki kikamilifu katika mkutano wa AMECEA kama sehemu ya ujenzi wa Kanisa la Kisinodi linalopania kukuza umoja, ushiriki na utume, kwa kujikita katika majadiliano ya kina yanayofumbatwa katika dhana ya kusikilizana. AMECEA na ACWECA ni Mashirikisho mawili yanayotegemeana na kukamilishana katika uinjilishaji, katekesi na huduma za kijamii bila kusahau utunzaji bora wa mazingira nyumba ya wote. Ulinzi wa watoto dhidi ya nyanyaso za kijinsia “SCORE na ECD” ni utume unaopewa kipaumbele cha pekee katika maisha na utume wa ACWECA sanjari na ujenzi wa Jumuiya Ndogondogo za Kikristo. Hayo yamebainishwa na Sr. Rosalia Sakayombo, Rais wa ACWECA, tarehe 13 Julai 2022 katika hotuba yake kwenye maadhimisho ya Mkutano wa wa 20 wa AMECEA, unanogeshwa na kauli mbiu: “Utunzaji wa Mazingira kwa Ajili ya Maendeleo Endelevu ya Binadamu.” Hii ni kauli mbiu inayochota maudhui na utajiri wake kutoka katika Waraka wa Kitume wa Baba Mtakatifu Francisko, “Laudato si” yaani “Sifa iwe kwako” juu ya utunzaji wa nyumba ya wote.” Shirikisho la Mabaraza ya Watawa wa Kike Afrika Mashariki, ACWECA. “The Regional Association of Consecrated Women in Eastern and Central Africa) lilianzishwa kunako mwaka 1974 kwa sasa linajiandaa kuadhimisha Jubilei ya miaka 50 tangu kuanzishwa kwake, hapo mwaka 2024.

ACWECA 2022
13 July 2022, 17:54