Vietnam:Makuhani waitwa kuwa wamisionari na huruma
Na Sr. Angella Rwezaula – Vatican.
Kueneza Neno la Bwana na kupeleka thamani za kikatoliki kwa watu mahalia, ndiyo utume wa mapadre 15 wapya waliopata daraja la ukuhani mnamo tarehe 3 Desemba 2021 katika Siku Kuu ya Mtakatifu Francis wa Xaveri kwa kuwekwa mikono na Askofu Mkuu Joseph Vu Van Thien wa Jimbo Kuu Katoliki la Hanoi, katika Kanisa la Hoang Nguyen, mji mkuu huko Vietnam. Na wakati huo huo na Mapadre 9 walipewa daraja la upadre tarehe hiyo hiyo na Askofu Joseph Chau Ngoc Tri wa jimbo la Lang Son Cao Bang, katika Kanisa Kuu la Cua Nam huko Lang Son.
Askofu Mkuu Van Thien, hata hivyo baada ya kutamka kuwa mwaka 2022 katika Kanisa lao mahalia utakuwa mwaka wa Uinjilishaji, kama ilivyokuwa miaka mngine iliyopita ambayo waliadhimisha mwaka wa Umoja na Utakatifu, aliwashauri makuhani wapya kufuata mfano wa Mtakatifu Francis Xaveri aliyeinjilisha India yote na anayefikiriwa kuwa kama mmisionari mkubwa wa enzi mpya na mfano wa wainjilishaji wote wa leo hii. Askofu Mkuu alisema, makuhani wapya wanaweza kuwa kweli na uwezo kuwa wavunaji, wenye shauku ya kutoka nje katika kambi na kupeleka roho za watu kwa Mungu.
Askofu Mkuu Van Thien pia alikumbusha juu ya tabia za huduma ya kuhani na umisionari kwamba makuhani wanaitwa kuwa wamisionari wa kweli na kutumwa katika maisha ya sasa kwa ajili ya kueneza Neno la Mungu, kushuhudia Yesu Kristo katika maisha na kuwakusanya kondoo waliopotea. Ushauri kwa vijana hao wapya mapadre kutoka kwa Askofu Mkuu pia ni kufanya kazi na walei ili shughuli za kichungaji ziweze kuleta matunda. Huo ndiyo uzuri wa kimisionari katika maisha ya makuhani, alsisitiza na kuomba kusali kwa pamoja ili makuhani wao wageuke kuwa wachungaji wema ambao wanaponesha majeraha ya kiroho na kimwili ya waamini. Jimbo la Hanoi kwa sasa lina makuhani 203 ambao wanahudumua Parokia 171 na jumla ya wakatoliki 320,000.
Askofu Joseph Chau Ngoc: Upendo mkuu kwa ajili ya utume wa uinjilishaji
Askofu Joseph Chau Ngoc Tri wa Jimbo katoliki la Lang Son Cao Bang kwa upande wake wakati wa mahubiri alikumbusha makuhani hao kwamba ili kuweza kuwa padre na mmisionari kama Mtakaifu Francis Xaveri, inahitaji kuwa na moyo unaowaka mapendo makuu kwa ajili ya utume wa uinjilishaji. Makandidati hao walisikiliza wito wa Mungu kwenda katika eneo hilo la mbali kwenye mlima na mbali na marafiki na wazazi ili kuhudumia watu hao wa Mungu. Hapo alielezea kuhusu eneo hilo maskini sana ambalo sehemu kubwa ni makundi ya makabila yanayozungumza lugha tofauti kwa kufuata ibada zao za kimila au kidini. Pamoja na matatizo hayo,alisema makuhani wapya kwa kuiga mfano wa umisionari kama Mtakatifu Francis Xaveri, walikwenda huko kupanda mbegu ya imani bila woga wala kukata tamaa.
Kutokana na maelezo hayo Askofu aliwashauru makuhani wapya kuwatunza kwa moyo wa kibaba watoto na vijana walioko katika maeneo hayo na kuwafuatilia katika maeneo yao ya mbali ya jimbo la Mlimani, makuhani wazee, kwa kuwapa umakini na kujenga uhusiano kidugu na ndugu wote mahalia, vile vile na watawa wengine pamoja na waseminari. Pamoja na matatizo mengi yaliyomo katika nchi hiyo na hasa kwa usambaaji wa virusi vya UVIKO-19 mwaka huu, majimbo 10 ya kaskazini watakuwa na makuhani 137 wapya na mashemasi 43 wa mpito.