Kitabu kipya:Kwa ajili ya demokrasia baada ya ubaguzi wa rangi
Na Sr. Angela Rwezaula – Vatican.
Katika duka la vitabu, la Mtakatifu Paulo kinapatikana kwa sasa kitabu kipya cha watunzi wake Filomeno Lopes na Roberto Mancini chenye kichwa: “Kwa ajili ya demokrasia baada ya ubaguzi wa rangi”. Ni barua iliyo wazi kwa Maaskofu wa Italia na Afrika juu ya mgogoro wa uhamiaji. Utangulizi wa kitabu hicho umeandikwa na Bwana Andrea Riccardi Mwanzilishi wa Jumuiya ya Mtakatifu Egidio na maelezo ya baadaye yameandikwa na Askofu Carlos Alberto Moreira Azevedo wa Ureno, ambaye tangu tarehe 11 Novemba 2011 ni mwakilishi wa Baraza la Kipapa la Utamaduni. "Leo hii kwa sababu ya utandawazi, ulioboreshwa na itikadi mamboleo na kufuatia kwa janga la Covid-19, tunashuhudia kuzidisha kwa kujenga kuta za kutengenisha, kuenea kwa serikali za utaifa, mlipuko wa ubaguzi wa rangi kama mantiki “ya kawaida”, ya dharura na kutengwa kwa wengine". Hizo ni ndondoo za kitabu hicho chenye kurasa 256.
Mbele ya kukabiliwa na mwenendo huu, jibu letu ni nini, kama Wakristo na Wakatoliki ambao wanaishi Italia na Magharibi mbele ya misalaba mipya ya historia inayobisha hodi katika milango ya nchi zetu, kwa njia inayoonekana kuwa isiyo ya kawaida? Je! Ni changamoto zipi zinazosababisha matukio kwa ukatoliki wetu katika mtazamo wetu wa maoni ya kidini, kiroho, kimaadili na kisiasa? Je! Tunaweza kushinda saratani hii ya ubaguzi wa rangi na ukabila pamoja kuunda demokrasia ya baada ya ubaguzi wa rangi na ukabila?
Maswali yote haya yanahitaji kujibiwa katika kitabu hicho yaliyotungwa kama barua wazi kwa Maaskofu wa Italia na Afrika. Wito wa nguvu unaotolewa katika kitabu hicho kwa ajili ya kujenga jamii ya pamoja, ya kidemokrasia, ya kaka na dada, ambayo inahitaji Wakatoliki kuchangia kuunda nafasi za kukutana ili kuanzisha hatua mpya ya kisiasa ambayo inahamasisha kurudi tena kwa ubinadamu, hadhi, haki na amani.
Kuhusiana na watunzi hawa wa kitabu, Filomeno Lopes ni mwandishi wa vitabu na mwandishi wa habari wa Radio ya Vatican, asili yake ni kutoka Guinea-Bissau ambaye anazungumza kiitaliano kwa ufasaha. Mnamo mwaka wa 2015 alichapisha kwenye Matoleo ya SUI kitabu kitwacho “Kutoka upendeleo hadi ubora”. Ni tafakari za kifalsafa za wahamiaji wa Kiafrika. Mnamo 2020, na mchapishaji wa Castelvecchi, kitabu kingine kiitwacho “sipendi wabaguzi wa rangi” kikiwa na Dibaji ya Enrico Letta, mwanasiasa wa Italia aliyekuwa Waziri Mkuu wa Italia tangu Aprili 2013 hadi Februari 2014.
Wakati huo huo Roberto Mancini ni profesa wa kawaida wa Falsafa ya Kinadharia katika Chuo Kikuu cha Macerata. Yeye ni mkurugenzi wa Shule ya Uchumi wa Mabadiliko katika Chuo Kikuu cha Amani cha Marche. Mnamo 2009 alipokea Tuzo ya Zamenhof ya ‘Sauti za Amani’. Miongoni mwa machapisho yake ya hivi karibuni tunakumbuka: ‘Chaguo la kukaribisha’, toleo la Qiqajon, Magnano (BI) 2016, na ‘Falsafa ya wokovu’. Njia za ukombozi kutoka katika mfumo wa kujiangamiza, Matoleo ya Chuo Kikuu cha Macerata, 2019.
Kitabu hicho cha watunzi Filomeno Lopes, Roberto Mancini, “Kwa ajili ya demokrasia baada ya ubaguzi wa rangi". Barua ya wazi kwa Maaskofu wa Italia na Afrika juu ya shida ya uhamiaji, kwa sasa kinapatikana katika toleo la Mtakatifu Paulo 2021, chenye kurasa 256 na kinauzwa Euro 20.00.