Congo DRC,Kard.Ambongo Besungu:Pasaka ni mwaliko wa kuongoka&jitihada ya wema kwa Taifa
Na Sr. Angela Rwezaula – Vatican.
Katika ujumbe wa Kardinali Fridolin Ambongo Besungu, Askofu Mkuu wa Kinshasa, Congo DRC, katika fursa ya kutoa ujumbe wake kwa waamini wa Pasaka 2021, ameandika kuwa: “Bwana anatupenda na kututunza, na wakati huo huo anatuhitaji ili jamii ibadilike na kwa njia hiyo ni lazima sana uongofu wetu”. Katika ujumbe huo Kardinali anatoa ushauri kwa wakongo wote kuwa na dhamiri ya kwamba kila mtu ni mwenye thamani mbele ya Mungu. Yeye yuko karibu nao na kuwaokoa dhidi ya kudhalalishwa, chuki, njaa ,magonjwa, hasa la janga la Covid-19 na kifo
Ili kuweza kuchangia mpango wa wokovu wa Mungu,Kardinali Ambongo Besungu anaongeza kuandika kuwa inahitaji kukemea ukosefu wa haki na kuheshimu hadhi ya binadamu na kwa maana ya uwajibikaji na jitihada ili kila mmoja aweze kuwa na maisha yenye hadhi. Kardinali akiwalekeza waamini wote amesema “ Msiogope, Kristo amefufuka. Yu mzima. Yuko karibu nasi karibu na anapambana nasi ili kushinda kifo”.
Hatimaye katika ujumbe wake Askofu Mkuu wa Kinshasa, anawashauri watu wote kwa namna ya pekee wale wanahusika na uwajibikaji kimamlaka waaondokane na mioyo ya mawe, ya ubinafsi, ya kutojali, ya uchu wa mali, ya ugumu na choyo ili kuweza kuwa na moyo mzuri, wenye huruma kama wa Mungu. Kwa kufanya hivyo, anaongeza kusema kuwa Nchi yao itabadilika. Kardinali anasema Kristo Mfufuka aweze kuwapa nguvu ya kufanya kazi pamoja katika kuboresha hali ya maisha na kufanya kazi na wakongo wote kike na kiume.