Siku ya Kimataifa ya Udugu wa Kibinadamu:dini zina nafasi ya kuchangia amani na haki
Na Sr. Angela Rwezaula – Vatican.
Dini zina jukumu la kuchangia amani na haki. Ni uthibitisho wa Baraza la Maaskofu Ujerumani (Dbk), katika barua iliyotiwa saini na Askofu Bertram Meier, Makamu rais wa Tume ya Mazungumzo ya kidini. Tafakari ya wakuu wa kanisa imekuja katika fursa ya Siku ya kwanza ya Kimataifa ya Udugu wa Binadamu, iliyotangazwa na Umoja wa Mataifa kwamba kila tarehe 4 Februari ni kukumbuka siku hii. Maadhimisho hayo ni siku ya kumbukumbu ya “Hati juu ya udugu wa kibinadamu kwa ajili ya amani ya ulimwengu na kuishi pamoja”, iliyosainiwa huko Abu Dhabi, katika Falme za Kiarabu, mnamo tarehe 4 Februari 2019 na Papa Francis na Imam Mkuu wa Al-Azhar, Ahmad Al- Tayyib ambapo leo mchana, Papa mwenyewe atajiunga na mipango iliyopangwa kufanyika katika fursa hiyo.
Kila mmoja anaitwa kufanya kazi ya utamaduni wa amani na uvumilivu
“Kila mmoja wetu ameitwa kufanya kazi kwa ajili ya utamaduni wa amani na uvumilivu, kutetea haki za binadamu na kushinda kile kinachotugawanya. Papa na Imam Mkuu wanajua juu ya chuki na ushabiki ambao umetolewa kwa jina la dini. Na ni kwa sababu hii ndiyo wanatukumbusha sana kwamba sisi sote ni watoto wa Mungu, sawa katika haki na utu, tumeitwa kuishi pamoja kama dada na kaka ”ameandika Askofu Meier
Covid-19 ulimwenguni inaonesha wazi kuwa sisi ni sehemu moja ya wanadamu
“Siku hii anarudisha katika ishara wazi kwamba dini zina nafasi, lakini pia ni jukumu, kuchangia amani na haki duniani, nyumba yetu ya pamoja. Haijalishi ni vizuizi vipi vya kushinda kwenye njia ya amani ya ulimwengu, tunatembea ndani mwake tukimtumaini Mungu wetu ambaye anaunganisha mioyo iliyogawanyika na kuinua roho ya mwanadamu ”,amesisitiza kiongozi huyo wa Kanisa nchini Ujerumani. Kwa njia hiyo ameongeza tunaangalia muktadha mgumu wa ulimwengu unaosababishwa na janga la Covid-19 na ambao unamfanya kila mtu “kufahamu zaidi ukweli kwamba sisi sote ni sehemu ya familia moja ya wanadamu”.
Kuhamasishwa na roho ya udugu na kuungana na Wakristo
Hata hivyo Askofu Meier ametoa onyo juu ya jaribu linalozidi kuongezeka la ubinafsi na anawasihi Wakristo kuwa “watafsiri utume wa upendo kwa vitendo halisi”, kwa sababu “upendo wa Kikristo sio jambo la kibinafsi tu, lakini daima ina mwelekeo mkuu wa kijamii”. Kutokana na hilo ndipo anatoa mwaliko katika kuhitimisha kwa “kuhamasishwa na roho ya udugu na kuungana na Wakristo ulimwenguni kote ili kusali na kuomba Muumba” sala iliyotungwa na Baba Mtakatifu Francisko mwishoni mwa Waraka wake wa “Fratelli tutti” yaani Wote ni ndugu juu ya undugu na urafiki kijamii”.
Katika sala hiyo inasema: “Njoo Roho Mtakatifu! Tuonyeshe uzuri wako. Uonekane kwa watu wote wa dunia, ili kugundua kuwa kila mtu ni muhimu, na kwamba wote ni muhimu, kwamba ni wenye nyuso tofauti za ubinadamu ule ule uliopendwa na Mungu”. Amina