Italia:Maji ni Baraka ya Nchi kwa binadamu wote!
Na Sr. Angela Rwezaula- Vatican
Maji ni maisha. Mifano mingi ya Maandiko Matakatifu inamwongelea mtu na uumbaji ambao wanapata neema ya kuishi kwa kutumia maji. Mahali palipo na maji kuna uhai na ni chanzo cha uoto wa asili. Ni katika Ujumbe wa Baraza la Maaskofu la Italia (CEI) kwa fursa ya siku ya kushukuru itakayoadhimishwa tarehe 8 Novemba 2020 huku ikibeba kauli mbiu 'Maji ni baraka ya nchi' kwa kuwaalika kuwekeza katika mikakati ya muda mfupi na mrefu ili kupambana na uchafuzi wa maji duniani.
Utafiti wa Maaskofu unaonesha kuwa, “leo kuna hitaji kubwa la kuwa na miongozo katika utumiaji wa rasilimali huku watu wakiwekeza zaidi katika miundo mbinu ya utumiaji wa maji. Kwani maji ni hitaji la msingi la mwanadamu lisiloepukika katika kuishi na katika kutegemeana. Uwiano unaotegemeana na kukamilisha kati ya maumbile na miundo mbinu ya kimaendeleo ni wa muhimu sana kama alivyosema Baba Mtakatifu Francisko katika wosia wake wa Laudato si’. Kwa njia hii kunaweza kuimarishwa katika ya shughuli za kilimo zinazotumia maji na kwa akina mama wakitimiza wajibu wa wito wao wa kuandaa chakula kwa ajili ya maisha yao.
Papa Francisko katika ujumbe wake alioutoa baada ya sinodi ya Amazonia aliandika akitumia lugha ya picha ya ndoto ya maji inayodai tafakari ya kina juu ya uhalisia katika kumtegemeza mwanadamu. Pindi, rasilimali maji itakapokosekana maisha yote yakageuka kuwa mateso. Wakulima wanalitambua hilo lakini jamii nyingine bado inapuuzia na kutotilia maanani juu ya mabadiliko ya nchi ambayo yanayageuza maeneo mengi duniani kuwa jangwa. Kwa sasa suala la utunzaji wa maji ni la lazima na kuweka mipango mkakati wa kulinda vyanzo vya maji si jambo mbadala kwa mafao ya watu.
Hii ni kutokana na kushuhudia uchafuzi wa mazingira na utupaji wa takataka kutoka viwandani kuishia kwenye mito na katika maziwa na baharini hali inayohatarisha afya kwa ujumla. Upingaji wa matendo hayo, utambuzi na utumiaji w abusara ni silaha malidadi znazoweza kupunguza madhara ya uchafuzi wa mazingira. Kufanya hivi ni kutii amri ya Mwenyezi Mungu ya kuilima na kuitunza nchi (Mwa 2:15) wamesema Maaskofu wa Italia na pia kutunza maji ni wema kwa wote. Kutoka na hilo hakuna sababu za kibiashara ambazo zinaweza kujiridhisha kwa namna yeyote ile ili ziendelee kuharibu mazingira mahalia.
Kuadimika kwa rasilimali ya maji siyo changamoto pekee inayosababishwa na viwanda vya kilimo bali pia viwanda vimeweza kutengeneza tatizo la kiulimwengu lililopelekea kuwepo kwa janga la COVID -19 ambalo limeleta madhara makubwa kwa watu. Hata hivyo bado kuna hitaji la kuvikuza viwanda vya kilimo ili viweze kusaidia katika ukuaji wa uchumi wa nchi huku tahadhari zote za utunzaji wa mazingira zikichukuliwa.