2021.05.13 Wakimbizi wa ndani wa Palma wakiwa  Pemba nchini Msumbiji. 2021.05.13 Wakimbizi wa ndani wa Palma wakiwa Pemba nchini Msumbiji. 

Msumbiji:Waliohamishwa Palma wanahitaji msaada wa kila kitu

Kulingana na shirika kimataifa la kibinadamu (IOM),karibu watu 900,000 watakabiliwa na shida kubwa ya chakula kati ya Cabo Delgado,Niassa na Nampula,kabla ya mavuno Aprili – Septemba mwaka huu hivyo kuna uhitaji wa msaada kwa yote.Jimbo kuu la Nampula wameanza kujenga nyumba 200.

Na Sr. Angela Rwezaula – Vatican.

Katika mashambulizi ya tarehe 24 Machi katika jiji la Palma nchini Msumbiji, limeongeza kuwa na hali halisi ngumu ambayo tayari ilikuwapo ya kibinadamu katika Wilaya ya Cabo Delgado, Kaskazini mwa Msumbiji. Kabla ya mashambulizi huko Palma zaidi ya watu 696.200 walikuwa tayari wamehamishwa ndani, Kaskazini mwa Nchi. Hii inawakilisha ongezeko la karibia la watu 28,000 tangu mwishoni mwa 2020 kwa mujibu wa Shirika la Kimataifa la uhamiaji (IOM). Kulingana na shirika hilo la kibinadamu, karibu watu 900,000 wanatarajiwa kukabiliwa na shida kubwa ya ukosefu chakula katika maeneo ya Cabo Delgado, Niassa na Nampula, kabla ya mavuno ya tangu Aprili hadi Septemba.

Mzozo, ambao unasababisha kuacha makazi na watu  kuendelea kukimbia , umesitisha shughuli za kilimo na masoko yaliyopooza na shughuli za uvuvi, kwa sababu jamii za wavuvi zimelazimika kukimbilia mbali na pwani, hasa katika wilaya za kaskazini za jimbo hilo. Kwa kuongezea, mavuno katika maeneo ya pwani na kati ya majimbo ya Cabo Delgado na Nampula yanatarajiwa kuwa chini ya wastani, kwa sababu ya mvua isiyo ya kawaida, joto kali lisilo la  kawaida na uharibifu unaosababishwa na wadudu kama ‘Spodoptera frugiperda’.

Ili kuwapokea wakimbizi wa ndani, serikali imeanzisha kituo cha usafirishaji kwenda katika Kituo cha Michezo cha Pemba, chenye uwezo wa kuchukua watu karibu 400. Pamoja na kuwasili kwa boti kadhaa za wakimbizi hivi karibuni idadi ya watu wanaoishi katika kituo hicho imeongezeka hadi 213, wakiwemo wazee, watu wenye ulemavu na wanawake wajawazito.

Mbali na mashirika ya kimataifa na asasi za kiraia, Kanisa Katoliki pia linajitoa kutoa msaada kwa waliokimbia makazi yao. Jimbo kuu la Nampula limeanzisha mradi wa kujenga nyumba 200 ili kuchukua maelfu ya watu waliohamishwa ambao kwa sasa wanakaribishwa na Jimbo kuu katika mahema. Ni  Familia 200 zenye jumla ya watu 3,170 wengi wao walitoroka shambulio mnamo 24 Machi huko Palma. Jiji lilichukuliwa rasmi na vikosi vya serikali kutoka mikononi mwa kundi la wanajihadi ambao walijitangaza kuwa wafuasi wa Dola la Kiislamu. Lakini vyanzo vya ndani vinaripoti mashambulio  yapo kuzunguka jiji na kuna hofu hata kwamba lengo linalofuata la wanajihadi linaweza kuwa jiji la Pemba, kiti cha jina moja, ambalo wamo katika wilaya ya Palma. Hata hivyo ikumbukwe kwamba wanajihadi wamedhibiti mji wa bandari wa Mocímboa da Praia tangu Agosti iliyopita.

13 May 2021, 18:21