Serikali ya Tanzania, Jumapili tarehe 5 Julai 2020 imezindua Banadari ya Kabwe, iliyoko mkoani Rukwa kwa gharama ya shilingi bilioni saba. Serikali ya Tanzania, Jumapili tarehe 5 Julai 2020 imezindua Banadari ya Kabwe, iliyoko mkoani Rukwa kwa gharama ya shilingi bilioni saba. 

Tanzania Yazindua Bandari ya Kabwe iliyoko Mkoani Rukwa!

Serikali ya Awamu ya Tano itaendelea kudhibiti matumizi ya fedha za umma ili iweze kuendelea na ujenzi wa miradi ya kimkakati zikiwemo bandari kwa lengo la kuboresha maendeleo ya wananchi wake. Changamoto ya usafirishaji wa mizigo na abiria kati ya Tanzania na DRC itakuwa historia baada ya: upanuzi, kuboreshwa na kujengwa kwa miundombinu ya bandari katika wa Ziwa Tanganyika.

Na Ofisi ya Waziri Mkuu, -Rukwa.

Waziri Mkuu wa Tanzania Kassim Majaliwa amesema Serikali ya Awamu ya Tano inayoongozwa na Rais Dkt. John Pombe Magufuli itaendelea kudhibiti matumizi ya fedha za umma ili iweze kuendelea na ujenzi wa miradi ya kimkakati zikiwemo bandari kwa lengo la kuboresha maendeleo ya wananchi wake. Pia, Waziri Mkuu amesema changamoto ya usafirishaji wa mizigo na abiria kati ya Tanzania na Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo (DRC) itakuwa historia baada ya kuboreshwa na kujengwa kwa miundombinu ya bandari katika wa Ziwa Tanganyika ukiwemo upanuzi wa bandari ya Kasanga. Waziri Mkuu aliyasema hayo Jumapili jioni Julai 05, 2020, alipozungumza na wananchi baada ya kuweka jiwe la msingi katika mradi wa upanuzi wa Bandari ya Kasanga iliyoko wilaya ya Kalambo akiwa katika ziara ya kikazi mkoani Rukwa. Mradi huo unagharimu zaidi ya sh. bilioni 4.7. Alisema upanuzi wa bandari hiyo utawezesha mizigo inayotoka nchini Tanzania kwenda DRC kufika kwa wakati kwa sababu itasafirishwa moja kwa moja bila kupitia katika nchi nyingine kama ilivyo sasa, ambapo madereva wanalazimika kupita kwenye Mataifa mengine na kutumia muda mrefu.

“Mradi huu ukikamilika utaongeza pato la mwananchi mmoja mmoja pamoja na Taifa kwa ujumla. Rais Dkt. Magufuli amedhamiria kuboresha maendeleo ya wananchi nchi nzima ikiwemo na wilaya hii ya Kalambo. Ujenzi wa miradi hii unatoa fursa za ajira kwa wananchi, hivyo zichangamkieni.” Vilevile, Waziri Mkuu alisema mapambano dhidi ya vitendo vya rushwa bado yanaendelea nchini, hivyo mtu yeyote atakayebainika anajihusisha na masuala hayo atafutwe popote alipo akamatwe na achukuliwe hatua za kisheria kwa sababu rushwa ni adui wa haki. Pia, Waziri Mkuu aliendelea kuwakumbusha watendaji ndani ya Serikali wahakikishe wananchi wanapofika katika maeneo yao ya kazi wawapokee, wawasikilize na kuwahudumia bila ya ubaguzi. “Hatuangalii sura wala kabila yeyote atakayekanyaga kwenye maeneo yenu ahudumiwe ipasavyo.” Kwa upande wake, Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano, Mhandisi Isack Kamwelwe alisema Tanzania na Congo zimeungana kwa Ziwa Tanganyika, usafiri wa barabara uliokuwa unatumika awali uliyalazimu maroli ya mizigo kupitia nchini nyingine na kuchelewa kufika. Alisema kukamilika kwa upanuzi wa bandari hiyo pamoja na ujenzi wa barabara kwa kiwago cha lami kutoka Sumbawanga hadi Kasanga kutarahisisha usafirishaji wa abiria na mizigo kwa kutumia bandari hiyo kuingia nchini Congo moja kwa moja bila kupita kwenye nchi jirani.

Waziri Kamwelwe alisema kuwa awali kulikuwa na changamoto ya barabara hali iliyosababisha meli kufika kwenye Bandari ya Kasanga na kulazimika kusibiri mizigo ambayo ilikuwa ikichelewa kufika kutokana na ubovu wa barabara na sasa tayari Serikali imeitatua kwa kuijenga kwa kiwango cha lami. Awali, akitoa taarifa ya maendeleo ya mradi huo, Kaimu Katibu Mkuu wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano anayeshughulikia Uchukuzi, Mhandisi Thomas Ngulima alisema mradi huo umeanzishwa ili kuongeza ushindani na tija katika shughuli za kibandari kusini mwa Ziwa Tanganyika. Alisema mradi huo unahusisha upanuzi mkubwa wa gati ilililopo sasa lenye urefu wa mita 20 lifikie mita 120, ambazo zitawezesha kuhudumia  meli mbili hadi sita kwa wakati. Kazi nyingine ni ujenzi wa miundombinu ya bandari ikiwemo jengo la kupumzikia abiria, mgahawa na nyumba za watumishi. Mhandisi Ngulima alisema mradi huo unaojengwa na kampuni ya Inter-Consult Limited umefikia asilimia 70 na unatarajiwa kukamilika mwishoni mwa mwezi Septemba, 2020 na kwamba utafungua na kuboresha njia ya biashara ya mazao ya chakula katika nchi za DRC, Burudi na Zambia.Aliongeza kuwa, ujenzi wa barabara ya kimkakati inayoanzia Manispaa ya Sumbawanga hadi Kasanga (km 107), pamoja na upanuzi wa bandari unaoendelea, utawezesha mtiririko wa shehena za saruji, makaa ya mawe, chokaa na sabuni kuongezeka hivyo kukuza uchumi wa wananchi na Taifa.

Wakati huo huo, Waziri Mkuu Kassim Majaliwa amezindua Bandari ya Kabwe uliyojengwa na kampuni ya Kitanzania ya Sumry’s Enterprises kwa thamani ya sh. bilioni saba. Ujenzi huo wa Bandari ya Kabwe yenye eneo la ukubwa wa mita za mraba 10,864 unalenga kuongeza tija katika shughuli za bandari kwenye mwambao wa Ziwa Tanganyika na kupanua fursa za kibiashara. Waziri Mkuu amezindua bandari hiyo Jumapili, Julai 05, 2020 wakati akiwa katika ziara ya kikazi mkoani Rukwa. Bandari hiyo imenjengwa Kata ya Kabwe, wilayani Nkasi, mkoani Rukwa. Waziri Mkuu ameipongeza kampuni ya Sumry’s Enterprises kwa kujenga vizuri mradi huo. “Rais wetu Dkt. Magufuli amesema Watanzania tunaweza na huyo mkandarasi amedhihirisha hilo.” “Hizi ni jitihada zinazofanywa na Serikali ya Awamu ya Tano inayoongozwa na Rais Dkt. John Pombe Magufuli za kuhakikisha maendeleleo yanawafikia wananchi wote bila ya ubaguzi.” Waziri Mkuu ametumia fursa hiyo kuwasisitiza wananchi washirikiane na Serikali katika kulinda miundombinu ya mradi huo ili iweze kudumu. “Hatuna historia mbaya hapa, endeleeni kudumisha uaminifu na uadilifu ili bandari hii iwe ni mahali salama kwa abiria na mizigo. Bandari hii itaongeza fursa za kibiashara kati yetu na nchi jirani.”

Kwa upande wake, Mwakilishi wa Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Bandari Tanzania (TPA) Dkt. Baraka Mdima amesema mradi huo utakuwa chachu ya kukuza uchumi na kuboresha usafiri. “Mradi huu wa bandari utaboresha usafiri wa majini kwa wananchi waishio kandokando ya Ziwa Tanganyika hususani wilaya ya Nkasi na katika kata ya Kabwe na vijiji vinavyoizunguka.” Amesema mradi umehusisha ujenzi wa gati la kupaki meli lenye uwezo wa kuhudumia meli kubwa za kubeba abiria na mizigo zenye urefu hadi mita 75 na miundombinu mingine ya bandari kama jengo la kupumzikia abiria, majengo ya ofisi, nyumba za kuishi watumishi na eneo la mgahawa.

06 July 2020, 09:10