Ni wazee wanaokuza utamaduni wa matumaini na kuhakikisha uhai wa nchi,uzalendo na Kanisa, kwa mujibu wa  maelezo kutoka kwa Papa Francisko Ni wazee wanaokuza utamaduni wa matumaini na kuhakikisha uhai wa nchi,uzalendo na Kanisa, kwa mujibu wa maelezo kutoka kwa Papa Francisko 

Baba Mtakatifu Francisko:uzee ni tunu zenye kuzaa matunda!

Katika siku ya kimataifa ya wazee,kwa mara nyingine tena umesikika wito wa Baba Mtakatifu Francisko akiwataka watu wenye mapenzi mema kuwasaidia wazee ikiwa pamoja na vijana,hiyo ni kwa sababu wazee ndiyo wanaokuza utamaduni wa matumaini na kuhakikisha uhai wa nchi,uzalendo na Kanisa.

Na Padre Angelo Shikombe, - Vatican

Baba Mtakatifu Francisko katika kuadhimisha siku ya wazee duniani tarehe Mosi oktoba 2019, ametoa mwaliko wa kuwathamini na kuwasaidia wazee kwa maana wazee ni kama mmea wenye kuzaa matunda. Baba Mtakatifu ameyasema hayo katika mkutano wa kimataifa ulioandaliwa na Jumuiya ya Mtakatifu Egidio huko Firenze Italia. Ameutaka Umoja wa Mataifa kuwapa kipaumbele wazee wanaohitaji msaada katika jamii. Kauli mbiu ya mwaka huu katika kuadhimisha siku ya wazee duniani ni kuwaenzi watetezi wazee wa haki za binaadamu, kwa kuimarisha haki zao, kuzidisha utambuzi wao katika jamii na kutatua changamoto wanazopitia.

Siku ya wazee duniani inafanyika kila tarehe Mosi Oktoba ambapo wazee kutoka kila kabila na Taifa wanaalikwa kufurahia maisha yao wakimshukuru Mungu kwa zawadi ya uhai na nguvu alizowajalia hadi kufikia uzee. Naye Mtaalam huru wa Umoja wa Mataifa Rosa Kornfeld mnamo tarehe 30 Septemba 2019 ametoa mwaliko wa kushirikiana na wazee na kuwasaidia katika mahitaji yao. Kutokana na taarifa zilizotolewa na umoja wa Mataifa zinasema, takriban watu milioni 700 kwa sasa wana umri wa miaka 60, na ifikapo mwaka 2050 watu bilioni 2 ambayo ni zaidi ya asilimia 20 ya idadi jumla ya watu duniani watafikisha umri wa miaka 60 au zaidi.

Kuongezeka kwa idadi ya wazee duniani litakuwa jambo kubwa na litakalokwenda haraka zaidi katika dunia ya sasa inayoendelea huku bara Asia likiwa na idadi kubwa ya wazee na Afrika nayo ikifuata kuwa na idadi hiyo kubwa ya wazee. Katika kupambana na changamoto zinazowakabili wazee duniani, Baraza la Umoja wa Mataifa tangu mwaka 1991 liliweka sheria kuhusu haki za wazee kwa kuzingatia kuwa wazee wana mahitaji makubwa na kuzeeka au kuwa mkongwe hakuondowi utu na haki za msingi za mwanadamu.  Umoja huo ulianzisha siku hii ya kuwaadhimisha wazee, kwa lengo la kutoa ulinzi kwenye masuala ya uhuru, ushiriki, huduma, heshima na utu wao. Umoja wa Mataifa unasema ni jukumu la vizazi vyote kulinda haki ya jamii inayozeeka.

Na huko nchini Tanzania, Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa amepokea maandamano ya wazee katika fursa ya Maadhimisho ya siku ya Wazee duniani yaliyofanyika Kitaifa kwenye uwanja wa Nangwanda Sijaona, mjini Mtwara. Waziri mkuu Kassim Majaliwa wakati wa hotuba yake ameelezea jinsi Serikali inavyotekeleza majukumu yake ya kuwalinda na wazee. Pamoja na kuweka mikakati ya uhakika katika ulinzi wa maisha ya wazee ameliomba Baraza la Umoja wa Mataifa kutumia rasilimali zilizopo kwa ajili ya kuwasaidia wazee!

01 October 2019, 14:29