Ziara ya Parolin nchini Kameruni ni ishara ya umakini wa Papa kwa bara la Afrika
Na Sr. Anagela Rwezaula – Vatican
Kardinali Pietro Parolin, Katibu wa Vatican kuanzia Alhamisi tarehe 28 Januari hadi tarehe 3 Februari atakuwa nchini Kameruni akisindikizana na Monsinyo Ivan Santus, Afisa wa Kitengo cha Uhusiano na Mataifa cha Katibu wa Serikali.
Ziara hiyo ina lengo la kuonesha kwa mara nyingine tena katika muktadha wa sasa wa dharura ya kibinadamu, ya virusi vya corona, umakini wa Kanisa na wa Baba Mtakatifu kwa ajili ya bara la Afrika, ardhi yenye utajiri wa kibinadamu lakini iliyo na mateso makubwa. Na zaidi, anataka kuwa ishara ya kweli ya jitihada za pamoja, mshikamano na ushiriki katika kulinda na kuhamasiaha hadhi na wema wa wote, kwa ajili ya kujihusisha zaidi kwa huruma, mapatano, uponywaji , heshima na ukarimu, mambo ambayo yameeelezwa katika Ujumbe wa 54 wa Siku ya Amani duniani, mnamo tarehe Mosi Januari 2021 kwa kuongozwa na kauli mbiu “ “Utamaduni wa Utunzaji kama Njia ya Amani”.
Katika ziara hiyo inaonesha ratiba ya mikutano na viongozi wakuu wa nchi. Aidha mikutano ya kidini ambapo , Kardinali Parolin ataadhimisha Misa Takatifu katika Kanisa Kuu la Bamenda na kumvisha Palio Askofu Mkuu wa Jimbo hilo Andrew Nkea Fuanya. Atatembelea “Foyer de l'Esperance”, Yaani Foyer ya Matumaini huko Yaoundé, kituo kilichoanzishwa miaka 40 iliyopita na Padre mjesuit Yves Lescanne kwa ajili ya vijana wa barabarani na vijana waliofungwa.