Rais Kersti Kaljulaid akutana na kuzungumza na Papa Francisko mjini Vatican, Alhamisi tarehe 28 Novemba 2019. Rais Kersti Kaljulaid akutana na kuzungumza na Papa Francisko mjini Vatican, Alhamisi tarehe 28 Novemba 2019. 

Rais Kersti Kaljulaid wa Estonia akutana na Papa Francisko!

Baba Mtakatifu na Rais wa Estonia wameridhishwa na uhusiano mwema uliopo kati ya nchi hizi mbili pamoja na kukumbukia hija ya kitume ya Baba Mtakatifu Francisko nchini Estonia kunako mwaka 2018, kama sehemu ya maadhimisho ya Jubilei ya Miaka 100 ya Uhuru wa Estonia. Wamejadili pia umuhimu wa elimu, haki jamii pamoja na utunzaji bora wa mazingira nyumba ya wote.

Na Padre Richard A. Mjigwa, C.PP.S. – Vatican.

Baba Mtakatifu Francisko, Alhamisi, tarehe  28 Novemba 2019 amekutana na kuzungumza na Mama Kersti Kaljulaid, Rais wa Jamhuri ya Watu wa Estonia, ambaye baadaye amekutana pia na kuzungumza na Kardinali Pietro Parolin, Katibu mkuu wa Vatican aliyekuwa ameambatana na Askofu mkuu Paul Richard Gallagher, Katibu mkuu wa mambo nchi za nje na ushirikiano wa kimataifa mjini Vatican. Katika mazungumzo kati ya Baba Mtakatifu na mgeni wake, wameridhishwa na uhusiano mwema uliopo kati ya nchi hizi mbili pamoja na kukumbukia hija ya kitume ya Baba Mtakatifu Francisko nchini Estonia kunako mwaka 2018, kama sehemu ya maadhimisho ya Jubilei ya Miaka 100 ya Uhuru wa Estonia.

Baadaye, Baba Mtakatifu pamoja na Rais Kaljulaid wamegusia kuhusu umuhimu wa elimu, haki jamii pamoja na utunzaji bora wa mazingira nyumba ya wote. Mwishoni, Baba Mtakatifu pamoja na mgeni wake, wamejielekeza zaidi kwenye masuala ya kikanda na kimataifa lakini kwa namna ya pekee kabisa masuala ya amani na usalama; umuhimu wa Jumuiya ya Kimataifa kushirikiana ili kuzuia na kutafuta suluhu ya migogoro mbali mbali kwa njia ya amani. Baba Mtakatifu amefanya rejea kwenye mgogoro wa kivita nchini Ukraine pamoja na changamoto inayoendelea kulikabilia Bara la Ulaya kwa siku za mbeleni!

Papa: Estonia
28 November 2019, 17:12