Askofu Paul Olawoore ateuliwa kuwa Askofu mpya Jimbo la Ilorin!
Na Padre Richard A. Mjigwa, C.PP.S. – Vatican.
Baba Mtakatifu Francisko ameridhia ombi la kung’atuka kutoka madarakani lililowasilishwa kwake na Askofu Ayo-Maria Atoyebi, O.P. wa Jimbo Katoliki Ilorin, lililoko nchini Nigeria. Wakati huo huo, Baba Mtakatifu amemteuwa Askofu Paul Adegboyega Olawoore kuwa Askofu mpya wa Jimbo Katoliki la Ilorin. Kabla ya uteuzi huu Askofu Paul Adegboyega Olawoore alikuwa Askofu mwandamizi mwenye haki ya kurithi Jimbo Katoliki la Ilorin.
Itakumbukwa kwamba, Askofu Paul Adegboyega Olawoore alizaliwa tarehe 30 Novemba 1961. Baada ya masomo na majiundo yake ya Kikasisi, akapewa Daraja takatifu ya Upadre tarehe 3 Oktoba 1992, kama Padre wa Jimbo Katoliki la Oyo, nchini Nigeria. Tarehe 4 Aprili 2018, akateuliwa na Baba Mtakatifu Francisko kuwa Askofu mwandamizi mwenye haki ya kurithi Jimbo Katoliki la Ilorin, Nigeria na hatimaye, kuwekwa wakfu tarehe 13 Julai 2018.