Papa:Uponeshwaji wa moyo unaanzia na usikivu!

Papa katika tafakari yake kabla ya sala ya Malaika wa Bwana amefafanua jinsi ambavyo waamini wanakosa muda wa kusimama na kusikiliza aliye karibu kwa maana hiyo hata Neno la Mungu.Yesu anaponesha kiziwi na sisi sote tuna masikio,lakini mara nyingi hatusikilizi walio karibu.Papa ameelezea pia hija ya Budapest na Slovakia.

Na Sr. Angela Rwezaula – Vatican.

Dominika tarehe 5 Septemba 2021, Papa Francisko ameongoza sala ya Malaika wa Bwana katika uwanja wa Mtakatifu Petro jijini Vatican. Kabla ya sala hiyo ameanza na tafakari yake na kwa kuongozwa na masomo ya siku kuwa: "Injili katika liturujia ya leo inawakilisha Yesu ambaye anatenda miujiza ya uponeshwaji wa kiziwi. Katika simulizi inashangaza namna ambayo Bwana anatenda ishara hiyo ya miujiza. Na anafanya hivi: “Akamtenga na mkutano faraghani, akatia vidole vyake masikioni mwake, akatema mate, akamgusa ulimi, akatazama juu mbinguni, akaugua, akamwambia, Efatha, maana yake, Funguka (Rej. Mk 7,33-34). Katika uponeshaji mwingine wa magonjwa kama hayo makubwa, kama vile kupooza au ukoma, Yesu hafanyi ishala nyingi. Lakini ni kwani sasa anafanya hivyo licha ya kuwa walimsihi kumwekea mgonjwa mikono tu? Kwa nini ishara hizi?"

Papa Francisko akiendelea kufafanua amesema kwamba labda ni kwakuwa hali ya mtu huyo ilikuwa na hali fulani kwa namna ya kialama. Kuwa kiziwi ni ugonjwa, lakini pia ni alama. Na alama hii na kuwa na  jambo fulani la kutuambia sisi sote. Je ni kitu gani? Ni jambo la kiziwi. Mtu huyo hakuweza kuzungumza kwa sababu halikuwa hawezi kusikia. Yeye kiukweli ili aweze kutakaswa sababu ya ugonjwa huo alitia vidole vyake masikioni mwake, baadaye midomoni. Lakini kwanza ni katika masikio. Papa Francisko amesema kuwa “sisi sote tuna masikio, lakini mara nyingi hatuwezi kusikia. Kwanini Kaka na dada? Kwa hakika kuna uziwi wa undani na ambao leo hii tunaweza kumwomba Yesu auguse na kutakasa. Na uziwi huo wa ndani ni mbaya zaidi kuliko wa kimwili, kwa sababu ni uziwi wa moyo. Kutokana na haraka, mambo mengi ya kusema na kufanya, hatuna muda wa kusimama na kusikiliza anayezungumza. Tuna hatari ya kugeuka mpira usiopenyeza kwa kila kitu na bila kutoa nafasi kwa yule mwenye kuhitaji kusikilizwa, kwa mfano, Papa amekumbuka watoto, vijana, wazee na wenye shida ambao hawahitaji sana maneno na mahubiri bali kusikilizwa.

Papa ameongeza: “tujiuliza je usikivu wangu ukoje. Ninaacha niguswe na maisha ya watu, ninajua kujitoa muda wangu kwa kwa ajili ya yule aliye karibu nami ili kumsikiliza?  Hii ni kwa ajili yetu wote, lakini kwa namna ya pekee kwa mapadre. Kuhani anapaswa asikilize watu na sio kwenda kwa haraka. Kusikiliza na kutafuta namna ya kusaidia, lakini ni baada ya kusikiliza. Na sisi sote awali ya yote tusikilize kwanza  na baadaye kujibu. Tufikirie maisha katika familia: ni mara ngapi wanazungumza bila kusikiliza kwanza, badala yake ni kurudia rudia maneno yale yale! hatuwachi mwingine amalize kuzungumza na kujieleza …  sisi tunamkatisha ; yaani ni watu wasio na uwezo wa kusikiliza. Kuzaliwa kwa upya mazungumzo mara nyingi yanapitia si katika maneno, lakini kwa ukimya, na si mkazo bali ni kuanza tena kwa uvumilia ili kusikiliza mwingine, kusikiliza ugumu wake anaoubeba ndani mwake. Uponeshwaji wa moyo unaanza kwa kusikilizwa. Kusikiliza ndiyo kunatakasa moyo. Papa akitoa mfano amesema “wengine wanaweza kulalamika kwamba mwingine daima anarudia maneno yale yale… lakini ni vema kuyasikiliza. Na baada ya kumaliza kuzungumza, ndipo uweke neno lako lakini kwanza ni kuyasikiliza yote”, ameshauri Papa Francisko.

Hali hiyo hiyo pia inahitajika kwa Bwana. Papa Francisko ameomba  kuongeza maombi mengi lakini ni lazima kufanya vizuri awali ya yote kumpatia usikivu. Yesu mwenyewe anaomba. Katika Injili, walipoumuuliza ni amri ipi iliyo ya  kwanza alijibu “ sikiliza Israeli. Baadaye akaongeza  amri ya kwanza ni “Mpende Bwana Mungu wako kwa moyo wote (…) na jirani yako kama nafsi yake (rej Mk 12, 28-31). Lakini awali ya Yote anasema “ Sikiliza Israeli. Sikiliza wewe. Swali: je tutakumbuka kujiweka katika usikivu kwa Bwana?  Sisi ni wakristo lakini labda kati ya maelfu ya maneno ambayo tunasikia kila siku, hatupati hata nukta moja ya kuweza kusikiliza ndani mwetu maneno ya Injili. Yesu ni Neno. Ikiwa hatusimami na kumsikiliza, anapita mahali pengine. Mtakatifu Agostino alikuwa anasema “ Ninaogopa Bwana atakapopita”. Hofu yake ilikuwa Bwana anaweza apite bila yeye kumsikia. Lakini ikiwa tutajikita muda wetu kwa ajili ya Injili tutapata siri kwa ajili ya afya yetu ya kiroho, Papa Francisko amefafanua.

Na ndiyo tazama dawa: kila siku lazima kufanya ukimya kidogo na kusikiliza." Je ni  maneno mangapi yasiyo na maana na wakati maneno ya Mungu  ndiyo yanahitajika yawe zaidi. Daima Injili iwe mfukoni ambayo itusaidie sana. Tuhisi maneno haya yanatueleza sisi kama siku ile ya ubatizo, na  meneno yake ya Yesu: ‘Efatha’, maana yake, Funguka. Funguka masikio. Ninatamani Yesu unifungulie Neno lako, Yesu nifungulie usikivu wako, Yesu niponesha moyo wangu uliofungwa, niponeshe moyo wangu dhidi ya haraka, niponeshe moyo wangu dhidi ya ukosefu wa uvumilivu", amesisitiza Papa. Kwa kuhitimisha amesema "Naye Bikira Maria aliyejifungulia usikivu wa Neno ambalo lilifanyika mwili, atusaidie kila siku kusikiliza Mwanae katika Injili na kwa kaka na dada kwa moyo wa upole, uvumilivu na umakini".

Mara baada ya tafakari Papa Francisko amekumbusha matukio mbali mbali yaliyotekea wikii hii na mengine yatakayotokea kwa upande wake kama vile: amesali kwa ajili ya watu wa Afghanistan ambao wanaendelea na mgogoro, ameombea watu wa Marekani waliokumbwa na dhoruba kali ambayo imesababisha madhara makubwa; amekumbusha pia hija yake ya kitume jijini Budapest  na nchini Slovakia inayotarajiwa kuanza tarehe 11 hadi 17 Septemba 2021. Wakati huo huo, amekumbusha aliyetangazwa mwenyeheri mpya anchini Argentina Ndugu Mamerto Esquiu na Askofu wa Argentina. Hakusahau kutaja siku kuu ya Mtakatifu Mama Teresa wa Kalkuta na kumalizia kwa salamu kwa mahujaji wote na waamini waliofika kutoka pande mbali mbali katika uwanja wa Mtakatifu Petro na kuwatakia Dominika njema na wasisahau kusali kwa ajili yake.

TAFAKARI YA PAPA DOMINIKA
05 September 2021, 13:04