Baba Mtakatifu Francisko katika Barua yake Binafsi "Motu Proprio" "Antiquum ministerium" yaani "Huduma Kale" anatangaza rasmi kwamba, Ukatekista ni Huduma ndani ya Kanisa, huduma kale! Baba Mtakatifu Francisko katika Barua yake Binafsi "Motu Proprio" "Antiquum ministerium" yaani "Huduma Kale" anatangaza rasmi kwamba, Ukatekista ni Huduma ndani ya Kanisa, huduma kale! 

Papa: Antiquum ministerium: Huduma Kale: Makatekista!

Papa Francisko tarehe 11 Mei 2021, Mama Kanisa anapoadhimisha kumbukumbu ya Mtakatifu Yohane wa Avila (1499 – 1569) Padre na Mwalimu wa Kanisa, anatarajia kutangaza rasmi kwamba, Ukatekista sasa ni Huduma ndani ya Kanisa Katoliki, huduma ambayo imekuwepo tangu kale. “Antiquum ministerium”. Haya yamo kwenye barua yake binafsi, “Motu Proprio ya tarehe 11 Mei 2021.

Na Padre Richard A. Mjigwa, C.PP.S.  – Vatican.

Kwa Barua binafsi ya Baba Mtakatifu Francisko “Motu Proprio” “Spiritus Domini” yaani “Roho wa Bwana”: Utume wa Waamini Walei kutoka katika Ubatizo”, kuanzia sasa wanawake wenye sifa wanaweza kupewa daraja la Usomaji na utumishi Altareni. Hii ina maana kwamba, wanaweza kusaidia kugawa Ekaristi Takatifu wakati wa Ibada ya Misa takatifu. Madaraja haya yatatolewa katika Ibada. Uamuzi huu ni sehemu ya utekelezaji wa mapendekezo yaliyotolewa na Mababa wa Sinodi na Mabaraza ya Maaskofu Katoliki kutoka sehemu mbalimbali za dunia. Utume huu wa waamini walei unapata chimbuko lake katika Sakramenti ya Ubatizo na unatofautiana na huduma ya Daraja Takatifu ya Upadre.

Baba Mtakatifu Francisko aliambatanisha na Barua aliyomwandikia Kardinali Luis Francisco Ladaria Ferrer, Mwenyekiti wa Baraza la Kipapa la Mafundisho Tanzu ya Kanisa kuhusu sababu msingi za kitaalimungu zilizopelekea hadi akafikia uamuzi huu. Baba Mtakatifu anasema, Roho Mtakatifu, mahusiano ya upendo katika Fumbo la Utatu Mtakatifu hujenga ushirikiano na uelewano wa watu wa Mungu. Ni katika mwendelezo huu, Baba Mtakatifu Francisko, Jumanne tarehe 11 Mei 2021, Mama Kanisa anapoadhimisha kumbukumbu ya Mtakatifu Yohane wa Avila (1499 – 1569) Padre na Mwalimu wa Kanisa, anatarajia kutangaza rasmi kwamba, Ukatekista sasa ni Huduma ndani ya Kanisa Katoliki, huduma ambayo imekuwepo tangu kale. “Antiquum ministerium” yaani hii ni “Huduma kale”. Haya yamo kwenye barua yake binafsi, “Motu Proprio ya tarehe 11 Mei 2021.

Mtakatifu Yohane wa Avila, ni Padre na Mwalimu wa Kanisa aliyekazia zaidi malezi na majiundo ya waamini walei sanjari na mihimili ya uinjilishaji. Alitaka kuona waamini wanafahamu vyema Maandiko Matakatifu na Mafundisho ya Kanisa. Ni katika muktadha huu, Mtakatifu Yohane wa Avila, akatunga Katekisimu ya Watu wazima na watoto. Hii ni Katekisimu iliyosheheni mafundisho ya Kikristo! Lengo la Baba Mtakatifu ni kuwahusisha zaidi Makatekista katika mchakato wa uinjilishaji kadiri ya mafundisho ya Mababa wa Mtaguso Mkuu wa Pili wa Vatican.

Makatekista ni watu ambao kwa miaka mingi wamejisadaka kwa ajili ya kufundisha Katekesi, ili kuwasaidia waamini kukutana na Kristo Yesu katika: Neno, Sakramenti na Huduma mbalimbali zinazotolewa na Mama Kanisa kwa watu wa Mungu kama kielelezo makini cha imani tendaji. Huduma ya Katekista ndani ya Kanisa inapaswa kupewa mwelekeo wa Kijumuiya, kwa kujali na kuthamini karama na tunu mbalimbali ambazo Roho Mtakatifu amewakirimia watu wa Mungu kwa ajili ya mchakato wa uinjilishaji wa kina unaogusa mahitaji ya mtu mzima: kiroho na kimwili. Hiki ni kipindi cha kujenga na kudumisha ari na mwamko wa kimisionari, kwa kutangaza na kushuhudia Habari Njema ya Wokovu!

Papa Huduma Kale
10 May 2021, 16:11