Tarehe Mosi Septemba 2019, Baba Mtakatifu Francisko ametoa ujumbe wake wa Siku ya Kuombea Utunzaji Bora wa Mazingira! Tarehe Mosi Septemba 2019, Baba Mtakatifu Francisko ametoa ujumbe wake wa Siku ya Kuombea Utunzaji Bora wa Mazingira! 

Papa:Siku ya Kuombea Utunzaji wa Viumbe:Tuchague maisha bila kuchelewa!

Kazi ya uumbaji ni mtandao wa kijamii wa Mungu,kila mmoja asuke nyuzi za mtandao wa maisha.Tuchague maisha bila kuchelewa zaidi,kwa maana kuna dharura ambazo haziwezi kusubiriwa.Ndiyo wito wa Baba Mtakatifu Francisko kwa Siku ya Kuombea Utunzaji Bora wa Mazingira ambayo kilele chake ni tarehe Mosi Septemba.Maadhimisho haya yataendelea hadi tarehe 4 Oktoba wakati wa sikukuu ya Mtakatifu Francis wa Assisi.

Na Sr. Angela Rwezaula-Vatican

Jumapili tarehe Mosi Septemba ni Siku ya Kuombea utunzaji  Bora wa Mazingira, ikiwa ni madhimisho ya mwaka wa tano tangu ilipoanzishwa na Baba Mtakatifu Francisko kunako tarehe 10 Agosti 2015. Kufuatia na tukio hili, Baba Mtakatifu ametoa ujumbe wake kwa waamini na watu wote wenye mapenzi mema kwamba: Siku ya kuombea viumbe ni siku yenye tabia ya kiekumene kwa sababu ya kuadhimishwa pamoja na Kanisa la kiorthodox. Siku hii ndiyo mwanzo wa kipindi kiitwacho cha Uumbaji kinachoanzia tarehe Mosi Septemba hadi kufikia tarehe 4 Oktoba, ambapo wakristo wote duniani wanaalikwa kusali kwa pamoja katika kuombea utunzaji wa kazi ya uumbaji yaani mazingira. “Mungu akaona kuwa ni vyema” (Mw 1,25).  Mtazamo wa Mungu tangu mwanzo wa Biblia ni wa Huruma. Kuanzia ardhi ya kukaa hadi kufikia maji ambayo yanarutubisha maisha, kuendelea katika miti ambayo inatoa matunda na wanyama ambao wanakaa katika nyumba ya pamoja, na kila kitu ni chema, machoni pa Mungu ambaye anamapatia mwanadamu kazi ya uumbaji kama zawadi yenye thamani ya kutunza.

Jibu la binadamu kuhusu zawadi ya Mungu, limegeuka kuwa dhambi

Kwa bahati mbaya jibu la binadamu juu ya zawadi hiyo imegeuka kuwa dhambi, kuanzia kujifunga na kujitegemea binafsi, uchu wa kuwa navyo na unyonyaji. Ubinafsi na upendeleo mwingi, katika kazi ya uumbaji umeweza kuwa uwanja wa mashindano na mapigano, badala ya kuwa sehemu ya kukutana na kushirikishana. Kwa maana hiyo wameweka mazingira hatarini na jambo ambalo ni jema machoni pa Mungu limegeuka kuwa la kunyonywa katika mikono ya binadamu. Kuharibiwa kumeongezeka kwa miaka kumi ya mwisho kama vile  uchafuzi unaoendelea, matumizi mabaya ya uchimbaji wa mafuta, kunyonywa kwa kilimo, uchomaji hovyo wa misitu na  kuongezeka kwa joto duniani kwa ngazi ya kutisha!

Matukio ya mara kwa mara ya mabadiliko ya tabianchi na ukame

Baba Mtakatifu amesema, kuna kuongezeka kwa kina kwa matukio mara  kwa mara ya mabadiliko ya tabianchi na ukame wa ardhi unaosababisha majaribu magumu na zaidi kwa walioathirika kati yetu. Kuyeyuka kwa barafu, hukosefu wa maji katika vyanzo vya maji na ongezeko la utupaji plastiki katika bahari, haya  yote ni mambo mengi ya kuleta wasiwasi, ambapo mashirika yanayo husika na dharura hizo wanaeleza bayana na kuonya bila kuchoka. Baba Mtakatifu kwa namna hiyo anaongeza kusema “Tumeunda dharura ya tabianchi ambayo inataharisha asili na maisha yetu ya pamoja”.

Tumesahau kuwa sisi ni nani, yaani sura na mfano wa Mungu

Baba Mtakatifu kuhusiana na na madhara na uharibifu amesema, katika mzizi huo tumesahau sisi ni nani, ambao ni sura na mfano wa Mungu (Mw 1,27) tunaoalikwa kuishi kama ndugu, kaka na dada katika nyumba moja. Hatukuumbwa kuishi kila mmoja kivyake na kutawala, bali sisi tulifikiriwa na kupendwa, ambacho ni chanzo  cha mtanzamo mmoja wa maisha yanayoundwa na milioni ya maisha kwa ajili ya upendo wake kutoka kwa Muumba wetu. Ni wakati wa sasa ambapo tunataka kupiga hatua ya kugundua kwa upya wito wa kuwa wana wa Mungu na ndugu kati  yetu, walinzi wa kazi ya uumbaji. Ni kipindi cha kutubu na kuwa na uongofu ili kurudi katika mizizi. Sisi ni viumbe  tuliopendelewa na Mungu na kutokana na wema wake anatualika kupenda maisha na kuishi kwa umoja tukiungana na muumba.

Ni mwaliko wa nguvu katika kusali kipindi hiki

Baba Mtakatifu Francisko amesisitiza, kwamba, ni mwaliko wa nguvu kwa waamini ili kukita nguvu zao zote katika sala kwa kipindi hiki, ambacho kinatoa fursa zilizo anzishwa kwa mantiki ya kiekumene na kujiunda  kwa dhati kama kipindi cha uumbaji. Ni kipindi zaidi cha kujikita katika sala na matendo ya ufadhili wa nyumba yetu ya pamoja, kinachofunguliwa kuanzia Mosi Septemba ambayo ni siku ya Kuombea utunzaji wa mazingira na kitamalizika tarehe tarehe 4 Oktoba, siku ambayo Kanisa linamkumbuka Mtakatifu Francisko wa Assisi. Ni fursa ya kuweza kuhisi kwa mara nyingine tena na  zaidi kuungana na ndugu, kaka na dada wa imani mbalimbali za kikristo. Baba Mtakatifu anamkumbuka kwa namna ya pekee waamini wa kiorthodox ambao kwa miaka 30 hivi, wamekuwa wakiadhimisha siku hii. Anasema , hii ina maana ya kuhisi kwa pamoja na kwa kina kama  wanaume na wanawake wenye mapenzi mema kwa pamoja wanaoalikwa kuhamasisha katika mantiki ya kipeo cha ekolojia ambayo inatazama kila mmoja, kuwa mlinzi wa mtandao wa maisha ambayo sisi sote tu sehemu yake.

Ni kipindi cha kusali wa ajili ya asili na kutoa shukrani kwa upendo

Hiki ni kipindi cha kusali ndani ya wingi wa asili, ambao umetolewa na bila kulazimisha kwa shukrani kwa Mungu muumba. Mtakatifu Bonaventura, ambaye ni maarufu kwa hekima ya kifransiskani, alikuwa anasema kwamba:Uumbaji ndiyo kitabu cha kwanza cha Mungu alichofungua mbele ya macho yetu, kwa sababu ya kushangazwa na utaratibu na uzuri ambao kama tunaongozwa ndani mwake, tunapata kumpenda na kumsifu Muumba. (rej.Breviloquium, II,5.11). Katika kitabu hicho, kila kiumbe kimepewa “Neno la Mungu” (Rej. Commentarius in librum Ecclesiastes, I,2). Katika ukimya na katika sala tunaweza kusikiliza sauti moja ya uumbaji, Baba Mtakatifu Francisko anasisitiza,  ambayo inatuhimiza tutoke ndani ya kujifunga kwetu ili kujitolea kwa  kugundua kuwa, sisi tumezungukwa na huruma ya Baba na tunafurahi kushirikishana zawadi tulizozipokea. Kwa maana hiyo tunaweza kusema kwamba, uumbaji, mtandao wa maisha, sehemu ya kukutana na Bwana kati yetu, ndiyo “mtandao wa kijamii wa Mungu”(Hotuba kwa viongozi  na Scout wa Ulaya, tarehe 3 Agosti 2019.  Na huo unatupelekea  kuweza kuimba kwa sauti moja ya wimbo wa sifa ya kazi ya muumbaji, kama maandiko matakatifu yanavyo fundisha: “msifuni Bwana enyi mimea yote duniani, mwimbieni sifa na mtukuzeni milele” (Dn 3,54).

Kutafakari juu ya mtindo wa maisha na uchaguzi watu kila siku.Hatua za kinabii

Baba Mtakatifu Francisko katika ujumbe wake anasema, hiki ni kipindi cha kutafakari juu ya mitindo yetu ya maisha na jinsi gani ya uchaguzi wetu wa kila siku, katika tendo la chakula, matumizi, usafiri, matumizi ya maji, umeme na mema mengi ya vifaa ambavyo mara nyingi havifikiriwi na vyenye madhara. Kwa walio wengi  tunatawala juu ya uumbaji, lakini anaongeza kusema: “Tuchague kubadilika, tuchukue wajibu wa kuwa na  mtindo ya maisha rahisi zaidi na heshima!  Ni wakati sasa wa kuachana na utegemezi wa mafuta na uchumbaji madini, ili kuchukua uamuzi kwa namna ya haraka  na mabadiliko katika kuelekea mtindo wa nishati safi na uchumi endelevu unaozunguka. Na tusisahau kuwasikiliza watu wa asilia, ambao hekima yao ya ulimwengu inaweza kutufundisha kuishi vizuri  kuhusu uhusiano na mazingira. Baba Mtakatifu katika ujumbe wake anasititiza kwamba, ni wakati sasa wa kuchukua hatua za kinabii! Vijana wengi wako wanapaza sauti zao duniani huku wakiomba kuwa na  uchaguzi wenye ujasiri. Wamekatishwa tamaa na ahadi nyinyi ambazo hazitimizwi  na jitihada zilizo anzishwa na kuachwa kwa sababu ya maslahi binafsi na kuwekwa pembeni. Vijana wanatukumbusha kuwa, ardhi siyo wema wa kupoteza, bali ni urithi wa kuridhirisha, wa kutegemea na siyo hisia tu, bali ni zoezi ambalo linatakiwa lijikite katika matendo ya kweli leo hii. Kwa upande wao, lazima kuwapatia majibu ya kweli na siyo majibu matupu na wala ya udanganyifu, Baba Mtakatifu amehimiza!

Wito kwa wahusika wa sera za kisiasa na raia 

Baba Mtakatifu  Francisko anatoa wito kwamba, sala zetu na miito yetu iwaandee  na kuhamasisha wale  wote wahusika wa kisiasa na raia. Anakumbuka kwa namna ya pekee, Viongozi wa Serikali ambazo kwa miezi ijayo watakutana kwa ajili ya jitihada za kutoa maamuzi juu ya mtazamo wa  sayari ya maisha, badala ya kukutana na kifo. Kwa maana hiyo, akilini mwake anakumbuka maneno ambayo Musa aliwatangazia watu kama ushuhuda wa urithi kiroho kabla ya kuingia katika Nchi ya ahadi kwamba: “basi chagua uzima, ili uwe hai, wewe na uzao wako; (Kum 30,19). Haya anasema Baba Mtakatifu Francisko, ni maneno ya kinabii ambayo tunaweza kuyachukua sisi na kwa ajili ya  hali ya ardhi yetu. Tuchague maisha!  Tuseme “hapana”  juu ya kuwa na uchu  wa utumiaji na kwa madai ya nguvu, njia za kifo; tuchukue njia zinazo tazama upeo wa mbele zaidi, zilizo tengenezwa kwa  kujikatalia na kuwajibika leo hii, kwa kuhakikisha juu ya matarajio ya maisha kesho. Tusiangukie katika maoni mabaya hasa ya kuwa na vipato rahisi, bali  tufikirie kesho kwa ajili ya wote! Baba Mtatakati amebainisha.

Hatimaye katika ujumbe wake Baba Mkatifu kuhusu mkutano wa Umoja wa Mataifa

Baba Mtakatifu Francisko hatimaye anasema kwa maana hiyo, upo umuhimu maalum wa Mkutano wa wakuu wa Umoja wa Mataifa ujao, kuhusu tabianchi, mahali ambapo, serikali zitatakiwa kuwa na zoezi la kuonesha utashi kisiasa, katika sera ya kuharakisha hatua za kufikia nishati safi ili kukidhi tamaa ya kimataifa katika kupunguza joto kwa zaidi ya 1.5C, katika mtazamo wa  kabla ya viwanda, sambamba na malengo ya Mkataba wa Paris. Kadhalika Baba Mtakatifu Francisko katika ujumbe huo, anaonesha kwamba mwezi Oktoba kuna suala la Sinodi inayotazama Amazonia na ambayo iko hatarini , na ndiyo kitakuwa kiini cha Sinodi Maalum ya Maaskofu.  Anawaalika  waamini wote na wenye mapenzi mema kupokea fursa hizi kwa ajili ya kujibu kilio cha maskini na Ardhi! Kila mwamini mkristo na  mjumbe wa familia ya kibinadamu, anaweza kutoa mchango wa kusuka kama vile  uzi mwembamba, japokuwa ni mmoja, lakini unahitajika katika  kukidhi matendo ya maisha ambayo yanakumbatia wote!  Lazima kuhisi kuwa,  wote ni wahusika kulichukulia suala hili ndani ya moyo na kwa sala, katika jitihada za utunzaji wa mazingira. “Mungu mpenda maisha” (Hek 11,26) atupatie ujasiri wa kutenda mema bila kungojea wengine waanze na bila kuchelewa sana.( Ujumbe kwa lugha mbalimbali: “Mungu mpenda maisha” (Hek 11,26) atupatie ujasiri wa kutenda mema bila kungojea wengine waanze na bila kuchelewa sana.(Ujumbe kwa lugha mbalimbali: http://press.vatican.va/content/salastampa/it/bollettino/pubblico/2019/09/01/0647/01341.html#ITA

01 September 2019, 13:13