Papa Francisko asikitishwa na maafa huko Nepal!
Na Padre Richard A. Mjigwa, C.PP.S. – Vatican.
Baba Mtakatifu Francisko katika ujumbe ulioandikwa kwa niaba yake na Kardinali Pietro Parolin, Katibu mkuu wa Vatican kwenda kwa viongozi wa Kanisa na serikali nchini Nepal, anapenda kuungana na wale wote walioguswa na kutikiswa na madhara makubwa ya dhoruba iliyotokea, Jumapili, tarehe 31 Machi 2019 na kupelekea watu zaidi ya 31 kupoteza maisha na wengine 400 kupata majeraha makubwa, Kusini mwa Mkoa wa Kathmandu, nchini Nepal.
Baba Mtakatifu anapenda kuonesha mshikamano wake wa upendo kwa wale wote wanaolia na kuwaombolezea ndugu zao waliofariki dunia na bila kuwasahau waliojeruhiwa vibaya! Baba Mtakatifu anapenda kuwatia shime wale wote wanaoendelea kujisadaka kwa ajili ya huduma ya uokoaji na msaada kwa waathirika. Wote hawa anawaombea baraka na faraja, nguvu na uponyaji!