Papa Francisko Biashara ya binadamu inadhalilisha utu na heshima yake!
Na Padre Richard A. Mjigwa, C.PP.S. – Vatican.
Baba Mtakatifu Francisko mara baada ya Sala ya Malaika wa Bwana, Jumapili tarehe 29 Julai 2018 kwenye Uwanja wa Kanisa kuu la Mtakatifu Petro mjini Vatican ameyaelekeza mawazo yake katika maadhimisho ya Siku ya Kupambana na Biashara ya Binadamu, ambayo inaadhimishwa Jumatatu, tarehe 30 Julai 2018. Baba Mtakatifu anasikitika kusema kwamba, hii ni saratani inayowatumbukiza watu wengi katika biashara ya binadamu na utumwa mamboleo hata hapa mjini Roma. Hawa ni watu wanaohusishwa na biashara na utalii wa ngono sehemu mbali mbali za dunia, biashara ya viungo vya binadamu, kazi za suluba, wizi na ujambazi wa kulazimishwa.
Baba Mtakatifu anakaza kusema, wakati mwingine, wimbi kubwa la wakimbizi, wahamiaji na watu wasiokuwa na makazi maalum, limetumiwa ili kuwatumbukiza watu katika biashara haramu ya binadamu! Baba Mtakatifu anawaalika waamini pamoja na watu wote wenye mapenzi mema, kusimama kidete, kupambana na vitendo hivi vinavyodhalilisha utu na heshima ya binadamu.