2021.08.19 Siku ya Kimataifa ya Wahudumu wa Kibinadamu 2021.08.19 Siku ya Kimataifa ya Wahudumu wa Kibinadamu 

Siku ya wahudumu wa kibinadamu:Wito wa Caritas kuwa inahitajika ekolojia fungamani

Katika fursa ya kuadhimisha Siku ya Wahudumu Kibinadamu ulimwenguni, tarehe 19 Agosti,Caritas itarnationalis inasema ekolojia fungamani ndiyo njia pekee kwa ajili ya kudhibiti mgogoro wa tabianchi.Vile vile Caritas inatoa wito wa nguvu kwa ajili ya kipeo cha Aghanistan na mgogoro wa Lebanon.

Na Sr. Angela Rwezaula – Vatican.

Wito kwa ajili ya mzozo wa nchi ya Afghanistan na Lebanon, janga la Uviko 19, kuathirika kwa mazingira, kuongezeka kwa kiwango cha bahari, ukame, mafuriko, moto kuharibu misitu katika kanda mbali mbali za sayari na sasa inaongezea mgogoro wa Afghanistan, Lebanon na tetemeko la Haiti. Ni vyanzo vingi vya dharura za kibinadamu ambazo zimeundwa kutokana na matokeo ya asilia au ya mkono wa binadamu na ambayo kwa sasa yanawakumba hasa Nchi zaidi zilizo maskini zaidi ulimwenguni.  Dharura hizi kwa hakika zinathibitisha kuwa ekolojia fungamani  ya kibinadamu iliyohamasishwa na Papa Francisko ndiyo suluhisho pekee.

Umwagaji wa takataka za kila aina kama vile plastiki zinaharibu mazingira na hali ya hewa
Umwagaji wa takataka za kila aina kama vile plastiki zinaharibu mazingira na hali ya hewa

Ni uthibitisho uliotolewa kwa maandishi na Caritas Internationalis katika fursa ya maadhimisho ya Siku ya Kimataifa ya wahuduma wa kibinadamu ambayo huadhimishwa kila mwaka ifikapo tarehe 19 Agosti. Kiungo hiki  Katoliki ambacho kinaunganisha mashirika 162 ya upendo na hisani ambayo yanafanya kazi zake kwa nchi 200 kinatoa ushauri kwa maana hiyo kwa waamuzi wa kisiasa ili kupiga hatua za kijasiri, kwa maana bila utashi wa kisiasa wenye msimamo thabiti, maisha ya kibinadamu yako hatarini na mahali ambapo inateseka sehemu ya ubinadamu inateseka familia nzima ya kibinadamu inateseka yote.

Maombi matano kwa maana hiyo yameombwa na Caritas Internationalis. Awali ya yote Viongozi wa ulimwengu wanaombwa kutenga fedha za kutosha ili jumuiya mahalia ziweze kufanya shughuli za maendeleo ya jumuiya zao za kilimo na zisizo za kilimo, ambazo zinawahakikishia njia ya kujikimu na usalama wa chakula. Pili, jumuiya nzima mahalia, lazima zihusike katika hatua za kibinadamu, zikiwaachia nafasi ya kipaumbele katika usimamizi wa majanga. Caritas Internationalis inasisitiza hitaji la kuhamasisha serikali za mitaa kuanzisha ushirikiano wa karibu na asasi za kiraia na vikundi vya kidini katika eneo hilo ili kushughulikia kwa ufanisi zaidi matokeo ya mabadiliko ya tabianchi. Ombi la nne linahusu upatikanaji wa huduma msingi za afya kwa walio hatarini zaidi, pamoja na chanjo ya magonjwa mabaya.

Kupata chanjo kwa wote katika kujikinga na maradhi hasa hili la Uviko
Kupata chanjo kwa wote katika kujikinga na maradhi hasa hili la Uviko

Caitas Internationalis kwa kuangaziwa na kauli mbiu ya mwaka huu ambayo imejikita katika ‘mgogoro wa mabadiliko ya tabianchi’ ambao unatishia kusambaratisha nyumba, uwezo wa watu kuishi na maisha yao miongoni mwa watu maskini kabisa duniani, hatimaye kwa viongozi wa kisiasa wanaombwa kujitoa kukuza sera za ulimwengu za uchumi na viwanda zenye lengo la kupunguza athari kwa ongezeko la joto duniani na uharibifu wa mifumo ya ekolojia. Caritas aidha inahimiza Cop-26 itakayo fanyika huko Glasgow, kulichukulia suala hilo kama kipaumbele cha dharura kwa kupendekeza suluhisho halisi na za kutosha na kutenga rasilimali za kutosha na njia za kuzifanikisha hili. Akirejea suala la hivi karibuni katika hali, nchini Afghanistan na Lebanon, Caritas Internationalis inasisitiza hitaji la kuhakikisha usalama wa idadi ya watu wa Afghanistan na usambazaji wa mahitaji  msingi kwa watu wa Lebanon.

Mhudumu wa Kibinadamu akiwasaidia  watoto
Mhudumu wa Kibinadamu akiwasaidia watoto

Ofisi ya Umoja wa Mataifa ya kuratibu misaada ya kibinadamu na masula ya dharura OCHA imetoa shukrani zake kwa wahudumu wa kibinadamu popote  walipo katika kuokoa maisha. Na kupitia ujumbe wake kwa ajili ya siku ya kimataifa ya Wahudumu wa kibinadamu, naye Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa, Bwana Antonio Guterres amesema  duniani kote wahudumu wa kibinadamu wanakabiliwa na ongezeko la vitisho, na  katika miaka 20 iliyopita matukio ya kupigwa risasi, kutekwa na mashambulizi mengine dhidi ya mashirika ya kibinadamu yameongezeka mara 10.  Ameongeza kuwa mwaka huu pekee, wahudumu wa masuala ya kibinadamu 72 wameuawa katika maeneo ya mizozo, na kwa mantiki hiyo amesisitiza kuwa: “Katika siku hii ya wahudumu wa masuala ya kibinadamu tunawaenzi wahudumu hao kila kona ya dunia na kuahidi kufanya kila liwezekanalo kuwalinda wao na kazi yao muhimu.”

Watoto wakicheza katika mazingira machafu
Watoto wakicheza katika mazingira machafu

Lengo na kampeni kubwa ya siku ya mwaka huu imejikita katika mada ya ‘mgogoro wa mabadiliko ya tabianchi’ ambao unatishia kusambaratisha nyumba, uwezo wa watu kuishi na maisha yao miongoni mwa watu maskini kabisa duniani.  Katibu mkuu ametamka kila mtu kujiunga na kampeni hiyo TheHumanRace ili kusaidia kufikisha ujumbe kwa viongozi wa dunia kwamba hatua dhidi ya mabadiliko ya tabianchi hazitomwacha yeyote nyuma.  Kwa maana hiyo Bwana Guterres amehimiza ulimwengu kuwa “Dharura ya mabadiliko ya tabianchi ni mbio tunazopoteza. Lakini ni mbio tunazoziweza na lazima tushinde. Hebu tukaze buti zetu zetu za kukimbilia, jiunge na Kampeni ya TheHumanRace, na kwa pamoja, hakikisha kila mtu anakamilisha mbio hizo.” Tukumbuke wahudumu wa kibinadamu ni wanawake na wanaume mashujaa ambao hufikisha msaada wa kuokoa maisha kama malazi, huduma muhimu za afya, chakula, maji na huduma za usafi kwa watu wasiojiweza na walio hatarini, hivyo wanastahili kuheshimiwa na kupongezwa.

19 August 2021, 14:20